Tuesday 16 June 2015


Ndugu zangu Waislam, nachukuwa nafasi hii kuwakumbusha na kuikumbusha nafsi yangu, kumcha Allah na kuwacha yale yote tuliokatazwa na Mwenyezi Mungu, na haswa tabia ya kuwafanyia wengine Hasadi.

HASADI ni maradhi ambayo yameenea sana katika nyoyo zetu sisi Waislam, kiasi cha kuondoa mapenzi miongoni mwetu.

Hasadi ni jambo baya sana likimvaa mtu, hasadi ni ugonjwa wa kujitakia, maradhi haya ya hasadi, uenea kwa haraka sana kwenye mwili wa binadamu kama vile kirusi cha HIV kinavyoweza kuenea kwenye mwili wa muhathirika, kiasi cha kuharibu ubongo wake na afya ya mwili na akili yake.

Sisi wanadamu ndivyo baadhi yetu tunaishi tukiogelea kwenye bahari ya hasadi na chuki zilizopindukia mipaka. Wapo wenye kuweweseka na aidha ilmu, uwezo, furaha au utajiri wa mtu Fulani, wakati mwingine hata wajihi na mwonekano wa Fulani utaka wao ndio waupate au kustaiki wao.

Pia wapo wenye kuona vibaya jinsi mahusiano au masikilizano kati ya mtu na mtu wangestahiki wao, kwa kuwa tu Fulani anapendwa na wengi au kusikilizwa na wengi kwa ilmu au hikma zake, wakatamani hayo yote wapewe wao na mtu huyo anyimwe rehma hizo kwa kuwa tu anamchukia.

Hasadi ni mbaya, na mwenye hasadi hatazamii jema kwa mwenzie, ila ufurahi kuona mwenzie akiharibikiwa, na utamani kuona mwezie adharauliwe, hasusiwe na kama maradhi yake ndio hayo, basi haridhiki mpaka ahakikishe anafukiwa kaburini tena isitoshe si hasha akatamani nafsini mwake ahadhibiwe hata kama alikuwa mtu mwema, bali yeye ampendi tu, wapo watu wa namna hii.

Uchukia kila zuri la asiyempenda, daima huwa anawaza lini atapata nafasi asimuone adui wake akiwa na furaha. Mtu wa namna hii hata sehemu anapofanyiakazi uwa hana raha na anaweza kuharibu kazi ya watu pale anapoona hasimu wake akifanikiwa au kupandishwa cheo.

Hata humu mitandaoni, utawaona wakikesha kusoma habari za mahasidi wao, ili kuona nini ameandika, ili ajitengenezee uadui, akikosoe kile kilicho andikwa hata kama ni kweli au atukane tu, kwa kufanya hivyo anafikiria kuwa anamkomoa hasimu wake huyo kumbe ndio anazidi kujiangamiza katika kaburi la kisaikolojia, kiasi mtu huyu hukosa raha nafsini mwake, japokuwa mbele za watu hujifanya ni mwenye furaha na mafanikio tele, kumbe moyoni yu ateketea kwa chuki na hasadi zake.

Hasadi hizi ufanywa na wanaume na wanawake dhidi ya wenzao, lakini la ajabu wengine uwafanyia hata ndugu zao wa toka nitoke, uwarambazia uwadui huo.

Kwanini mtu aumwe kwa jambo ambalo hata mwezio akilipata halikupunguzii au kukuzidishia chochote katika maisha yako? Hiwe kapata cheo nawe upendi, kapata elimu, wewe upendi, anapendwa na watu wewe upendi, akisaidia watu wewe upendi, kila jema analofanya wewe upendi.
Kiasi cha kumwendea mafichoni na kumfanyia uhasidi kwa watu na yawezekana ukafika mpaka kwa wachawi na kutafuta kumroga ili ahribikiwe.
Hasidi hajui kuwa hayo yote ni majaaliwa yake Mola, umpa amtakaye, umnyanyua amtakaye, mimi na wewe hatuna uwezo wa kumteremsha au kumpandisha yoyote hapa duniani.

Kwanini tusiangalie nafsi zetu kwanza, kabla ya kurusha vijembe kwa wengine, maana tabia hizi za hasadi uzeesha mtu kiasi cha kuonekana mzee kabla ya umri wake, sababu wewe kila ukimuona au ukiona kile unacho kfanyia hasadi, unakunja sura kama matuta ya viazi, vipi usizeeke kabla ya wakati wako, ili hali hasadi imekujaa kila mahala!?

Hasidi hawezi juwa kuwa kila anapofanya hasadi zake, yule anayefanyiwa hasadi ndio anazidi kufanikiwa, ukimsema vibaya mtu kwa hasadi zako, MwenyeziMungu mtu huyo umjaza mapenzi kwa watu, na uzidi kupendwa na jamii, na mwisho wa hasidi huyu ni kuwa dhalili, mgonjwa na ukonda si kwa maumbile bali analika kwa chuki na hasadi na choyo zake, na kama ni unene basi si wa siha au maradhi au ukoo bali ni kwa safura zinazotokana na hasadi zako.

Kwa wenye maradhi haya ya hasadi basi huu ni wakati wa kujirekebisha na si kumfanyia uhasidi mwandishi wa makala hii, maana kwa husuda na choyo zao, wanatamani maneno haya wangeandika wao.

Nawatakieni kila la kheri-Wabillah Tawfiq. Assalamu Alaiykum wa rRahmatullah wa Barakatuh


0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!