Saturday 15 October 2016

Natamani Kuifunga Jela Mifupa yake

Ni Miaka 17 sasa tangia alipofariki kule jiji London, nchini Uingereza, tarehe 14 Oktoba 1999

Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, alizaliwa nchini Tanganyika kijiji cha Butiama, mkoani Mara, pembezoni mwa Ziwa Nyanza, 13 Aprili 1922 alikuwa wairiki mkuu wa kwanza na baadae kuwa rais wa kwanza wa Tanganyika na baade Tanzania. Ndiye mwasisi wa itikadi ya ujamaa na kujitegemea nchini Tanzania iliyohasisi Azimio la Arusha.

Wengi watamkumbuka kama rais, lakini kwa wale wote ambao walikuwa watu wazima na wenye fahamu zao, watamkumbuka kama mtawala na si kama kiongozi kwa sababu Kipindi cha utawala wake kilikuwa ni kipindi cha uonevu kwa raiya wengi, wengi walio athirika ni makabwela (walalahoi), na ikapelekea watu wengi kuwa waarifu wa sheria kwa sababu sheria kuhusu vyakula na bidhaa muhimu kama chakula aliviwekea sheria kali matokeo yake ni kuzuka kundi ambalo likajinufaisha kutokana na sheria hizo.

Waislamu wa Tanganyika ndio waliyompa Nyerere umbele kwa vile walikuwa na niya safi ya kutaka maendeleo ya nchi yao. Haikuwapitikia hata chembe kuwa wanachukua silaha  na kumpa adui aitumie kwa kuwauwa wenyewe.

Mara tu baada ya Nyerere kupata nguvu za kiserikali, alianza polepole kuwaondoa na kuwaweka kando viongozi wote wa Kiislamu. Alimuanza Sheikh Suleiman Takadiri kisha alimpikia jungu Cheif Said Abdalla Fundikira. Baada ya hapo aliwaandama Sheikh Said Tewa, Sheikh Zubeir Mtemvu, Sheikh Ali Mwinyi Tambwe, Bibi Titi Mohammed na wengineo wengi.

Hawa wanatosha kuwataja miongoni mwa viongozi wazalendo wa TANU na serikali yake ambao Mwalimu amewafikishia aliyowafikishia, akiamini kuwa hawa sio katika yeye; damu yao mbali na damu yake.  Hawa ni watu wa kauli moja sio kumi na moja!

Aliwabana Waislamu katika kila kipembe, kwenye nafasi mbalimbali za kiuongozi, aliwaondoa wale wote wenye mawazo na misimamo tofauti na yeye. Kuanzia uongozi wa juu serikalini mpaka kwenye ukurugenzi wa viwandani na fursa hizo akawapa wale ambao aidha wanamkubali na haswa wasiokuwa Waislamu.

Na si katika kuwaondoa tu wale Waislamu waliopigamia uhuru wa nchi ya Tanganyika kwa kuwanyima nafasi mbalimbali za kiuongozi wa nchi, kwamba nchi ilikuwa njema, la lile Jinamizi la kuwazurumu Waislamu, likapelekea yeye na serikali yake kushindwa kwenye mipango ya uchumi. Kiasi baadhi ya raiya wakaona ni bora tungeendelea kutawaliwa na Mwingereza, kuliko serikali hii iliyo hasisiwa na Mwalimu Nyerere. Kiasi cha kuona kuwa Wakoloni walikuwa bora kuliko Nyerere kwa mipango ya uchumi mizuri kwa ajili ya nchi Tanganyika na baada Tanzania.

Kipindi cha utawala wa Nyerere kwa kweli ni kipindi ambacho serikali yake ishindwa kuendesha uchumi wa nchi. Hata pale alipo amua kuanzisha Azimio la Arusha kama njia ya kujikwamua kiuchumi, bado hatukuona nafuu yoyote ile kwa mlalahoi, au makabwela. Na Kwa bahati nzuri mtoto yule aliyejulikana kwa jina la Azimio la Arusha alimfia mikononi kabla hata mzazi wake hajafariki. Hata ile siyasa ya Ujamaa na kujitegemea aliyopanga na wachumi wake uchwara, nayo ikapata ugonjwa wa kifaduro. Nayo akaishuhudia ikimfia mikononi.

Huyu mtu kama angeendelea kutawala na kwa aina ya uongozi wake basi nchi ingekuwa nyuma sana na hali mbaya sana zaidi ya Zimbabwe.

Barabarani kulikuwa na vizuizi vingi sana eti kuzuiya mali ya magendo, vipi mtu alime shamba lake la mahindi, apalilie, kisha avune na kwenye kuuza umpangie bei ya kuuza, hujui ametumia gharma gani mpaka kufikia hapo alipo. na umuwekee masharti eti hakuna kusafirisha mahindi kwenda mkoa mwingine.

Wakati wao wakitumia magari yao ya serikali ambayo hakuwa yakikaguliwa kusafirisha nafaka na bidhaa mbalimbali kutoka mkoa mmoja kwenda mkoa mwingine.

Kama kweli alikuwa muumini wa ujamaa kwanini hakutumia mabasi ya abiria kama wananchi wengine?

Kwanini ilikuwa hakuna kutumia magari binafsi na hata kuuziwa mafuta siku za weekend, yaani Jumamosi na Jumapili? Ukitaka kutumia gari lako basi lazima huwe na kibari maalumu cha kuendesha gari siku za weekend.

Nakumbuka Vita dhidi ya wahujumu Uchumi, vilianza mwanzo mwa miaka ile tuliyopata uhuru walipo taifisha viwanda na baadae majumba ya watu binafsi na miaka ile ya themanini ilikuwa ni mwendelezo tu wa kuwaibia raiya mali zao. Bila kusahau elimu ya U.P.E (Universal Primary Education kwa kiswahili ilijulikana kama Elimu ya Msingi kwa Wote), Kuwapeleka kwa nguvu watu kwenye vijiji vya ujamaa, maduka ya kaya, kutaifisha majumba, mashamba n.k.

Mambo haya ya kulazimishana ndio yakapelekea maafa makubwa kule Mkoani Shinyanga kwa kuuliwa watu kadhaa kwa tuhuma mbalimbali, wakati huo Mzee Mwinyi alikuwa waziri wa mambo ya ndani, kiasi akajiuzuru.

Nakumbuka ili kuangalia TV, mpaka kipindi cha sikukuu ya sabasaba kwenye banda la Yahaya Hussein, hii ni kwa wakazi wa jiji la DSM, Sijui uko mikoani hali ilikuwaje.

Zaidi ya hapo kila kitu kilikuwa kwa foleni, nchi nzima shule za sekondari za kuhesabika kwa vidole vya mkono. Chuo kikuu kimoja tu, kama kimejaa basi, subiri mwakani au ndio basi tena. Ilifikia wakati hata ukiwa na gari zuri basi wewe ni bepari kila kitu kwa kibali, ukiona gari aina ya Benz basi hiyo ni mali ya Ikulu, watu binafsi si rahisi kumiliki gari kama hiyo yaani hata kuvaa nguo nzuri ilikuwa ni ubepari.

Sera za ujamaa na kujitegemea kwa kweli hazikuwa sera nzuri hata kidogo. Na hata alipo ambiwa kuwa sera ni mbovu, badala ya kufuata ushauri wa kitaalam, yeye akatumia sura na maumbile yake akichanganya na uongozi wake na umahiri wa kuzungumza na kuvutia kuzitetea sera zake mbovu mpaka nchi ya Tanzania ikaangamia. Kusema kweli Mwalimu Nyerere alikuwa ni mahiri sana kwenye kutoa hotuba za kuvutia na zenye kuleta matumaini mazuri, maneno yake kwa kweli yalijaa ushawishi wa hali ya juu sana. Lakini ukija kwenye matendo ya zile hotuba nzuri hakuna hata kijiji kimoja cha maonyesho kuonyesha kuwa alifanikiwa kwenye sera zake. Hivi leo hakuna kijiji hata kimoja ambacho kinafahidika na sera zile za ujamaa na kujitegemea.

Nakumbuka aliyekuwa rais wa Kenya enzi hizo (Jomo Kenyatta) aliwahi kumwambia wanahabari kuwa "kama unataka watendaji wazuri katika sekta ya mbalimbali njoo Kenya na kama unataka wahutubiaji wazuri kila eneo liwe la siyasa, uchumi, biashara, kilimo n.k basi kwenda Tanzania kamwambie Nyerere akupe anao tele”

Ni kweli kwani ile siyasa ya ujamaa iliwaharibu sana viongozi wa taifa ili. Nyerere alitengeneza wahutubiaji wazuri si watendaji na wachapa kazi wazuri kwani karibia wote walipitia vyuo vya siyasa. Alipenda sana watu ambao kazi yao ni kuimba kwa nguvu hadi kufoka mate mdomoni kwa kusema "Zidumu fikra za mwenyekiti..." . Na wala sishangai maana hata leo na hata hao walio upande wa pili wenyewe wanajiita vyama vya upinzani wengi wanaiga tabia ya Nyerere ya kuwa wahutubiaji wazuri kuliko kuwa watendaji na wachapa kazi.

Na kwa kawaida sehemu yoyote ile maendeleo hayawezi kuja hivi hivi, lazima yafanyiwe kazi ili yapatikane. Kazi hiyo haitegemewi kufanywa na mwingine yoyote isipokuwa watawala na watawaliwa (serikali na raia).

Watawala ndio wenye jukumu la kupanga na kuratibu mipango na kutafuta njia za kusaidia utekelezaji wake ili watawaliwa waweze kufanya hayo ambayo yameshapangwa. lakini watawala wetu wale walikuwa kama wafalme, kazi yao ilikuwa kunyoosha vidole tu, bila kuonyesha mifano hai.

Mpaka leo hakuna ambaye anaweza kutuambia, ni ugonjwa gani uliotupata Watanzania, baada ya serikali ya Nyerere kutaifisha mashirika na mashamba. Tulikuwa na mashirika mengi tulio yaita ya Umma kama vile Viwanda vya nguo vya Urafiki, Sunguratex, Mwatex na kule Musoma pia kulikuwa na kiwanda cha nguo, ila sina uhakika kama bado kipo, tulikuwa na kiwanda cha kusindika nyama, Tanganyika Packers, kiwanda cha viatu kule Morogoro, na kile cha dar, pia kulikuwa na RTC na Ugawaji na mengine mengi. Yote haya leo ni marehemu na makaburi yake yashafutika kwenye ulimwengu wa Mtanzania.

Serikali ya Nyerere baada ya kutaifisha mashirika na makampuni na kukuta pesa nyingi kwenye hayo mashirika, wakaona bora kuanzisha vikundi vya sanaa vya mashirika ya umma. Vikundi ambavyo vilikuwa si vya uzalishaji mali, bali vilikuwa vinapata ruzuku kwa asilimia mia 100% kutoka kwenye hayo mashirika. Vikundi vingi kufikia mwishoni mwa miaka ya themanini 1980 vingi vilianza kudolola. Mashirika mengi yalianza kupungukiwa na uwezo wa kuviendesha vikundi hivyo kwa sababu nayo yalikuwa taabani kifedha.

Huwa najiuliza wakati  mwingine, ni vipi bidhaa kama Pamba, Katani au bidhaa kutoka kwenye mashamba au makampuni ulio dhurumu, yaani umuuzie yule yule uliye mnyang’anya, hivi inaingia akilini kweli!?

Nakumbuka ili kuangalia TV, mpaka kipindi cha sikukuu ya sabasaba kwenye banda la Yahaya Hussein, hii ni kwa wakazi wa jiji la DSM, Sijui uko mikoani hali ilikuwaje.

Zaidi ya hapo kila kitu kilikuwa kwa foleni, nchi nzima shule za sekondari za kuhesabika kwa vidole vya mkono. Chuo kikuu kimoja tu, kama kimejaa basi, subiri mwakani au ndio basi tena. Ilifikia wakati hata ukiwa na gari zuri basi wewe ni bepari kila kitu kwa kibali, ukiona gari aina ya Benz basi hiyo ni mali ya Ikulu, watu binafsi si rahisi kumiliki gari kama hiyo yaani hata kuvaa suti ni ubepari. 
Nakumbuka mwaka mmoja aliyewahi kuwa naibu waziri mkuu salim Ahmed Salim, alikuwa Mtwara anahutubia wengi wa wale walio hudhuria walikuwa wamevaa majunia ya mbolea kama nguo.

Baada ya kutawala zaidi ya miaka ishirini na kushuhudia kila kitu kikishindwa na maji yapo shingoni, yanakaribia kuingia mdomoni, kiujanja ujanja na kiutu uzima akaamua kutoroka uongozi, ndio akamtupia Mwinyi maiti akitegemea miujiza ya kufufuliwa, alisha sahau kuwa enzi za wafu kufufuliwa zilisha pita... Akasingizia kuwa anan’gatuka mapema. Kumbe alikuwa ameshindwa kuendesha uchumi wa taifa ili.

Ndio maana leo hii kila nikikumbuka madhira ya utawala wake inanifanya nitamani kwamba mifupa yake ipelekwe gerezani. Kwani ni yeye aliyetudhurumu Waislamu na akahasisi siyasa na sera mbovu dhidi ya taifa ili la Tanzania na mpaka leo hatujainuka tena.

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!