Tuesday 16 June 2015

Leo kidogo, nilikuwa nimejipumzisha ndani ya chumba changu, nilichopanga uku kwa walalahoi wenzangu. Kausingizi kakanipitia kwa mbaaali! Kama unavyojuwa jinsi usingizi ulivyo mtamu kuliko kulala.

Mara nikashtushwa na mazungumzo nje ya dirisha langu. Nikawa najiuliza kuna nini na nini kinazungumzwa? Nikatega sikio, EEh! Kumbe wapangaji wenzangu walikuwa wakimzungumzia mmoja wa wapangaji ambaye amehamia hivi karibuni, akiwa yeye na mkewe.

Nikamsikia mdada mmoja akisema: Mmmh! Menzangu, umemuona huyo mumewe, alivyo kibushuti, sasa sijui uwa anambeba au...! Maana wakitembea kama vile anampeleka mwanawe shule ya vidudu!

Akamalizia na kicheko: Eeeeee! Cheko lako ilooo jilani!

Akadakia na mwenzake: Na huyo mke mwenyewe umemuona jinsi alivyo, yaani kama sanamu la michelini, loh! Hivi dawa zote hizo za kuondoa unene hazioni, yaani akitembea ardhi yote inatetemeka, loh! Mwanamke shepu babu eeh!

Sikuweza tena kuwavumilia, nikanyanyuka zangu, nikatoka na kuwakemea kuwa wanachokifanya sicho. Walicho nijibu, ilibidi nirudi ndani nitafakari zaidi, maana siwezi hata kukiandika hapa.

Kufika ndani mawazo yakawa yananipitia nikawa najiuliza, hivi Nani amewaambia kuwa ndani ya ndoa kuna Mashindano ya Miss wedi, Hivi kwenye ndoa kuna rifarii au jaji. Si ni wana ndoa wenyewe jinsi walivyochaguwana?

Kama mtu anaonekana kuwa kachagua ''kituko" Si mumuwache na kituko chake! Kwa sababu yeye ndio anayejuwa kwanini kachagua kile Kituko na kinamfaa kuwa Mke/Mume.

Wengi wetu tunafikiria kuwa Mke/Mume ni Muonekano wa nje au maumbile. Wanawake wengi wanafikiria mume kuwa na sijui siksi paki au kuwa na bonge la msuri ndio kapatia.

Na hata wanaume Wengi wanafikiria kuwa Mke kuwa na Makalio makubwa au nyonga nyembamba au mapaja manene ndio kupatia, sasa sijui nani kawaambia kuwa makalio au nyonga ndio yanaendesha ndoa.

Kwa taarifa yenu  hayo yote hayaendeshi ndoa, ndoa ni maelewano kati ya watu wawili. Nyie wengine hayawahusu.

Na nyie Wanawake mnaoshangaa Mwanamke anapoamua kuolewa na 'sura mbaya' na kuanza kumsimanga Shosti nae ndo nini kuolewa na mtu mfupi kama kama kashata. Nasema mkome kabisa na hizo tabia zenu tena Muache. Mwenyewe anajuwa Kashata yake kama ataitengenezea Kahawa au ataila hivi hivi na ndoa itakuwa tamu na maisha yataendelea.

Nyie Wanawake nyie, mwenye akili huwa hawachagui Misuli na siksi paki wala sura nzuri, wanachagua mtu mwenye mapenzi ya kweli na mwenye kujali, anaweza kuwa maskini lakini ndani ya moyo wake kuna Utajiri wa mapenzi ambao nyie manungaembe na magube-gube hamuwezi kuyaona ila yeye ameuona na anajifaidia ile roho inapenda.

Nyie kaeni hapo hapo tu mkisubiri mahandisamu boi ambao kazi kuvaa serawili chini ya matako na wanawake ambao kazi kila kukicha kwenye kioo.

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!