Monday 6 July 2015


Salaam wandugu na marafiki, matumaini mu wazima wa afya na siha njema. Leo nimewakumbuka, ila sijui kilichonifanya niwakumbe, labda ile ndoto nilio ota jana usiku, ndoto iliyonikumbusha mbali sana kimaisha.

Kipindi ambacho kule kwetu nchi ya Bongoland, wenyewe tukiita Nchi ya Musa, au ya Mchonga, Rais pekee ambaye hakuwahi kugombea kiti chake cha urais na mtu yoyote yule mpaka anaondoka madarakani, msiniulize kwanini, sitaki umbea, kwanza icho sicho nilichotaka kukisimulia hapa naona tu mshaanza kunitolea mimacho...! Ah ah ah

Wacha nirudi kwenye ile ndoto yangu ambayo imenifanya nusu niwe na uzuni, robo furaha, na robo nyingine ya machozi, sijajuwa ya uzuni au furaha au ni zile kumbukumbu za ile ndoto iliyonikumbusha zamani.

Kila nikikaa naiona tena na tena kwenye hisia na mawazo yangu, ndoto ambayo inaniletea twasura ya Mwanamke aliyenipenda kwa dhati, bila masharti wala kulazimishwa, upendo wake ulikuwa dhahiri, ukijionesha wazi wazi machoni kwake na hata vitendo vyake viridhihira upendo wa kweli.

Nilikuwa nikideka na kubembelezwa, nikipakatwa na kusimuliwa visa mbalimbali vya kuvutia na kufurahisha. Mwanamke yule alijuwa nini haswa ninataka, alijuwa wakati gani nina njaa, hata kama sikumwambia, alijuwa kile nisichokijua katika maisha... Hakika zilikuwa siku za furaha na raha katika maisha yangu, kiasi cha kutamani siku zile zirudi tena kama zamani.

Hakika zilikuwa siku za furaha na amani katika uhai wa binadamu yoyote yule...! Ile twasira kila ikinijia uja na kumbukumbu zile zile za miaka ile mingi iliyopita, kiasi imeacha athari ambayo haitaweza kufutika katika maisha yangu yote mpaka naingia kaburini. Labda mapenzi yale naweza kuwasimulia watoto wangu na Mungu akipenda labda wajukuu zangu kama nikijariwa kuwa nao.

Hakika sina mfano wowote ambao naweza kumfananisha mwanamke yule na jinsi alivyojitolea muda na wakati wake kuniangalia na kuhakikisha kuwa ninakuwa mtu mwenye furaha wakati wote, hata kipindi kile ambacho nchi ilikuwa na upungufu wa vyakula, hakusita kujinyima na kunifichia ili nikirudi kutoka kwenye miangaiko yangu isiyoeleweka basi unipatia kile alichokificha ili nitulize njaa tumboni. Tena wakati huo uniwekea maji uko bafuni na kunitaka nikakoge kabla sijatia chakula tumboni. Hakika kila nikimkumbuka machozi unilenge lenga uku nikiwa na tabasamu la uzuni usoni kwangu.

Hama kweli siku hazigandi, leo ni miaka imepita tangia alipofariki Mwanamke aliyenipenda kwa moyo wake wote na kuhakikisha kuwa ninakuwa Mwanamume mwenye kujitegemea na kuweza kuishi na watu mbalimbali kiasi cha kupigiwa mfano.

Kwa hakika sina ambacho naweza kumlipa Mwanamke yule ambaye hakuwa mwingine zaidi ya Mama yangu Mzazi aliyenilea kwa mapenzi makubwa, akinifundisha hishima na adabu, nai jinsi ya kuishi na watu.

Hakika si rahisi kwa mtoto aliyelelewa na mzazi wake, waliosumbuka ulipoumwa, ikawa rahisi kusahau na kutupilia mbali kumbukumbu zote za malezi, na kukesha kule, hakika Mwenyezi Mungu amesema kweli aliposema...!

Na tumemuusia mtu kwa wazazi wake wawili. Mama yake ameichukua mimba yake kwa udhaifu juu ya udhaifu, na kumwachisha ziwa baada ya miaka miwili: 

Nishukuru Mimi na wazazi wako. Ni kwangu Mimi ndiyo marudio
Surat Luqman [31]: 14

Alhamdulillah...!

Mola wangu Mlezi! Nighufirie mimi na wazazi wangu, na kila aliye ingia nyumbani mwangu kuwa ni mwenye kuamini, na Waumini wote wanaume, na Waumini wanawake.
Ewe Mwenyezi Mungu msamehe Mama yangu na ipandishe daraja yake katika wailoongoka, na weka badili yake kwa aliyowacha nyuma na utusamehe sisi na yeye ewe Mola wa viumbe vyote, umkunjulie yeye katika kaburi lake na umtilie mwangaza ndani yake.
Amiyn, Amiyn, Amiyn

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!