Monday 18 January 2016

VISA NA MIKASA MITAANI

Nakumbuka Zamani, Huku Mitaani Kwetu Ambako Mnapaita Uswahilini au Kwa Lugha ya Kisiku Hizi Uswazi, Kulikuwa na Tabia Moja Linapokuja Swala la Harusi au Hata Unyago.

Wengi walipendelea kuita vikundi vya ngoma na haswa ngoma ya Mdundiko... Ngoma hii ilikuwa ikipigwa na kina baba na wachezaji wengi walikuwa ni kina mama na watoto wadogo.

Siku hizi ngoma hii haipo tena labda kupatikanaji wake ni wa nadra sana. Sasa hivi kuna vikundi vingine kama vile Mchiriku au Mnanda, siku hizi wanaita Singeli, kuna pia Baikoko na vinginevyo.

Ndio utakuta wengine nahisi ndio hawa wamekuwa wapiga debe wa mabasi ya daladala vituoni na wengine nadhani kama wameajiliwa kuwa mgambo wa manispaa.

Wapigaji wa ile ngoma ya Mdundiko enzi zile walikuwa kama mateja kwa kuzoea kwao kupigapiga zile ngoma, kiasi ambacho nahisi wakikosa kupiga basi hamu yao umalizikia kwa watu wengine na haswa kwa wake zao.

Kuna wanaume ambao mpaka leo wanadhani, kwa akili zao fupi kuwa kupiga wake zao ndio kuonyesha kuwa wao ndio wanaume wa ukweli.

Juzi kati hapa kwetu jamaa mmoja mwenye akili fupi kama hizo, ambaye daima haoni tabu kumshushia mkewe kipondo kama vile anapiga ngoma ya Mdundiko au Mganda, Siku hiyo yalimkuta makubwa maana siku hizi anatembea kama yule ndege Penguini, huku anachechemea.

Siku hiyo hisiyo na jina, wapangaji wote tulikuwa vyumbani mwetu. Kama mnavyojua hizi nyumba za kupanga zisizo na dari unasikia kila kitu nini mtu anafanya au anafanyiwa.

Si ajabu kwa kila chumba kusikia sauti za redio au Luninga ya stesheni tofauti.

Huku wengine utawasikia wakikoroma wengine wakicheka wengine wakinung’unika, ndio maisha yetu tena ya kila siku.

Ghafla bin vu, tukaanza kusikia vikombe na sahani zikivunjwa, kelele za mabishano makali yakaanza. Tukajua jamaa yetu kisha lianzisha kwa mkewe kama ilivyo kawaida yake.

Kisa haswa kilikuwa jamaa katafuta chupi yake haioni.

Taabu ikaanza jamaa kama kawa akaanza kumshushia kipondo mkewe puu... puu... puh! Mama wa watu akaanza kulia kwa uchungu.

Tukaenda kuamulia ugomvi tukakuta wamejifungia ndani, ikawa sasa ni kujaribu kumsihi jamaa. Kila tulipogonga kumsihi afungue mlango, alitujibu Hayawahusu tokeni Tukabaki kusikia tu kilichokuwa kikiendelea kule ndani.

MUME: Shenzi wewe (puuh… puuh… puuh!), huna akili (puuh… puuh… puuh!) chupi yangu iko wapi, umeshahonga kwa mabwana zako, (puuh… puuh… puuh!).

Ni wazi kabisa, mwanamke alikuwa anashindiliwa ngumi nzito nzito.

MKE: Uuuuuuuuuuuuhwiii…! Mume wangu unaniua bure sijui mwenyewe umeweka wapi!

MUME: Kufa (puuh… puuh… puuh!), kufa shenzi we (puuh… puuh… puuh!), Wanakufa panya itakuwa wewe...!

MKE: Baba watoto nisamehe kumbukua mimi mjamzito, muogope Mungu Mume wangu!

MUME: Kwanza mimba siyo yangu (puuh…), Malaya mkubwa (puuh…).

Ghafla kukawa kimyaaaaaaa! Mke halii wala mume haongei na ngumi zimesimama.

Tukajua mambo mawili yeshatokea aidha jamaa kamdedisha mkee au kauwa mkewe...! Punde, dakika chache tukasikia sauti nyembamba ya ukali, kama mtu anayeugua ugonjwa wa pumu ya pua...!

MUME: We malaya ntakuua….! Nasema ntakuua... (kisha kikapita kimya cha dakika tatu nzima).

MUME: Nakwambia niache...!

Mke kimya.

MUME: Aise! Ntakufanya kitu kibaya sana niachie nakwambia!

Mke kimyaaa...

MUME: (Kwa upole, uku sauti ikitoka kama mgonjwa wa pumu) Unajua unaniumiza mwenzio...!

Mke kimya...

MUME: Aise niachie bwana...!

Mke kimyaaa, tunasikia tu ile sauti ya kupumua.

MUME: Nyamtondo mke wangu pliiizi niache, naomba uniachie... Unajua utaniua kizazi mke wangu... niachie nakuomba. Mama mpenzi naomba niachie... mwezioo, Oooh! Mmmh! iiiiih... Uuuuwii, We mwanamke niachie mwenzioo, Aaakh!

Huku nje wambea tukashangaa vipi leo mtemi anabembeleza? Kuna nini?

MUME: Ndugu zangu nisaidieni mke wangu ananiua ukuuu, uwiii ananiua ameshika nanihiiiuuuu... Jamani nisaidieni...EeeeH Mmmh! iiiiih... Uuuuh, nakufa mie mwenenu, iiih, aaah!

Kwa kuwa mlango ulikuwa umefungwa ilituchukua muda kuuvunja, wakati huo jamaa tumemkuta hoi bin taaban, kijasho kikimtoka sanjari na machozi, yaliyochanganyika na makamasi mepesi kama mgonjwa wa mafua, vinamtoka kwa pamoja, mke katulia kimya, ameminya sehemu nyeti.

Yaani jeshi la mgambo kama si la sungusungu wamekamata Ikulu na nchi imesalimu amri...!

Jamaa yetu kawa mpole kuliko mwanasesere wa kuchezea...!

Ana mwezi wa pili sasa anatembea kama wale Pengwini au Bata mzee!

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!