Wednesday 17 February 2016

Jamaa yangu kaja kunitembelea na mimi nilifurahi sana, maana sijaonana naye tangu tulipokuwa shule miaka hiyo. Kwa hiyo tulianza na stori za shule na kukumbuka wale jamaa wenye vituko tuliosoma nao, na kukumbushana vituko vyao.

Kadiri muda ulivyokwenda nikagundua kuwa jamaa hana mpango wa kuondoka kwangu, basi nikajitayarisha kisaokolojia kuwa jamaa atalala hapa kwangu, kwa vile nilikuwa na chumba cha wageni haikunisumbua sana. Kati ya mengi aliyoniambia ilikuwa ni swala la ndoa yake. Jamaa aliniambia alipata bahati ya kumuoa binti mmoja mrembo aliyemkuta kwenye tamasha moja la muziki akiwa mmoja wa wanamuziki wa kibongo flava.

Binti huyu ambaye alikuwa maarufu kutokana na kuwa na nyimbo kadhaa zilizopendwa na pia picha yake kuwa katika magazeti mbalimbali, ilikuwa kama ndoto jamaa kukutana naye na wakagundua wanapendana. Siku ya kwanza wakabadilishana namba za simu na palepale mambo ya kuchat kwenye whatsApp yakaanza, mapenzi motomoto masaa ishirini na nne.

Hatimae kupitia whatsApp wakakubaliana kuoana. Siku ya harusi jamaa yangu kachukua mtoto na kurudi naye kwake kwa mara ya kwanza. Pamoja na haya yote rafiki alitoa chozi akilalamika na kunionya nisioe supastaa, maana yake kesho yake alfajiri binti alibeba vitu vyake na kuita teksi na kurudi kwao.

Kila nikimuuliza jamaa tatizo lilikuwa nini mwenyewe akasema mpaka leo haelewi. Nikamuuliza maswali mengi ya kiutu uzima ambayo siwezi kuyarudia humu, jamaa yangu kasema yote hayo hayakuwa tatizo. Na hawajawahi kuwasiliana mpaka leo, kwani supastaa hataki kujibu meseji wala simu.

Nikamuonea huruma sana rafiki yangu, hatimae nikamuonesha chumba cha kulala. Masaa machache baadaye nilishtuka usingizini, sijui nini kilinishtua lakini nilipoamka harufu kali na mbaya mithili ya panya aliyeoza iliniingia puani, ikanifanya usingizi wote uishe.

Alfajiri niliwahi kuamka kabla ya mnadi swalah! Ili niwahi niondoe hiyo harufu mgeni wangu asije akakosa raha akiamka, nilipofungua mlango harufu ilizidi, nilipoangalia mlangoni kwenye chumba alicholala mgeni wangu nikaona kavua viatu kaviacha nje na soksi zake, huwezi amini harufu kali ile ilikuwa viatu na soksi za mgeni.

Nilibeba viatu na soksi na kuvitoa nje, na palepale nikapata jibu kwa nini mke alimkimbia siku ya kwanza. Harufu ile haivumiliki nakwambia!

Na ili ni tatizo la wanaume wengi sana, utamuona mwanamume mtanashati kavaa nguo zimemkaa kama kazaliwa nazo, sasa basi likija swala la kuvua viatu ndio utajuwa harufu ya nguru au papa au kitunguu inanukia vipi.

Yani mtu soksi zina mwezi mguuni, na utakuta wengine hata kufuri kubadirisha ni baada ya wiki mbili, tena baada ya kuchukuliwa na panya na kusokomezwa uko kusikojulikana ndio atatafuta nyingine avae.

Hivi ili tatizo linatokana na nini kaka zanguni, kwanini lakini hatutaki kuwa watanashati kwenye masuala ya kubadilisha soksi na chupi a.k.a Kufuri!?

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!