Thursday 18 August 2016

Hoja iliyo kubwa kabisa tunayoweza kuitoa kwamba kwa nini Uislam ni (Dini) mfumo sahihi wa maisha na si Ukomunisti, Ujamaa, ubepari au Mifumo mingine yenye kuamini uwepo wa MwenyeziMungu kama vile Uyahudi, Ukristo, Uhindu, na Ubudha!?

Hili ndilo swali la maana na la halali kabisa kila kipengele cha itikadi ya Kiislamu kinakubali utafiti na hoja. Hakuna mfumo mwingine wa maisha unaokubali misingi ya imani yake ihojiwe.

Mfumo sahihi wa Maisha unaowastahiki walimwengu wote wa nyakati zote haunabudi kuhakikisha kuwa kila mmoja anapata haki zake sawa za kibinafsi na kijamii bila ya upendeleo au ubaguzi wa aina yoyote.

Uislamu ndio mfumo sahihi wa maisha ya mwanadamu na ndio dini ya Mweyezi Mungu (s.w.) aliyemuumba Mwanaadamu kwa lengo maalum. Ni Muumba pekee anayejua mahitaji halisi ya Mwanaadamu na ni yeye pekee anayejua njia sahihi ya kumfikisha mwanaadamu kwenye lengo lake la maisha.

Mwenyezi Mungu anatuambia kwenye Qur'an:

Bila ya shaka Dini mbele ya MwenyeziMungu ni Uislamu. Na walio pewa Kitabu hawakukhitalifiana ila baada ya kuwajia ujuzi, kwa sababu ya uhasidi ulio kuwa baina yao. Na anaye zikataa Ishara za Mwenyezi Mungu basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu.
Qur'an Surat Al I'Mran 03:19

UTAIFA, UKABILA, DINI AU RANGI

Dini, kabila, taifa, rangi au hadhi havitazingatiwa na mfumo (dini) sahihi katika kumpatia kila mtu haki yake anayostahiki. Mfumo sahihi hauna budi kuwa na utaratibu wa kusimamia na kuchunga haki ya kila mtu na kuwahukumu na kuwaadhibi wakosa kwa usawa ili kuiweka jamii kwenye furaha na amani ya kweli katika maisha. Mfumo (Dini) sahihi haunabudu kuwa na sharia ambazo zinamgusa kila mtu kwa usawa.

Mwenyezi Mungu anatuambia kwenye Qur'an:

Na hakika tumewatukuza wanaadamu, na tumewapa vya kupanda nchi kavu na baharini, na tumewaruzuku vitu vizuri vizuri, na tumewafadhilisha kwa fadhila kubwa kuliko wengi miongoni mwa tulio waumba.
Qur'an Surat Al-Isra 17:70

Enyi watu! Hakika Sisi tumekuumbeni kutokana na mwanamume na mwanamke. Na tumekujaalieni kuwa ni mataifa na makabila ili mjuane. Hakika aliye mtukufu zaidi kati yenu kwa Mwenyezi Mungu ni huyo aliye mchamngu zaidi katika nyinyi. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua, Mwenye khabari.
Qur'an Surat Al-Hujurat 49:13

Mwanaadamu pamoja na kutunukiwa vipawa vya akili na utambuzi wa hali ya juu, bado fikra zake na uamuzi wake unaathiriwa sana na matashi ya nafsi yake. Akipenda kitu hupitisha uamuzi wa upendeleo pasina haki. Na akichukia kitu hupitisha uamuzi wa uonevu. Hivyo kutokana na udhaifu huu ukichukua jukumu la kuunda mfumo sahihi (dini) ataweka utaratibu utakao mpendelea yeye na wale walio karibu naye na kuwakandamiza wale wasio na uhusiano wa karibu naye.

Kwa mfano, Mtakatifu Thomas Aquinas, Mwanatheolojia aliyekuwa na ushawishi mkubwa mno miongoni mwa wanatheolojia wa Kikristo wa Kidominika, anazuia matumizi ya akili pale anapoendea misingi ya imani ya Kikristo kisha anajaribu kuhalalisha imani hiyo.

Hivyo kuhoji “Kwa nini Ukristo?” si swali halali lakini, Allah analikaribisha swali “Kwa nini Uislamu” Hakuna dini nyingine yenye ujasiri wa kutosha kuitoa imani yake kama changamoto ya akili ya binadamu

Uislamu ni mfumo wa kimantiki ambao sio tu unaruhusu maswali bali pia unaipa hadhi na heshima elimu kwa kiwango cha juu.

Hakuna mfumo au dini nyingine ambayo imetukuza elimu na jitihada za kuitafuta kama vile ambavyo Uislamu umefanya. Kwa kweli, kwa mara ya kwanza, katika Historia ya mwanadamu, kitabu cha dini kiliwataka watu wahoji umbile la Ulimwengu na kusema ndani ya (Ulimwengu) kuna ishara kwa watu wenye elimu. Kila jambo katika Uislamu linataka kutafitiwa kiakili.

Uislamu umekataza kuhoji jambo moja tu na hili ni jambo ambalo akili haiwezi kushughulika nalo. Hata hivyo, hii haina maana hilo ni jambo linalopingana na akili. Jambo pekee ambalo Uislamu umesema haliko ndani ya uwezo wa kiakili wa binadamu ni dhati ya Allah ambayo daima itaepukana na mtu kwani yeye yuko nje ya upeo.

Hata hivyo mpango wake, Lengo Lake, kazi yake makusudio yake na taathira zake vyote vyaweza kutambulika. Hata vipengele vya ibada katika Uislamu vyaweza kutazamwa kiakili. Kwa mfano kuna ufafanuzi wa kimantiki na kiakili kuhusiana na muda wa sala, idadi ya rakaa katika sala, na hata kwa nini tuvipindishe vidole vyetu vya miguu tunaposali. Hapana shaka, Muislamu wakati wote atazingatia kuwa jawabu alipatalo kutokana na uchunguzi wake wa kiakili si kamilifu.

Haliwezi kukubalika kwa hakika kuwa ndilo linalobainisha mambo kwa ujumla wake. Laweza kuwa potofu na pungufu. Hata hivyo, Uislamu unawahimiza wafuasi wake kuhoji “Kwa nini Uislamu?”Uislamu ni dini ya kiakili na kihistoria. Hakuna mambo ya siri wala mambo ya kutatanisha ambayo hayawezi kueleweka kwa mtu wa kawaida

MFUMO SAHIHI WA UISLAMU HAUWEKI VIKWAZO VYA KIAKILI.

Uislamu hauzushi madai ya kuitanza akili. Uislamu haumwelezi mtu kile ambacho akili haiwezi kukielewa. Mtu yeyote anaweza kuelewa Uislamu kwani ni dini ya Ulimwengu mzima. Lakini dini zingine kama vile Uhindu, kwa mfano, inahalalisha ushirikina kwa watu wenye elimu ndogo inasema si watu wote wanaweza kuelewa dini ya juu ya Brahman

KULAZIMISHANA
Uislamu haushurutishi mtu kuchagua dini miongoni mwa dini mbalimbali kwani umejumuisha mafundisho ya msingi ya dini zote katika ujumbe wake wa Ulimwengu mzima.

Mtazamo wa Uislamu ni kuwa, kwa kila umma. Allah kampeleka Mtume na kwamba katika dini au itikadi yao mpya, lazima zimekuwemo chembechembe za ukweli kutoka katika mafundisho halisi ya dini ya asili [Diin ul –Fitra] au kwa maneno mengine ni Uislamu.

Uislamu unayaona majadiliano baina ya dini ni majadiliano ya ndani si majadiliano na watu wa nje kwa sababu, kwa mawanda yake, wanadamu wote ni ndugu wa dini moja ya Ulimwengu. Kwa hiyo, tofauti zilizopo baina ya Uislamu na dini nyinginezo zinachukuliwa kama ni tofauti za ndani.

Bila shaka Uislamu unanakosoa imani zingine kama vile wayahudi na Wakristo ambao wameipotosha imani yao. Hata hivyo ukosoaji huo unazingatia ukweli kuwa wametoka katika mafundisho ya asili ya dini yao. Hivyo basi, Uislamu ulikuwa dini ya kwanza duniani kutaka uhakiki wa vitabu vya dini. Muislamu anasema, kuziambia dini nyingine, tuvitazame pamoja vitabu vitakatifu vya dini zetu na tulinganishe maudhui yake na mafundisho ya asili ya dini zetu na tuone ni kwa kiasi gani tumefuata au kuyaacha mafundisho haya ya asili.

Hivyo basi, Muislamu asizishambulie dini nyingine kwa matusi na kejeri. Hata hivyo kwa mhindu, kama hakuzaliwa India basi hajatakasika, kwa Myahudi sheria takatifu inawahusu wao tu na kwa Mkristo, hakuna uwokovu nje ya kanisa. Hata hivyo, Uislamu unayakubali maadili ya Yesu na mafundisho yake, unakubali dhana ya dini ya kihindu ya kumkomboa binadamu kutoka katika Ulahidi, pamoja na maadili na utangamano katika jamii ya wanadamu yanayopatikana katika itikadi ya Wakonfyushasi.

Mwenyezi Mungu anatuambia kwenye Qur'an:

Hapana kulazimisha katika Dini. Kwani Uwongofu umekwisha pambanuka na upotofu. Basi anaye mkataa Shet'ani na akamuamini Mwenyezi Mungu bila ya shaka amekamata kishikio madhubuti, kisicho vunjika. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia, Mwenye kujua.
Qur'an Sura Al- Baqara 002:256

UVUMILIVU KWA IMANI ZINGINE

Uhindu, Ukomunisti, Ujamaa, Uyahudi, ubepari, Uyahudi, Ukristo, Uhindu, na Ubudha.

Uislamu unazivumilia dini nyingine na kuziona zina maana katika kuzikubali dini nyingine kuwa haki ya kisheria, Uislamu inawapokea wafuasi wake. Hakuna dini nyingine ambayo imezitendea haki sawa dini zote kama ulivyofanya Uislamu kwa zaidi ya miaka 1400.

Twajua fika kuwa, Uyahudi na Ukatoliki hazikuwa dini zenye uhalali wa kisheria enzi za Malkia Elizabeth wa kwanza. Nchini Hispania chini ya Ferdinand na Isabella, ilikuwa haramu kuwa na dini nyingine zaidi ya Ukatoliki, na Waislamu na Wayahudi walilazimika ama, kubatizwa kuhama nchi au kuuawa katika Mashariki ya kati, baadhi ya madhehebu ya Kikristo ambayo yaling’olewa kikatili na Wakristo wenzao Ulaya, yalisalimika baada ya karne 14 za utawala wa Waislamu. tawala za kisekula haziheshimu dini , zinabeza dini ama zinaamini dini yoyote tu itafaa au hakuna dini inayokubalika. Utamaduni wa kuzivumilia dini nyingine katika Uislamu unatokana na heshima kwani Uislamu unasema kuwa kila mtu ana fitra iliyopandikizwa kwa watu wote pale walipozaliwa na katika kila dini, kuna sehemu ya msingi ya dini ya maumbile.

KUZALIWA BILA DHAMBI
Uislamu umeeleza kuwa mtu huzaliwa na rekodi safi.

Mtu hakuzaliwa mwovu. Mtu ameumbwa akiwa mwema na amepewa shaksia ya kutimiza wajibu wake. Kwa mtazamo wa Uislamu, hadith ya maisha ya mwanadamu huanza baada ya kuzaliwa na si kabla yake. Uislamu haumuhesabu mtu Kama kiumbe aliyeshushwa hadhi na Mungu kwani ana silika njema na utukufu na wema

DUNIA NA AKHERA

Uislamu haugawanyi mtu, Nafsi yake, wala Maisha katika matapo mawili yaani maisha ya kidini na kimaadili na maisha ya kidunia au kimwili.

Uislamu unamuhesabu mwanadamu Kama ni kiumbe kamili. Matendo yote ya mtu na silika yake ni sehemu ya utu wake inayoambatana na matumaini, hofu, hakika, imani na yakini. Uislamu unataka yote haya yafungamane pamoja na hivyo tunaweza kusema kuwa Uislamu ndio afya bora zaidi ya akili. Uislamu unahesabu kazi ya bindamu au hata ngono kuwa ni kitendo cha ibada katika dunia hii, iwapo tendo ilo litafanywa kwa utaratibu unaoridhiwa na MwenyeziMungu.

LENGO LA MAISHA YA DUNIANI

Uislamu unayachukua maisha na makazi ya duniani kwa uzito ukielezea kuwa yana maana na lengo.

Maisha siyo mchezo, wala hayapo pale bila lengo. Kwa mawanda ya Uislamu, kila jambo lina maana kwa sababu mtazamo wa juu ya lengo la MwenyeziMungu katika maumbile unaleta maana katika maisha ya binadamu. Muislamu kamwe hachoshwi na maisha. Hakuna hofu ya maisha katika Uislamu. Muislamu huweza kuona utendaji kazi wa maumbile ya MwenyeziMungu wenye malengo mema katika kila kitu.

Muislamu anaishi katika Ulimwengu ambamo maisha Yana maana na lengo, hii maana yake ni kuwa Muislamu katu halegezi mizani ya akili yake kwa kweli maradhi ya akili ni adimu sana katika jamii ya Waislamu.

Mwenyezi Mungu anatuambia kwenye Qur'an:

Nami sikuwaumba majini na watu ila waniabudu Mimi. Na sitaki kwao riziki, wala sitaki wanilishe
Qur'an Surat Adh-Dhaariyaat 51:56-57

MAISHA NI NEHMA

Uislamu ni Ulimwengu thabiti kwa Muislamu dunia ni njema

Ni neema, imeumbwa njema ifaidiwe. Uislamu hauitazami dunia kama eneo baya, dunia haihesabiwi kuwa ni ya kishetani na hivyo ni sehemu ovu. Sio Ufalme ilioporomoshwa. dunia ndiyo ufalme pekee, Akhera sio Ufalme bali ni sehemu ya hukumu kwa matendo ya mtu wa kati wa maisha yake. Kwa Muislamu, dunia ni sehemu ya mapambo, lulu, mavazi na farasi vyote vitumiwe.

Kisichosahihi ni matumizi mabaya tu ya vitu hivyo kwa kuzingatia sheria ya maadili dunia ni nzuri na Waislamu wanatakiwa kuilima na kuifanya bustani. Kazi ya kumuunganisha mtu Kama jamii moja ni wajibu wa dini.

Hakuna dhana wala itikadi wala dini ya kulinganishwa na Uislamu katika msimamo wake thabiti wa dunia.

Waislamu wote wawe na mali na wawe matajiri. Ni shetani anayeahidi ufukara sio MwenyeziMungu. Kwa kweli Qur'an inawasema wale waliozembea na walioshindwa kuhama hawakuweza kujiinua kwa visigino vyao walipata walichostahili. Kuwa Muislamu ni kuishi na kuwa mtiifu duniani lakini usiwe juu au nje ya utii kwa MwenyeziMungu.

KUIJENGA DUNIA YAKO KWA MAISHA YA AKHERA

Katika kuijenga dunia hii na kuindesha kwa matakwa ya MwenyeziMungu, Waislamu wanaambiwa kuwa lazima wafanyekazi pamoja na sio mmoja mmoja.

Uislamu unajenga mfumo wa jamii na si mfumo wa kisufi. Mfumo wa jamii wa Kiislamu una meno, unaendeshwa kwa shariah. Uislamu unataka kujenga mfumo wa jamii wa kuamrisha mema na kuzuia maovu.

Pamoja na hivyo, kila Muislamu lazima aondoshe uovu. Ni wajibu kufanya hivyo Kama ulivyo wajibu wa kusali sala tano kwa siku. Katika Uislamu ni daraja kubwa mno la imani kwenda angani na kuleta mabadiliko Ulimwenguni kwa kuzingatia radhi za Allah.

Uislamu ni harakati kabambe za ujenzi wa jamii, sio mfumo wa kufikirika wala wa kitawa. Uislamu unasimamisha haki na jamii yenye murua. Inayoendeshwa kwa sheria. Uislamu unawahakikishia haki watu wote, Kwa kigezo cha jamii ya Madina. Katika zama hizo, haki haikuwa na bei.

Kwa karne kadhaa, chini ya utawala wa Kiislamu, raia yoyote aliyelalamika, alikuwa na hakika kuwa haki ingetendeka. Hakuna nadharia ya jamii inayoweza kuinufaisha jamii kwa kiasi kikubwa kama vile ambavyo nadharia ya Uislamu imefanya. Jamii iliyojengwa kwa msingi wa rangi, lugha au historia ni mifano ya dunia ya kinyama ambapo mbwa anamla mbwa mwingine. Mfumo wa jamii wa Kiislamu unakomesha hili na kuleta haki kwa wote. Kazi ya Muislamu ni kuleta murua na jamii hii ya kimataifa inayojengwa na Uislamu lazima ienezwe kwa Walimwengu wote na hivyo mfumo wa jamii wa Kiislamu unatakikana Ulimwenguni kote.

Mwenyezi Mungu anatuambia kwenye Qur'an:

Hakika ni juu yetu kuonyesha uwongofu. Na hakika ni yetu Sisi Akhera na dunia.
SURAT AL-LAYL 92:12-13

MFUMO WA MAISHA KWA ULIMWENGU MZIMA

Uislamu unatoa mfumo wa Jamii ambao sio tu unaonekana kuwa wa Ulimwengu mzima bali lazima uwe wa Ulimwengu mzima.

Mfumo wa Kiislamu ni mfumo wa maisha ya Ulimwengu mzima na lazima uenezwe Ulimwenguni kote, kama haukuenezwa Ulimwenguni kote basi utachukua sura ya utaifa ambao ni haramu katika Uislamu. Uislamu unajengeka kwa msingi wa maadili ambayo hayapo pale kwa ajili ya jamii fulani tu inayofuata, bali kwa wanadamu wote.

Allah ni MwenyeziMungu wa watu wote na dhana ya jamii ya Kiislamu lazima ienee Ulimwenguni kote. Je Uislamu unaikataa thamani ya utambulisho wa lugha, kabila na utamaduni wa Taifa? Hapana! Uislamu unayatambua makundi haya makabila na mataifa kwa vile yanavyostahiki kutambuliwa.

Uislamu sio tu unayavumilia bali pia unachagiza ustawi wa Jamii za makabila mbalimbali. Jamii huwa na mawanda yake mahususi juu ya maadili yanayoathiri jamii yake maadhali upo, utamaduni wa Taifa unahimizwa na Uislamu, lakini lazima ufuate shariah ambayo inaugubika Ulimwengu mzima.

Uislamu Umejenga jamii ya kiulimwengu, na ulikuwa ni Uislamu ulioanza kujenga mfumo bora wa sheria za kimataifa. Zaidi ya miaka 1400 iliyopita. Ni juzijuzi tu katika karne ya 20 ndipo Ulimwengu wa magharibi ulipoanza kupanua sheria za kimaifa. Grotious alichangia tu mawazo ya kutamani jambo hilo. Katika Ulimwengu wa magharibi sheria ya kimataifa ilikuwa ndotoni tu hadi baada ya vita ya kwanza ya dunia pale umoja wa mataifa ulipoanzishwa.

Mfumo uliopo wa sheria ya kimataifa ni duni kabisa kulinganishwa na mfumo wa Kiislamu wa sheria ya kimataifa kwa sababu chini ya mfumo wa kiislamu, sheria ya mataifa inasaidiwa na mahakama na si mahakama moja tu ya The Hague. Lakini mahakama yoyote ya shariah mahala popote pale duniani, inaweza kusikiliza shauri lolote la kimataifa ambapo pande husika sio tu mataifa bali hata watu mmojammoja. Kama tunataka kutatua matatizo ya kimataifa, lazima tutende haki kwa kila mtu chini ya sheria ya kimataifa.

Mwenyezi Mungu anatuambia kwenye Qur'an:

Amekuamrisheni Dini ile ile aliyo muusia Nuhu na tuliyo kufunulia wewe, na tuliyo wausia Ibrahim na Musa na Isa, kwamba shikeni Dini wala msifarikiane kwayo. Ni magumu kwa washirikina hayo unayo waitia. Mwenyezi Mungu humteua kwake amtakaye, na humwongoa kwake aelekeaye.
Qur'an SURAT ASH-SHUURA 42:13

UISLAMU NA MAISHA YA MWANADAMU, DUNIANI NA AKHERA

Uislamu ni dini inayotuwezesha kuishi maisha yetu kwa uwiano na maumbile, nafsi zetu na MwenyeziMungu.

Uislamu hautengenishi bali unaunganisha maisha ya mwanadamu. Hii ni kanuni ya jumla ya Uislamu kwani Uislamu unatuhakikishia furaha katika maisha haya ya dunia na yale ya Akhera.

Hivi sasa mwanadamu anawehuka na maisha ya dunia jambo ambalo limetokana na mvurugiko wa ekolojia ya maumbile kwa sababu ya uozo wa roho ya mwanadamu. Katika zama ambazo zina maendeleo ya sayansi na teknolojia ambayo hayakuwepo kabla, maisha ya dunia yamekuwa machungu na ya kuangamiza nafsi kwa sababu yamekosa mwongozo wa maadili.

Hivyo, maisha ya dunia bila dini yaweza tu kuleta na tayari yameleta maangamizi, kwa upande mwingine maisha ya dini bila dunia ni ndoto ya mchana tu. Uislamu unataka binadamu kuijenga dunia isiyo na mazingira ya wizi wala riba, kwapu kwapu na ubakaji na unasisitiza kuwa mwanadamu lazima atekeleze majukumu yake kwa kutii sheria ya maadili (shariah) kwani shughuli na mafanikio katika dunia hii ndivyo vitavyo muhakikishia mafanikio katika maisha ya Akhera.

Uislamu ndio dini pekee inayohakikisha furaha katika dunia na Akhera. Baada ya kutoa neema hii kubwa ya  MwenyeziMungu kwa wanadamu, na kingine tunachoweza kusema zaidi ya “tunasikia na tunatii na sifa njema zote ni za Allah mola wa Walimwengu

Mwenyezi Mungu anatuambia kwenye Qur'an:

Basi uelekeze uso wako sawasawa kwenye Dini - ndilo umbile la MwenyeziMungu alilo waumbia watu. Hapana mabadiliko katika uumbaji wa MwenyeziMungu. Hiyo ndiyo Dini iliyo nyooka sawa. Lakini watu wengi hawajui.
Qur'an Surat Ar-Rum 30:30

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!