JE, NI MASLAHI BINAFSI, UKOSEFU WA MSIMAMO AU
KUPUUZA HISTORIA YA MAUAJI TANZANIA?
Kuhama chama si dhambi. Dhambi ni kuhama misimamo, kuhama ukweli, na kuhama dhamana kwa wananchi. Historia ya mauaji inatukumbusha: cheo ni dhamana, si kinga. Mwanasiasa anayepuuza historia hii, leo akisifia, kesho akilaani, huyo anapigania tumbo lake tu.
Wanasiasa wa Tanzania wanapaswa kutambua kuwa historia itawahukumu vikali. Kitendo cha kuweka mbele maslahi ya matumbo yao na kuwa tayari kugeuka geuka kiitikadi kinazidi kuchelewesha upatikanaji wa Katiba Mpya na Tume Huru ya Uchaguzi, vitu ambavyo vingemaliza kabisa mzunguko huu wa ukatili na mauaji kila msimu wa uchaguzi. Bila kuwa na viongozi wenye msimamo thabiti (kama ule wa uwajibikaji wa Ali Hassan Mwinyi wa mwaka 1976), siasa za Tanzania zitabaki kuwa biashara ya watu wachache, huku raia wa kawaida wakiendelea kuwa wahanga wa upepo wa kisiasa.
---
1. UTANGULIZI:
“SIASA HAINA ADUI WA KUDUMU” – KAULI AU KISINGIZIO?
HAMAHAMA YA WANASIASA: Katika siasa za Tanzania hasa vyama vya siasa viliporuhusiwa au kurejeshwa tena, kumekuwa na wimbi la wanasiasa kuhama vyama, leo yupo chama fulani, kesho anarudi au kuhamia kingine. Swali kuu linabaki: je, hii ni ishara ya demokrasia yenye afya au ni dalili ya kukosekana kwa misingi, msimamo na uwajibikaji wa kisiasa?
Swali la Msingi: Wanatafuta Nini?
Ni kutafuta maslahi binafsi (matumbo), ukosefu wa msimamo thabiti, au kupuuza historia ya mauaji na ukandamizaji wa kiutawala nchini?
Mjadala huu hauwezi kukamilika bila kuangalia historia ya nchi, hasa matukio mazito ya kiusalama na mauaji ambayo yalipaswa kuwa somo kwa wanasiasa wa Tanzania ili kujenga misimamo thabiti.
SIASA ZA KUHAMAHAMA VYAMA: UHURU AU MASLAHI?
Kihalisia, katiba na sheria za vyama vya siasa zinamruhusu mwanasiasa kuchagua chama anachotaka. Hata hivyo, changamoto ipo kwenye nia na muda wa maamuzi hayo.
Kwa mujibu wa wachambuzi, wanasiasa wanaohama wamegawanyika makundi mawili:
WENYE MISINGI NA ITIKADI: Wanahamia chama chenye maadili wanayoamini. Ni Wanasiasa wachache sana, huhama kwa sababu za sera na mwelekeo.
WAPENDA MASLAHI BINAFSI: “Popote panapo maslahi watakwenda”. Hawa ndio waliozua msemo “Siasa Haina Adui wa Kudumu” kauli ambayo kwangu mimi naiona kama upuuzi na ulaghai.
Hawa ni wenye siasa za matumbo; hutanguliza maslahi binafsi kuliko maslahi ya wananchi. Hawa ndio wanaoleta mashaka makubwa kwa jamii. Wanapokuwa nje ya mfumo, huikosoa serikali kwa nguvu zote. Lakini wanapopata nafasi ndani ya mfumo huo huo:
Hawakatai uteuzi.
Wananyamaza au kubadilika ghafla.
Baada ya kuondolewa madarakani, hurudi kuwa wakosoaji wakubwa.
Tatizo linakuja pale mwanasiasa anapokuwa serikalini: anasifia mfumo. Akiondolewa au kumaliza muda, ghafla anakuwa mkosoaji mkubwa. Hii inazua maswali: je walikuwa wanaficha ukweli wakiwa madarakani? Au walikuwa wanakula keki kimyakimya?
2. HISTORIA YA MAUAJI YA KISIASA TANZANIA:
Na Athari Zake Kisiasa, Kwa Nini Inapaswa Kukumbukwa.
Kabla ya kumhukumu mwanasiasa anayehama, ni muhimu kuweka mizani ya historia ya damu iliyomwagika. Historia hii ndiyo inayopaswa kutengeneza misimamo ya viongozi.
2.1. Mauaji ya Shinyanga 1976 na Kujiuzulu kwa Ali Hassan Mwinyi.
Julai 1976, yalitokea mauaji mkoani Shinyanga. Ali Hassan Mwinyi, akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, alimuandikia Rais Mwalimu Nyerere barua ya kujiuzulu uwaziri. Alisema “Hakuna sababu ya kiongozi kujiuzulu baada ya kutokea mauaji” lakini yeye aliona ni wajibu kuwajibika.
Uamuzi huo ulimjengea heshima na baadaye mwaka 1985 akawa Rais wa Awamu ya Pili.
Somo hapa tunaona mfano wa uwajibikaji wa kisiasa, jambo ambalo siku hizi lhalipo. Leo, viongozi wangapi wako tayari kuwajibika mauaji yanapotokea?
2.2 Mauaji ya Mwembechai, 13 Februari 1998
Siku ya Ijumaa, 13 Februari 1998, polisi wa FFU walifyatua risasi kwa waumini wa Kiislamu Msikiti wa Mwembechai, Dar es Salaam. Angalau watu wanne waliuawa. Tukio lilitokana na mchungaji wa Kikatoliki kudai Waislamu walikuwa wakimkejeli Yesu, madai yaliyothibitika kuwa ya uongo.
Waziri wa wakati huo wa Mambo ya Ndani, Ali Ameir, alisema hali hiyo ilikuwa moja ya changamoto kubwa alizokumbana nayo.
Hili lilizua:
Maswali juu ya matumizi ya nguvu za dola
Hofu ya mgawanyiko wa kijamii
Wito wa uwajibikaji wa viongozi
Tukio hili liliibua maswali kuhusu uhuru wa dini na matumizi ya nguvu kupita kiasi na vyombo vya usalama.
Lakini, je, wanasiasa wa leo wanajifunza nini kutoka hapa? Au wanalitumia tu kama silaha ya kisiasa wanapokuwa nje ya madaraka?
Muda baadae, Msomi ambaye hapendi kuitwa Profesa, aliekuwa mhadhiri muandamizi Udsm, Professor Hamza Mustafa Njozi, akaandika kitabu "Mwembechai Killings and the Political Future of Tanzania" ni kazi inayochunguza mauaji ya Mwembechai ya mwaka 1998 jijini Dar es Salaam na kuangazia athari zake pana kwa haki, demokrasia, na utulivu wa kisiasa nchini Tanzania.
Kitabu kilipigwa marufuku kuingia nchini wakati wa Rais Mkapa.
Serikali ilikataa uchunguzi huru na ikapiga marufuku mkutano wa wanawake wa Kiislamu waliotaka kuzungumza unyanyasaji waliopata rumande. Mwembechai ikawa alama ya ubaguzi wa kidini na matumizi mabaya ya dola.
2.3 OPERESHENI MKIRU - (Mkuranga, Kibiti, Rufiji) 2013-2017
MKIRU ni kifupisho cha Mkuranga, Kibiti NA Rufiji. Hayo ni maeneo yaliyokumbwa na mauaji ya polisi na viongozi wa serikali kuanzia 2013.
Eneo la Pwani ya Tanzania, lilishuhudia mfululizo wa mauaji ya askari polisi na raia. Serikali ilianzisha Operesheni MKIRU ili kukabiliana na kile kilichoitwa ugaidi au uhalifu uliopangwa. Operesheni hii ilitumia ujasusi mkubwa na ilifanikiwa kupunguza matukio hayo.
Hata hivyo, ilizua madai ya ukiukaji wa haki za binadamu.
Chanzo kikuu kilichotajwa:
Chuki za wananchi dhidi ya polisi: 23 Januari 2013, mkazi wa Kibiti alifariki Muhimbili kwa madai ya kupigwa na polisi. Wananchi walifunga Barabara ya Kilwa kwa zaidi ya saa 3 na kuchoma kituo cha polisi.
Unyanyasaji wa kiuchumi: Ripoti ya Mwananchi Mei 26, 2017 ilieleza kuwa vijana wa MKIRU wanategemea mkaa, magogo, mazao, lakini wananyanyaswa na mamlaka, maliasili, mgambo na polisi.
Hadi leo, dhana 4 zinazunguka MKIRU: Ugaidi, Chuki za Kisiasa, Chuki Dhidi ya Polisi, au Uhalifu wa Kawaida.
Matukio haya:
Yalionesha changamoto za usalama.
Yalifichua mapungufu ya uwazi katika operesheni za dola.
Lakini bado, hakuna mjadala wa kina unaoongozwa na wanasiasa wenye msimamo, wengi huongea kwa msimu.
2.4 MAUAJI YA
ZANZIBAR KILA UCHAGUZI.
(Kuanzia
Mwaka 1995, 2000, 2005, Hadi 2021).
Zanzibar ina historia ndefu ya damu wakati wa uchaguzi:
29 Oktoba 2000: Uchaguzi ulivurugwa. Waangalizi wa Jumuiya ya Madola, OAU, SADC walisema ulikuwa na dosari kiasi cha kutokuwa na hadhi ya kuitwa uchaguzi.
27 Januari 2001: Polisi waliwaua waandamanaji wa CUF. Serikali ilisema waliuawa 23, CUF walisema 67. Human Rights Watch ilithibitisha angalau 35 na zaidi ya 600 kujeruhiwa. Zaidi ya 2000 walikimbilia Kenya kama wakimbizi.
2020-2025: Vikundi vya “Janjawid” na vikosi kazi vimedaiwa kutumika kuumiza wapinzani. Haji Omar Kheir, Mshauri wa Rais tangu 2023, ametajwa majukwaani na Maalim Seif kuwa muasisi wa vikundi hivyo.
Historia ya chaguzi za Zanzibar imekuwa ikihusishwa na:
Vurugu.
Mauaji.
Migogoro ya kisiasa.
Haya si mambo mapya, lakini swali ni:
Kwa nini bado yanajirudia kila uchaguzi?
2.5 TUKIO LA 29 OKTOBA 2025.
Hadi kufikia nyakati za hivi karibuni, ikiwemo matukio mabaya ya mfululizo wa utekaji, upotezwaji wa watu, na vifo vya wanaharakati pamoja na viongozi wa kisiasa wa upinzani (kama vile mauaji ya wanasiasa wa Upinzani, na wengine), damu inaendelea kumwagika. Wananchi wanapoteza maisha wakiamini wanapigania mfumo bora wa maisha, huku wanasiasa wakichukulia harakati hizo kama mtaji wa biashara zao binafsi.
Uchaguzi Mkuu wa 29 Oktoba 2025 ulifuatiwa na ukandamizaji mkubwa. Ofisi ya Haki za Binadamu ya UN iliripoti:
Mamia waliuawa, idadi isiyojulikana kujeruhiwa au kukamatwa.
Zaidi ya 150 walikamatwa tangu siku ya kura, wengi wakiwa watoto, wakishtakiwa kwa uhaini.
Inasemekana miili ilichukuliwa na vyombo vya dola na kupelekwa sehemu zisizojulikana ili kuficha ushahidi.
Miundombinu na mali za watu binafsi ziliharibiwa, kupelekea wengi kupata hasara na hata kufirisika.
Mashahidi walisema askari walifyatua risasi za moto moja kwa moja. Viongozi wa upinzani na makundi ya haki wanasema vifo ni “mamia hadi zaidi ya elfu”, wengi wakiwa vijana, wanawake, watoto. Asilimia 95 ya waathirika walipigwa risasi kichwani au kifuani kwa karibu, kuashiria “nia ya kuua sio kutawanya”.
Mtandao ulizimwa, vyombo vya habari vikadhibitiwa. UN ilitaka uchunguzi huru na kuachiliwa kwa Tundu Lissu na wengine.
Hali hii imepelekea kujiuliza mambo haya matatu:
Uhuru wa kisiasa
Usalama wa raia na mali zao
Nafasi ya vyama vya upinzani
Lakini badala ya kujenga hoja za pamoja, wanasiasa wengi wamegawanyika kulingana na maslahi yao binafsi.
3. KWA NINI WANASIASA “NJE YA MFUMO” HAWAJUMLISHI KUPATA MAJIBU?
Wengi wanaopinga serikali wakati wako nje ya madaraka, wanapopata vyeo huwa kimya au wanashiriki katika mfumo huo huo.
Ukosefu wa Uwajibikaji wa Kitaasisi: Tangu Mwinyi ajiuzulu 1976, ni viongozi wachache wamewajibika. Mauaji ya Mwembechai 1998, MKIRU 2017, Zanzibar 2001 na 2025, hakuna ripoti ya wazi ya serikali wala hatua kwa wahusika. Hii inafanya “nje ya mfumo” wasiamini mfumo utatoa haki.
Matumizi ya Dola Kulinda Maslahi: Historia inaonyesha polisi na vyombo vya usalama vikitumika kukandamiza upinzani. Hivyo mwanasiasa akitoka nje, anakuwa hana ulinzi.
“Maslahi ya Tumbo” vs Msimamo: Wapo wanaosubiri nafasi. Wakiwa nje wanasema serikali ni mbaya. Wakipewa uteuzi, wananyamaza. Hii ni “undumila kuwili na Ubarakala” – unafiki wa kisiasa. Lakini pia wapo wanaohofia uhai wao. Bila ulinzi wa kisheria, kusema ukweli ukiwa ndani ni hatari.
3.1. SIASA ZA KUHAMAHAMA VYAMA: UHURU AU MASLAHI?
Kihalisia, katiba na sheria za vyama vya siasa zinamruhusu mwanasiasa kuchagua chama anachotaka. Hata hivyo, changamoto ipo kwenye nia na muda wa maamuzi hayo.
Kwanini hawaunganishi dots (hawajumlishi, hawatoi wala kuzidisha, sembuse kugawanya) kupata majibu?
Wanasiasa wa Tanzania wanajua fika historia ya mauaji ya Shinyanga, Mwembechai, Zanzibar, na utekaji wa sasa. Wanajua kuwa tatizo ni mfumo wa kiutawala (Structural Problem) unaolinda madaraka ya chama kimoja na kuminya haki. Hata hivyo, hawataki kujumlisha matukio haya ili kujenga msimamo imara wa muda mrefu kwa sababu msimamo unagharimu. Kupigania mfumo wa haki kunahitaji kujitoa mhanga, jambo ambalo wanasiasa wengi hawapo tayari kulifanya pindi fursa ya "kula" inapojitokeza. Wanapigania maslahi ya matumbo yao na familia zao.
Unafiki wa kutosusia nyadhifa za kiserikaliHili ni swali la msingi sana: Kwanini mwanasiasa anayejinasibu kuwa upande wa wananchi akichaguliwa au kuteuliwa kwenye nafasi ya kiserikali (kama ubunge, uwaziri, au ubalozi) hawakatai?
Wanapokuwa ndani ya mfumo, wananyamaza kimya kabisa. Hawazungumzii mauaji, hawazungumzii utekaji, na wanatetea bajeti na sera mbovu.
Wanajifanya kuona serikali ni mbaya na ina ukatili pale tu wanapomaliza muda wao au wanapoondolewa kwenye vyeo vyao (Political Rejection). Huu ni uthibitisho tosha kwamba hawakuwa na uchungu na nchi, bali walikuwa na uchungu wa kupoteza fursa ya kufaidika na mfumo.
"Mwanasiasa anayelalamika kuwa mfumo ni mbaya baada ya kufukuzwa kazi, halalamikii mfumo, analalamikia kukatwa kwa mirija yake ya ugali."
3.2 AINA TATU ZINAZO PELEKEA WANASIASA KUHAMAHAMA VYAMA:
Wenye Misingi ya Kiitikadi: Wachache sana, huhama kwa sababu za sera na mwelekeo.
Wanaotafuta Nafasi: Uhama pale wanaponyimwa uteuzi au mamlaka. Hawa ndio wale siasa za tumbo (Mslahi Binafsi). Hutanguliza maslahi binafsi kuliko maslahi ya wananchi. Wengine hubadili vyama ili kupata nafasi za kiserikali, mikataba, au ulinzi.
Ukosefu wa Taasisi Thabiti za Vyama: Vyama vingi vinategemea watu binafsi badala ya msimamo wa kiitikadi.
Kupuuza Historia: Wanasiasa wachache hujenga misimamo thabiti kuhusu mauaji ya kihistoria (Shinyanga, Mwembechai, MKIRU, Zanzibar) ili kuzuia kurudiwa. Badala yake, wengi hujikita katika siasa za Matukio ya sasa kwa faida binafsi.
3.3 MIFANO HAI YA VIONGOZI WALIOHAMAHAMA.
Wabunge na madiwani wengi wametoka vyama vya upinzani (kama CHADEMA, CUF) na kujiunga na CCM wakati wa mabadiliko ya uongozi, wakidai “kuunga mkono maendeleo.”
Baadhi ya viongozi wa zamani wa upinzani wamechukua nyadhifa serikalini na kuacha kuikosoa serikali kwa ukali walioonyesha awali. Hii inaweza kuashiria undumilakuwili, kuwa na sura mbili kulingana na nafasi.
Hizi ndizo sababu nizionazo zinazoleta mashaka makubwa kwa jamii. Wanasiasa wanapokuwa nje ya mfumo, huikosoa serikali kwa nguvu zote. Lakini wanapopata nafasi ndani ya mfumo huo huo:
Hawakatai uteuzi.
Wananyamaza au kubadilika ghafla.
Baada ya kuondolewa madarakani, hurudi kuwa wakosoaji wakubwa.
Hii inazua swali:
Je, tatizo ni nini?
3.4 CHART
|
Jina la Kiongozi |
Kuhama/Kubadili Msimamo |
Muktadha na Sababu |
|
Edward Lowassa |
Kutoka CCM kwenda CHADEMA (2015), kisha kurudi CCM (2019). |
Baada ya jina lake kukatwa CCM mwaka 2015, alihamia upinzani akidai mfumo wa CCM ni mbaya na haufai. Alikaribishwa na CHADEMA kama "shujaa". Baada ya uchaguzi kupita na upepo kubadilika chini ya Hayati Magufuli, alirejea tena CCM na kusifu kazi ya chama hicho. |
|
Dr. Willibrod Slaa |
Kutoka CHADEMA kwenda Diplomasia (CCM), kisha kurudi upinzani. |
Alikuwa katibu mkuu wa CHADEMA na nembo ya mapambano dhidi ya ufisadi. Mwaka 2015 alijiondoa CHADEMA kupinga ujio wa Lowassa. Na hata kuongeza misumari na kuituhumu CHDEMA kuwa inateka wanachama wake wenyewe. Baadaye aliteuliwa na serikali ya CCM kuwa Balozi. Baada ya kustaafu ubalozi, amerudi tena kwenye msimamo wa kuikosoa vikali serikali kupitia majukwaa ya kiraia. |
|
Lazaro Nyalandu |
Kutoka CCM kwenda CHADEMA, kisha kurudi CCM. |
Alikuwa Waziri ndani ya CCM, akahama na kwenda upinzani akidai mfumo unaminya demokrasia. Baada ya mambo kuwa magumu kisiasa, alirejea tena CCM akidai anaunga mkono juhudi za mwenyekiti. |
|
Prof. Kitila Mkumbo |
Kutoka ACT-Wazalendo kwenda CCM. |
Alikuwa mmoja wa waasisi wa ACT-Wazalendo na mkosoaji mkubwa wa kiuchumi wa serikali ya CCM. Baada ya kuteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Rais Magufuli, alihamia rasmi CCM na sasa ni Waziri na mtetezi mkubwa wa mfumo ule ule aliokuwa akiukosoa. |
|
Mch. Peter Simon Msigwa |
Kutoka CHADEMA kwenda CCM (Juni 2024), kisha kurudi CHADEMA (Mei 2026) |
Baada ya kushindwa kwenye uchaguzi wa Kanda ya Nyasa ndani ya CHADEMA dhidi ya Tundu Lissu, alitangaza kukihama chama hicho kwa hasira na kujiunga na CCM, huku akimshambulia vikali Freeman Mbowe kwa madai ya udikteta. Hata hivyo, baada ya kukaa CCM kwa takriban miaka miwili na kuambulia patupu kwenye kura za maoni za kuelekea uchaguzi, mnamo Mei 2026 ametangaza rasmi kurejea CHADEMA akidai "nimechoka kuishi kwa huzuni" na kuwaomba radhi Watanzania. |
Maneno ya Peter Msigwa Wakati wa Kuhama.
Uhamaji wa Mchungaji Peter Msigwa kwenda CCM uliambatana na kauli nzito zilizowaacha wananchi na maswali mengi kuhusu msimamo wake wa kiitikadi na "unabii" wa kisiasa aliokuwa akihubiri huko nyuma.
1. Kauli ya "Bata na Tai" (Kujitetea Kuhama CHADEMA)
Alipokuwa akihojiwa na vyombo vya habari kuelezea sababu ya kukimbilia CCM baada ya kushindwa uchaguzi wa ndani CHADEMA, Msigwa alitoa mfano wa ndege akisema:
"Mimi ni mtu wa kusema haki, mimi ni mtu wa kunyoosha maelezo, mtu wa kusema ukweli. Sasa kuna vitu ambavyo naona nikiwa upande huu [CHADEMA], ile umimi inashindwa. Naanza kuwa bata wakati natakiwa niwe eagle (tai). Sasa nikaona isiwe tabu..."
Kauli hii ilitumiwa na wakosoaji wake kuonyesha jinsi alivyokuwa akijitwika ukuu wa "Tai" (ndege anayeona mbali na mwenye nguvu), huku akidhalilisha taasisi na wanachama alioacha nyuma kama "Bata".
2. Kumlipua Freeman Mbowe na Kudai CHADEMA Hakuna Demokrasia
Wakati anapokelewa na Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Samia Suluhu Hassan mnamo Juni 2024, Msigwa hakusita kurusha makombora kwa viongozi wake wa zamani. Alimshambulia waziwazi Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, kwa kumlinganisha na madikteta wa nchi za jirani:
Alidai kuwa CHADEMA imepoteza mwelekeo, haina demokrasia ya kweli, na inafanya "siasa za uongo". Alidai kuwa ndani ya chama hicho hakuna anayetakiwa kuhoji mamlaka ya Mwenyekiti na yeyote anayejaribu kufanya hivyo anakatwa mabawa.
3. Kugeuka na Kusifu Mfumo wa CCM
Ndani ya kipindi chake kifupi akiwa CCM, msimamo wa Msigwa ulibadilika kwa digrii 180. Yule Mchungaji aliyekuwa akipiga kelele majukwaani akilaani ukatili wa serikali ya CCM, mauaji ya Zanzibar, na ukandamizaji, alianza kusikika kwenye mikutano ya kampeni (kama kule Ismani mkoani Iringa) akisema:
"Tanzania ipo salama chini ya Chama Cha Mapinduzi. Upinzani hawana sera za ukombozi, CCM pekee ndicho chama chenye uwezo wa kuongoza na kuwaletea wananchi maendeleo."
Ukweli wa Siasa za "Matumbo": Msigwa Katupwa Kabatini na Kurudi CHADEMA (Mei 2026)
Mchezo huu wa kuigiza wa Mchungaji Msigwa umekuja kuthibitisha kwa vitendo hoja kuu ya makala yetu, kwamba wanasiasa wanatafuta maslahi ya matumbo yao na fursa za madaraka.
Baada ya kuhamia CCM kwa mbwembwe na kugeuka kuwa "chawa" wa kusifu kila kitu, Msigwa aliamini angetunziwa heshima yake na kupitishwa kugombea Ubunge wa Iringa Mjini kupitia tiketi ya CCM. Hata hivyo, mfumo wa CCM ulimtumia kama "karai" la kupigia propaganda na kisha kumtupa kando. Kwenye mchakato wa kura za maoni ndani ya CCM kuelekea Uchaguzi Mkuu, jina la Msigwa liliangukia pua na halikuwemo hata kwenye majina matatu ya juu ya wanachama waliopendekezwa na wajumbe.
Baada ya kuona amewekwa "kabatini" na kupoteza umaarufu wote wa kisiasa mbele ya jamii, mnamo Mei 2026, Mchungaji Msigwa ameamua "kulamba matapishi yake" na kutangaza kurejea CHADEMA kwa aibu, akitoa kauli mpya inayovunja moyo:
"Nimechoka kuishi kwa huzuni, Watanzania naomba mnisamehe..."
Huu ni uthibitisho mwingine hai kuwa wanasiasa hawa hawana chembe ya msimamo wa kiitikadi; upepo wa maslahi binafsi ukivuma upande wa mashariki wanakuwa "Tai wa kijani", upepo ukiwakataa wanarudi upande wa magharibi kuwa "Bata wa bluu", huku damu ya wananchi wanaouawa kwenye harakati za kulinda vyama hivyo ikiendelea kupuuzwa.
Wimbo huu wa Peter Msigwa atangaza kurudi CHADEMA unaonyesha video ya tukio la hivi karibuni ambapo mwanasiasa huyo anaomba radhi hadharani na kutangaza rasmi kurejea chama chake cha zamani baada ya safari yake ya kisiasa ndani ya CCM kukwama.
3.5 BILA KUWAHUKUMU, TUANGALIE MIFANO YA TABIA:
Kundi la “Waliokurupuka 2015-2020”: Wanasiasa kadhaa walihama kutoka upinzani kwenda CCM wakati wa utawala wa Rais Magufuli. Hoja yao: “utawala umekubalika”. Wakosoaji wanasema walitafuta ulinzi baada ya kubanwa.
Kundi la “Waliotoka CCM 2022-2024”: Baadhi ya wabunge na madiwani walihamia upinzani baada ya kukosa teuzi au kura za maoni. Walidai “wanataka mabadiliko”. Lakini walipokuwa ndani, hawakuyasema.
Zanzibar: Haji Omar Kheir alishindwa uchaguzi Tumbatu, akalia kwenye mtumbwi. Baadaye ZEC ikamtangaza mshindi. Akiwa Waziri wa vikosi, vikundi vya kihalifu vilishamiri. Leo ni Mshauri wa Rais. Mfano wa jinsi mfumo unavyoweza kutumika.
3.6 TATIZO KUBWA: Ukosefu wa Msimamo wa Kisiasa
Wanasiasa wengi:
Hawajengi misingi ya kudumu ya sera.
Wanabadilika kulingana na upepo wa kisiasa.
Wanashindwa kuunganisha nguvu wanapokuwa nje ya mfumo.
Badala ya:
Kujenga hoja za pamoja.
Kutoa mbadala wa kisera.
Kulinda maslahi ya wananchi.
Wanageuka kuwa:
“Wapinzani wa muda na watawala wa muda”
4. JE, NI UNDUMILA KUWILI NA UBARAKALA?
Ndiyo, kama kigezo ni “unasema nini ukiwa ndani dhidi ya ukiwa nje”. Lakini pia ni swali la “mazingira”. Mfumo usio na uwajibikaji unazalisha wanafiki na wanasiasa tumbo, wenye kujipendekeza, kwani ukweli ni gharama.
Kwa kuangalia mienendo:
Mwanasiasa anapokuwa nje ya mfumo: Anaona mfumo ni mbaya.
Akiingia ndani ya mfumo: Anakwa karambishwa asali, Ananyamaza.
Akitoka/kufukuzwa: Anarudia ukosoaji ule ule.
Hii ni ishara ya:
Kukosa uadilifu wa kisiasa.
Kukosa ujasiri wa kusimamia ukweli.
Kuweka mbele maslahi binafsi kuliko taifa.
5. HITIMISHO: Nini Kifanyike?
Siasa za bendera kufuata upepo (Siasa Maslahi) ni usaliti mkubwa kwa damu ya Watanzania waliopoteza maisha huko Shinyanga, Mwembechai, Pemba, Unguja, na katika barabara za Dar es Salaam na Tanzania kwa ujumla, kupitia utekaji na mauaji ya kisiasa.
Wanasiasa wa Tanzania wanapaswa kutambua kuwa historia itawahukumu vikali. Kitendo cha kuweka mbele maslahi ya matumbo yao na kuwa tayari kugeuka geuka kiitikadi kinazidi kuchelewesha upatikanaji wa Katiba Mpya na Tume Huru ya Uchaguzi, vitu ambavyo vingemaliza kabisa mzunguko huu wa ukatili na mauaji kila msimu wa uchaguzi. Bila kuwa na viongozi wenye msimamo thabiti (kama ule wa uwajibikaji wa Ali Hassan Mwinyi wa mwaka 1976), siasa za Tanzania zitabaki kuwa biashara ya watu wachache, huku raia wa kawaida wakiendelea kuwa wahanga wa upepo wa kisiasa.
5.1 TUNAWAJIBIKA:
KUKUMBUKA HISTORIA: Shinyanga, Mwembechai, MKIRU, Zanzibar, 29 Oktoba 2025 – damu hizi ni dira. Mwanasiasa asiyejifunza historia atairudia.
UWAJIBIKAJI WA LAZIMA: Kama Mwinyi alivyojiuzulu 1976, tunahitaji utamaduni ambapo waziri, IGP, RPC anawajibika mauaji yakitokea.
TUME HURU ZA UCHUNGUZI: UN imeitaka Tanzania kuchunguza mauaji ya 2025. Bunge linapaswa kuanzisha tume huru kwa Mwembechai, MKIRU, na Zanzibar.
KATIBA MPYA: Ili kuzuia wanasiasa kutumia mianya ya “siasa haina adui wa kudumu”, tunahitaji katiba inayozuia wabunge kuhama vyama bila kurudi kwa wananchi.
WANANCHI WAWE MAKINI: Wasiangalie maneno bali matendo.
Vyama vijenge itikadi: Siasa isiwe ya mtu binafsi.
Historia ya kweli ya Tanzania, ifundishwe, ili makosa yasirudiwe.
6. MWISHO:
Kuhama chama si dhambi. Dhambi ni kuhama misimamo, kuhama ukweli, na kuhama dhamana kwa wananchi. Historia ya mauaji inatukumbusha: cheo ni dhamana, si kinga. Mwanasiasa anayepuuza historia hii, leo akisifia, kesho akilaani, huyo anapigania tumbo lake tu.
Jamii iulize: Kiongozi wako alisema nini kuhusu MKIRU akiwa Mkuu wa Wilaya au mkoa au hata ubalozi? Alisema nini kuhusu mauwaji ya kule Zanzibar na 29 Oktoba 2025 akiwa na cheo? Majibu yake ndiyo kipimo cha msimamo wake.
Wajibu wetu kama raia ni kudai uwajibikaji na kuelimishana ili siasa ziwe za maendeleo, si za faida binafsi.
Na kama historia ya mauaji na matukio ya kiusalama haijawafanya raia na wanasiasa kujifunza, basi swali linabaki wazi:
JE, WANATUMIKIA NCHI… AU WANAITUMIA NCHI?









