UCHAMBUZI YAKINIFU
URITHI, CHANGAMOTO, NA MUSTAKABALI WA SOKO LA MUZIKI MUBASHARA.
UTANGULIZI
Shabiki na mdau wa burudani ya mziki wa kizazi kipya (Bongo Fleva), karibu sana kwenye uchambuzi huu wa kina kuhusu tamasha la kihistoria la "Miaka 30 ya Bongo Fleva" lililofanyika Mlimani City, jijini Dar es Salaam. Tukio hili lilikuwa zaidi ya burudani, lilikuwa kioo cha wapi tulipotoka, wapi tulipo, na wapi tunaelekea na changamoto zinazotukabili mbele yetu.
Nimeandika uchambuzi huu, baada ya kutazama Mubashara muktadha mpana wa tamasha la Miaka 30 ya Bongo Fleva, pamoja na mijadala iliyoibuka mitandaoni.
Nyimbo za zamani (Classic Bongo Fleva) bado zina nguvu kubwa ya kihisia kwa mashabiki. Kazi za wasanii kama Feruz na TMK ziliamsha hisia kali za upendo na furaha, ikithibitisha kuwa nyimbo za kale zilikuwa na ujumbe mzito uliodumu moyoni mwa jamii.
Nyimbo nyingi zilizotumbuizwa (mfano "Tunataabika" ya Juma Nature/TMK) zinaeleza maisha halisi ya mtanzania wa chini, umaskini, ukosefu wa ajira, na mapambano ya kila siku. Hii inabaki kuwa roho halisi ya Bongo Fleva.
Lakini sasa kwenye jukwaa lile, mbele ya maelfu ya wadau, ukweli mchungu ulijitokeza waziwazi.
Kizazi cha wasanii waliobeba bendera ya muziki wa kisasa wa Tanzania kwa miongo mitatu, wengi wao walishindwa kutoa burudani ya moja kwa moja inayolingana na hadhi ya nyimbo zao. Kwa nini waimbaji ambao nyimbo zao tunaziimba kwa shauku, ambao midundo yao imetawala anga za Afrika Mashariki, walionekana kuyumbayumba, kukosa mwelekeo, na hata kutokumbuka mashairi yao wenyewe?
Miaka 30 ya Bongo Fleva si tukio la kawaida. Ni dirisha la kutazama safari ya muziki uliobeba ndoto, maumivu, vicheko, na misukosuko ya vijana wa Tanzania tangia miaka ya mwishoni miaka ya 1980s (1988) na mwanzoni mwa miaka ya 1990.
Kutokana na tukio hili la historia ya Bongo Fleva, dhamira kuu zilikuwa:
Kutambua waanzilishi wa Bongo Fleva.
Kuunganisha vizazi vya zamani na vya sasa.
Kuonyesha mchango wa muziki katika utamaduni wa Tanzania.
Kuthibitisha kuwa Bongo Fleva imekuwa sehemu ya utambulisho wa taifa.
Kuhamasisha wasanii wapya kujifunza kutoka kwa waliotangulia.
Kurejesha kumbukumbu za nyimbo zilizojenga tasnia.
Tamasha la maadhimisho lililofanyika Mlimani City limekuwa kama ndio kioo cha wanamuziki wa Bongo fleva, likionyesha uzuri, udhaifu, na ukweli mchungu, ambao mara nyingi hatupendi kuukubali.
Baada ya kutumia muda wangu, kutazama mwanzo mpaka mwisho, nikagundua mambo kadhaa, ikiwemo mjadala mpana unaoendelea mitandaoni: Je, Bongo Fleva imefika wapi? Na tunakwenda wapi, Je tunatosha kimataifa?
Hapa, nitachambua Historia, Utamaduni, Changamoto za kiufundi, na hatimaye mtazamo wangu wa kitaalamu (creative director’s critique) kuhusu nini kilitokea, kwa nini kilitokea, na nini kinapaswa kufanywa ili kuboresha mustakabali wa muziki wetu.
Wasanii Walikuwa Wanauza Kumbukumbu, Sio Muziki wa Bongo Fleva.
HISTORIA YA MUZIKI WA BONGO FLEVA KWA UFUPI
Muziki wa Bongo Fleva umefikia umri wa utu uzima. Muziki Uliobeba Hisia za Mtaani.
Bongo Fleva ilizaliwa kwenye makutano ya mitaa ya Dar es Salaam, Ubungo, Kinondoni, Temeke na Ilala, ambapo vijana walitumia muziki kama njia ya kujieleza.
Ilianza kama hip-hop ya Kiswahili, ikachanganyika na R&B, reggae, na baadaye Afro-pop.
Lakini kilichofanya Bongo Fleva kuwa kitambulisho cha taifa si midundo tu ni lugha, utani, maumivu ya maisha, na ujanja wa mtaa.
Historia ya Bongo Fleva ilianza rasmi mwishoni mwa miaka ya 1980 mwanzoni mwa miaka ya 1990 wakati vijana wa Kitanzania walipoanza kuiga muziki wa Hip Hop kutoka Marekani na kuuchanganya na vionjo vya nyumbani. Katika kuadhimisha safari hii, wadau na wasanii walisherehekea miaka 30 ya Bongo Fleva kupitia tamasha kubwa lililofanyika tarehe 10 Julai 2026 jijini Dar es Salaam.
BONGO FLEVA si muziki pekee, Ni historia ya Tanzania ya baada ya mfumo wa chama kimoja, ukuaji wa miji, ujio wa FM Radio, studio za kurekodia, ujio wa MTV, YouTube na baadaye Streaming.
Katika miaka 30, Kiswahili kimekuwa lugha ya muziki wa kisasa Afrika Mashariki.
Bongo Fleva imechanganya Hip Hop, R&B, Afrobeat, Dancehall, Taarab na muziki wa asili.
Wasanii wamekuwa mabalozi wa utamaduni wa Tanzania duniani.
Muziki umezalisha maelfu ya ajira.
Kwa hiyo tamasha hili linafananishwa na "jubilee" ya utamaduni wa muziki wa Tanzania.
Tamasha lilikuwa ni madhabahu ya kusherehekea historia hii, lakini pia nalitumia kama darasa huru la kuangazia mapungufu ya kiufundi yanayokabiliwa na kizazi chetu cha wasanii wa Bongo Fleva.
Hapa kuna hatua kadhaa zilizounda historia ya muziki huu:
Kuzaliwa kwa Wimbo wa Kwanza (Mwanzo wa Miaka ya 1990).
Kabla ya miaka ya 1990, vijana wengi nchini Tanzania walikuwa wakirap kwa lugha ya Kiingereza wakitumia midundo ya Kimarekani.
SALEH JABIR: Anatajwa kama mmoja wa waasisi muhimu baada ya kurekodi wimbo wa kwanza wa rap ya Kiswahili kati mwaka 1988 na 991 uitwao "Ice Ice Baby" (akigandamizia mdundo wa msanii Vanilla Ice). Hatua hii ilithibitisha kuwa Kiswahili kinaweza kutumika kurap.
Mwaka 1990 hadi 1996, Saleh Jabir na Hard Blasters Crew walipokuwa wanajaribu kuimba Hip Hop kwa Kiswahili, watu walisema haiwezekani. Leo, Kiswahili cha mtaani kimekuwa bidhaa ya kuuza nje. Bongo Fleva ndiyo iliyofanya Kiswahili kiwe lugha kwa vijana wa Afrika Mashariki yote.
Pili, ni kumbukumbu ya uhuru wa kiuchumi: Bongo Fleva ilizaliwa wakati vyombo vya habari binafsi viliporuhusiwa, studio ndogo za Mikocheni na Sinza zilipofunguliwa. Ni muziki wa kwanza wa Tanzania usio wa kuimbwa na bendi za serikali au taasisi. Ni sauti ya mjasiriamali mdogo.
Tatu, ni hifadhi ya historia ya mijini: Nyimbo kama, “Mtoto wa Geti Kali” ni archive ya maisha ya Dar es Salaam, jinsi tulivyovaa, tulivyopenda, tulivyotukanana. Bila maadhimisho haya, historia hiyo ingepotea YouTube tu.
Nne, Sauti ya Kizazi Kilichotengwa: Bongo Fleva ilitoa jukwaa kwa vijana wa mitaa ya Uswahilini, Dar es Salaam na kwingineko, kusimulia hadithi zao za mapenzi, magumu ya maisha, siasa, na ndoto kwa lugha yao ya Kiswahili cha mitaani. Iliwapa sauti wale ambao hawakuwa na sauti katika anga za kijamii.
CHANGAMOTO: Wakati huo, jamii ilitazama muziki huu kama uhuni, na haukuwa ukichukuliwa kama kazi rasmi.
KUPATIKANA KWA JINA LA BONGO FLEVA (1996)
Muziki huu ulifanya kazi kwa miaka kadhaa bila kuwa na jina rasmi la utambulisho.
Mike Mhagama: Mnamo mwaka 1996, mtangazaji wa redio kupitia kipindi cha DJ Show cha Radio One, ndiye aliyebatiza mtindo huu jina la "Bongo Fleva". Alifanya hivyo ili kutofautisha muziki wa Hip Hop na R&B wa Marekani na ule uliokuwa ukitengenezwa na vijana wa Kitanzania. Chimbuko hili lilianzia chini ya uongozi wa mtangazaji mkongwe Taji Liundi (Master T).
MAPINDUZI TOKA STUDIO.
Sauti za Mtaani (Miaka 1990 - 2000s).
Muziki ulianza kukua kibiashara baada ya kuibuka kwa maprodyuza wakongwe kama P Funk 'Majani' (Bongo Records) na Master Jay (MJ Records). Waliingiza vionjo vya kitamaduni kama Taarab na muziki wa Dansi.
Wasanii kama Abdul Sykes (Dully Sykes), Juma Kassim Ally (Juma Nature), Joseph Leonard Haule (Professor Jay), Joseph Osmund Mbilinyi (Mr. II Sugu) na Haroun Kahena (Inspekta Haroun) walianza kuimba kuhusu maisha halisi ya mtaani, umaskini, siasa, na mapenzi. Muziki ukawa sauti rasmi ya vijana.
KUINGIA KWENYE SOKO LA KIMATAIFA (2010 HADI SASA).
Kuanzia miaka ya 2010, Bongo Fleva ilihama kutoka kwenye utamaduni wa Hip Hop safi na kuegemea zaidi kwenye mahadhi ya Afrobeat na Pop yenye midundo ya kuchezeka. Wasanii kama Ali Saleh a.k.a Kibanio (Ali Saleh Gentamilah) kiusanii Alikiba. Jina lake la "Kiba" ni jina la utani ambalo alipewa na ndugu zake tangu akiwa tumboni mwa mama yake. Naseeb Abdul Juma Issack (Diamond Platnumz), na Rajab Abdul Kahali (Harmonize) wameufanya muziki huu kuwa biashara kubwa yenye kutengeneza mamilioni ya pesa na kupata tuzo pamoja na mashabiki duniani kote.
KUTOKA KWENYE CHANGAMOTO HADI FAIDA.
Kwa Zaidi ya miaka 30, muziki huu umefanya mambo makubwa.
Bongo Fleva limekuwa kioo cha jamii ya Tanzania. Kupitia mistari yake, vijana wamekuwa wakielezea mapenzi, umaskini, ukosefu wa ajira, imani, rushwa, ndoto za maisha, kuvunjika moyo, na hata uzalendo. Ni kumbukumbu ya mdomo ya maisha ya Watanzania kwa miaka 30. Kwa hiyo, maadhimisho hayakuwa tu ya kumsifu msanii fulani, bali yalikuwa ya kumheshimu mwananchi wa Tanzania ambaye amekuwa akielezea hisia zake kupitia muziki.
Umeunda mastaa wa kizazi kipya.
Umejenga tasnia ya burudani yenye nguvu Afrika Mashariki.
Umeleta mapinduzi ya mitindo, lugha, na utamaduni mpya kwenye muziki.
Umefanya Tanzania kuwa kitovu cha muziki wa kisasa Afrika Mashariki na kati.
Lakini safari hii haijakuwa nyepesi. Tamasha la maadhimisho limeonyesha wazi sehemu ambazo bado zinahitaji kufanyiwa kazi.
TAMASHA LA MIAKA 30
Katikati ya Sherehe Mubashara, Mambo Vururu Vururu .
Baada ya kutazama Mubashara baadhi ya watazamani na mashabiki waliokuwa wakifuatilia, wakaanzisha mijadala haswa matukio yaliotokea jukwaani. Mimi nitajikita upande mwingine kabisa:
LENGO LA KISANII LILIPOTEA: Dhana ya msingi (concept) ilikuwa nini? Je, hili lilikuwa ni tamasha la kusherehekea kufika miaka 30, au jukwaa la wazi kwa mtu yeyote mwenye umaarufu kuingia?
Kwa nini hatukusikia muziki ukipangwa kwa mfuatano wa historia, kutoka kwa wale waimbaji wa awali walioweka misingi, ukikua na kufikia kisasa. Lile jukwaa lingekuwa ni darasa la historia ya muziki wa Bongo Fleva, na wasanii wenyewe wangesukumwa kujiandaa ili kutojisimanga mbele ya urathi wao wenyewe.
UPOKEAJI WA MGENI (GUEST EXPERIENCE).
Tukio la miaka 30 ya urithi wa muziki wa taifa linahitaji kuwa na "red carpet experience" ya kipekee. Hapa, kulikuwa na mapungufu. Hakuna "narrative arc" hakuna kumbukumbu ya kwenda nayo nyumbani sidhani hata kama kulikuwa na mauzo ya album za wanamuziki na nyimbo zao zilizotamba zamani. Mgeni alikuwa anakuja, anakaa, anasikiliza sauti, na anaondoka bila kuwa na uzoefu wa kipekee. Tukio la kihistoria linahitaji kuwa na vitu vya kumbukumbu vifaa vya kihistoria, picha za zamani, maonyesho ya makumbusho. Hapa, hakuna hata kitu kimoja cha kihistoria kilichokuwa kimeonyeshwa kwa namna ya kitaalamu.
Jambo moja kubwa kabisa, linalojirudia mara kwa mara ni kutokuwepo kwa maandalizi ya kutosha, changamoto za sauti. Wasanii wengi walishindwa kuimba vizuri live, na wengine hata hawakumbuki vizuri mashairi ya nyimbo zao wenyewe au wengine wamepoteza pumzi haraka jukwaani.
Jukwaa lilikuwa kubwa, lakini lilionekana tupu. Wasanii walizurura kana kwamba wamepotea kwenye jangwa.
Hili Limeibua Swali Muhimu:
Kwa nini wasanii wengi wa Bongo Fleva wanashindwa kuimba Mubashara (live), ukilinganisha na wanamuziki wa Taarab na bendi za muziki wa dansi?
Hili ni swali muhimu lakini jibu lake halipaswi kuwa kwamba "hawajui kuimba."
Ninakubali kuwa si kila msanii anahitaji kuwa na sauti ya kuimba live lahasha, wapo wasanii ambao ni "performers" zaidi kuliko "vocalists." Lakini tukio la kumbukumbu la miaka 30 linahitaji kuwa na "vocal excellence." Hapa, kulikuwa na aibu.
Kuna sababu kadhaa za Kiufundi na Kitasnia Zinazowafanya Wasanii Washindwe Kuimba Mubashara.
Hili ni suala ambalo limekuwa likisumbua wapenzi wa muziki wa Tanzania kwa muda mrefu, na katika tukio la Mlimani City, lilitokeza wazi zaidi. Baada ya kuchambua livestream na mazingira ya tasnia ya muziki nchini, hapa ni mnimeahinisha baadhi ya sababu.
Bongo Fleva imezaliwa mtaani na kukulia studio na si jukwaani kama mziki wa Taarabu na Mziki wa Dansi.
Wasanii wengi walionekana kushindwa hata kuimba nyimbo zao wenyewe. Hii sio tu kuhusu uwezo wa sauti ni kuhusu heshima. Mtu anayekuja kutazama tamasha la kumbukumbu la miaka 30 anatarajia kuona ubora. Anatarajia kuona kwamba tasnia imekuwa. Badala yake, aliona kwamba baadhi ya wasanii hawana uwezo wa kuimba hata bila msaada wa studio.
Utamaduni wa Studio Kwanza, Sauti Baadaye:
Bongo Fleva imejengwa juu ya producer, sio juu ya mwimbaji. Msanii anaandika wimbo, producer anamnyoosha sauti kwa Melodyne na Autotune hadi inasikika tamu. Sauti halisi haijawahi kufanyiwa mazoezi. Hivyo jukwaani, anapokosa huo msaada wa kompyuta, anabaki uchi.
Kiufupi, Utengenezaji wa Muziki Unategemea Studio zaidi ya Jukwaa. Wengi wao ni "Studio Artists" wasanii wa studio na sio wasanii wa jukwaani.
Hakuna Shule ya Sauti: Kama ilivyowahi kujadiliwa kwenye jamii yetu ya wadau wa muziki, wasanii wetu hudhani kuimba live ni kubadilisha melody na kupiga kelele, badala ya kusikia sauti yake halisi na ushirikiano na gitaa na kinanda. Hakuna vocal coach, hakuna mazoezi ya kupumua, hakuna warm up.
Wengi wao hawana mafunzo ya jinsi ya kutumia sauti zao vizuri (vocal technique, breath control, pitch accuracy), matokeo yake wanashindwa kuimba vizuri live. Hii ni tofauti na nchi kama Nigeria au Afrika Kusini ambapo wasanii hufanya mazoezi ya sauti kwa muda mrefu kabla ya kutokea jukwaani.
Changamoto za Kiutendaji na Afya ya Sauti: Kutojali afya ya sauti ni dhambi kubwa. Wengi hawafanyi mazoezi ya kufungua sauti (vocal warm-ups), hawajui vyakula au vinywaji vya kuathiri koo, na huishi maisha ambayo hayasaidii uimara wa sauti. Ukichanganya na wasiwasi wa jukwaani, ambao ni mkubwa sana pale mtu anapojua hajajiandaa vya kutosha, koo hukauka, pumzi hupotea, na sauti hupotea, na msanii anaanza kuimba kwa hofu na si kwa ujasiri.
Wasanii wengi hawajui tofauti ya kuimba kwa kifua na kuimba kwa pua.
Uchumi wa Playback: Kwa miaka 15, promota alilipa msanii aje na flash disk. Gharama ya bendi kamili ni milioni 8 hadi 15, wakati gharama ya DJ na laptop ni laki 3. Kwa hiyo wasanii hawakulazimishwa kujifunza kuimba live, kwa sababu soko halikuwahi kudai hivyo. Wasanii wa Taarabu na Bendi za Muziki wanaweza kuimba live kwa sababu bendi ndiyo soko lao, Bongo Fleva soko lake ni klabu.
Katika tamasha nyingi za Bongo Fleva nchini, wasanii wamezoea kutumia "backing tracks" zenye sauti zao zilizorekodiwa, na wao hucheza tu jukwaani huku wakitoa sauti dhaifu au hawatoi kabisa. Hii imefanya kuwa utamaduni ambao wasanii hawahitajiki kuwa na uwezo wa kuimba live. Tukio la Mlimani City lilikuwa na wasanii wengi ambao walionekana kushindwa hata kuimba nyimbo zao wenyewe jambo ambalo linatisha sana.
Hofu ya Kisaikolojia na Aibu: Msanii anapojua hawezi, anaogopa. Hapo anaanza kuruka, kuongea na mashabiki, “mnaendeleaje Dar es Salaam”, ili kuficha mapumzi yanapokatika. Hii inafanya performance ionekane kama karaoke ya harusi.
Teknolojia Mbaya Jukwaani: Hata kama msanii anajua kuimba, monitor za sauti zilikuwa mbaya. Msanii hasikii anachokiimba, anasikia mwangwi wa ukumbi tu. Bila in-ear monitor, hata wasanii wa kimataifa wangefanya vibaya.
Mpango wa muziki ulionekana kuwa haujaangaliwa vizuri. Kuna mabadiliko ya ghafla kati ya wasanii, hakuna "flow" na nyimbo zilikuwa zikichezwa bila mpango wa kihistoria. Tukio la miaka 30 linahitaji kuwa na "musical journey" kuanzia mwanzo, kupitia kati, hadi mwisho.
NINGEPENDA KUONA:
Chronological set: Kuanzia nyimbo za mwanzo (1988-1990-2000) hadi za sasa.
Mash-ups ya wasanii wa zamani na wa sasa.
Tribute performances kwa wasanii walioaga dunia.
Live band inayoweza kucheza nyimbo za kila kipindi.
UHIFADHI WA HISTORIA "THE MISSING ARCHIVE".
Hili ndilo zao la dhahabu la tukio hili. Kama ilivyoandikwa na gazeti la Daily News, "hakuna hata picha moja ya albamu" iliyokuwa imehifadhiwa vizuri. Tukio la miaka 30 linahitaji kuwa na "archive exhibition" maonyesho ya kaseti za zamani, picha, poster, na hata mikrofoni iliyotumika. Hii sio tu kwa ajili ya wageni, bali ni kwa ajili ya vizazi vijavyo.
Tukio hili lilikuwa na uwezo wa kuwa na ujumbe wa kipekee, kwamba Bongo Fleva ni zaidi ya muziki, ni utamaduni, ni historia, ni utambulisho. Lakini ujumbe huu haukufikiwa vizuri kwa sababu ya utendaji mbaya wa wasanii na kupitia waandaaji wa ilo tamasha.
A. MUZIKI WA BONGO FLEVA UMEJENGWA JUU YA:
- Autotune na Melodyne: Programu ya kompyuta inayo pima na kurekebisha sauti ya mwimbaji ili ikae kwenye key sahihi ya muziki. Hurekebisha sauti zinazopinda au kutoka nje ya mdundo (off-key) ili ziweze kupatana na ala za muziki.
Wasanii wengi wa kisasa wanarekodi nyimbo zikiwa zimesafishwa sana kwa kutumia programu za kompyuta. Sauti zao zinapita kwenye vichungi vinavyorekebisha sauti (Pitch correction). Wanapopanda jukwaani bila msaada huo, mapungufu yao ya asili ya sauti (vocal pitch na key) yanajitokeza wazi.
- Vocal comping (kifupi cha composite tracking lengo ni kuchagua vipande bora na kuviunganisha).
Mambo haya yote na mengine zaidi ya hayo, yanayofanyika kwenye kurekodi na kuhariri sauti ya msanii akiwa studio, mara nyingi upelekea msanii kushindwa kuimba Mubashara ukilinganisha sauti yake halisi na ile iliyochakachuliwa studio.
B. KUTEGEMEA BACKING TRACKS:
Wasanii wengi wa kizazi cha Bongo Fleva, wamezoea kuimba juu ya playback na si Mubashara.
Ukosefu wa Mazoezi na Bendi (No Rehearsals with Live Band): Wasanii wengi hawana utamaduni wa kufanya mazoezi ya kutosha na bendi kabla ya shoo kubwa. Kuimba na "playback/CD" (Backing tracks) ni rahisi kwa sababu msanii anasindikiza tu sauti yake iliyopo kwenye CD. Live band inahitaji uwezo wa kusikiliza ala na kwenda nazo sambamba, stadi ambayo wasanii wengi hawana.
Wakati wasanii wengi hujitolea muda mwingi kurekodi studio, hawajitoi muda wa kutosha kwa mazoezi ya jukwaani. Kuimba live kunahitaji nguvu za ziada, kudhibiti pumzi, na kuwa na "Stage Presence" mambo ambayo hayapatikani bila mazoezi ya mara kwa mara.
Matumizi Mabaya ya Pumzi na Stamina Jukwaani: Wasanii wengi wanatumia nguvu nyingi kukimbia na kurukaruka jukwaani ili kuchangamsha mashabiki, jambo linalofanya wapoteze pumzi (breath control) haraka sana. Matokeo yake, wanaishia kuwaambia mashabiki "Imbeni nanyi!" au "Miko juu!" badala ya wao kuimba.
Wasanii wa Bongo Fleva, wengi hurekodi nyimbo zao kwa kutumia "digital audio workstations" (DAWs) ambapo wanaweza kurekodi sehemu moja mara nyingi hadi ikae vizuri. Hii inafanya kuwa rahisi kurekodi wimbo mzuri bila hata kuwa na uwezo wa kuimba vizuri. Lakini pale wanapokutana na jukwaa la live, ukweli huonekana
Sasa wanapolazimika kuimba live na band, matokeo yake, Tempo hubadilika, Key hubadilika na Phrasing hubadilika. Hapo ndipo changamoto inapoonekana.
C. UKOSEFU W MAFUNZO YA MUZIKI NA UIMBAJI.
Kuwa mtunzi mzuri si lazima uwe mwimbaji mzuri.
Kuna tofauti kati ya: Singer, Performer, Recording artist na Vocalist. Wasanii wengi wa Bongo Fleva ni recording artists. Sio wote ni vocalists wa kiwango cha juu.
Wasanii wengi: Hawajawahi kupata vocal coaching, Hawajui breath control, Hawajui projection na Hawajui kutumia microphone live.
- Wengi ni "vibe artists", na si "technical vocalists".
D. CHANGAMOTO ZA KIUFUNDI KWENYE MANYESHO.
Matamasha mengi ya Tanzania yanakabiliwa na:
Poorly mixed backing tracks, Bad monitors, Sound check za haraka, Backing tracks zisizoandaliwa kitaalamu na Ukosefu wa in-ear monitors.
Hivyo hata mwimbaji (Msanii) mzuri anaweza kuonekana anaimba vibaya.
E. NYIMBO NYINGI ZIMEANDIKWA KWA "STUDIO KEYS"
Baadhi ya nyimbo ziliimbwa miaka 15-20 iliyopita, kama si 30. Kadiri umri unavyoongezeka na ukosefu wa kuimba Mubashara, upelekea Vocal range hupungua na High notes huwa ngumu kuimba. Hivyo kuimba kwa key ile ile ya zamani huwa ni changamoto kubwa sana.
F. AUTO-TUNE: Imebadili matarajio ya wasikilizaji.
Leo watu wamezoea sauti iliyosafishwa, sauti iliyoboreshwa kutoka studio. Wanaposikia sauti halisi wanaweza kudhani msanii "hawezi kuimba", ilhali tofauti kubwa ni kwamba hakuna usindikaji wa studio.
F. UTAMADUNI WA TASNIA: Muonekano Zaidi ya Ujuzi.
Tasnia imejengwa juu ya Umaarufu, Mitandao ya kijamii, Drama (Kiki - Kick) na Maisha ya Kuiga Ufahari. Matokeo yake Sanaa ya Maonyesho ya Mubashara (live performance) imeachwa nyuma.
Nyimbo Zenyewe Hazijatengenezwa kwa Ajili ya kuchezwa au kuimbwa Mubashara (Live). Nyimbo nyingi Zina harmonies nyingi, Zina autotune kama sehemu ya utambulisho. Hivyo, kuziimba Mubashara ni changamoto.
4. UMUHIMU WA MAADHIMISHO MUBASHARA
Kwa Utamaduni wa Tanzania. Miaka 30 ya Bongo Fleva ni tukio la kihistoria kwa sababu:
Ni kumbukumbu ya safari ya vijana wa Tanzania.
Muziki huu umebeba Mapenzi, Maumivu, Ujanja, Ndoto na Uhalisia wa maisha ya mtaani.
Ni ushahidi wa nguvu ya Lugha ya Kiswahili. Bongo Fleva imefanya Kiswahili kuwa lugha ya muziki wa kimataifa.
Ni msingi wa tasnia ya burudani ya kisasa. Clouds, EFM, Wasafi na platforms nyingine zimejengwa juu ya msingi wa Bongo Fleva.
Ni utambulisho wa taifa. Kama Nigeria ilivyo na Afrobeats, Tanzania ina Bongo Fleva.
5. CREATIVE DIRECTOR'S CRITIQUE:
Nini Kilitokea, Kwa Nini, na Nini Kinahitajika.
Huu ni mtazamo wa wangu, uwenda pia wapenda mziki wengi waliliona hili, jambo moja tutakubaliana kwamba, tamasha la miaka 30 lilikuwa na mafanikio makubwa ya kihistoria, lakini limeonyesha maeneo ambayo yanaweza kuboreshwa ili kuifanya Bongo Fleva ionekane ya kiwango cha kimataifa.
DHANA ILIFIFISHWA: Jina “Miaka 30” ni kubwa, lakini ajabu muundo wa jukwaa (stage design) kulikuwa na bango moja tu. Hakukuwa na timeline ya picha, hakukuwa na video za archive, hakukuwa na storytelling. Creative direction ilitakiwa kuwa safari, kutoka kanda ya kaseti hadi streaming.
UBORA WA SAUTI: Hauwezi kuleta wasanii 20 na kuwapa mic moja ya wireless. Kila msanii alitakiwa kuwa na soundcheck ya dakika 30 na bendi moja ya Pamoja kabla ya onyesho, sio kila mtu na beat yake ya YouTube.
KURATIBU VIPAJI, SIO KUWAPANGA FOLENI: Walipandishwa kama wanafunzi wa shule, mmoja baada ya mwingine. Msmamzi mzuri angetengeneza medley, Chidi Benz anaingia kwenye kiitikio cha Dully, Dully anaingia kwa Fid Q anaingia kwa Nature, Nature anaingia kwa... Mtiririko usio na ombwe, ungeleta hamasa hata kwa watazamaji.
MAVAZI na BRANDING: Wakongwe walivaa vaa tu, kama wametoka mazoezini wengine kama harusini, shagala bhaghala. Hii ni sherehe ya miaka 30, ilitakiwa kuwa na dress code, “Smart Vintage”. Visuals ndizo zinazouza heshima.
KAMERA na LIVE STREAM: Kamera ya mjongeo Mubashara, ilikuwa moja tu ya kati, inatikisika, mchukuwa video akigeuza geuza kamera ili asipitwe na matukio. Mubashara wa kihistoria kulihitajika kamera kwa uchache 4, na ziwe zimeunganishwa na Sound system, kuwepo na msimamizi (mhariri) anayejua nini cha kukata wakati msanii anakohoa au kupiga chafya.
TATIZO HALIKUWA WASANII TU, BALI NI MFUMO MZIMA.
Tamasha lilionyesha:
Mandalizi ya live performance hayakuwa kiwango sawa kwa kila msanii.
Ukosefu wa vocal arrangement ya live, wasanii wengi walipaswa kuwa na vocal coaching, na hili ni tatizo kubwa, wengi wao walichukulia uzoefu na wengi wao walikuwa nje ya game kwa muda mrefu sana, kuliathiri ushirika wao kwenye steji, jambo ili lilipaswa liwe sehemu ya maandalizi kwa baadhi ya wasanii.
Mambo mengine ni Ukosefu wa rehearsal za kutosha, Ukosefu wa stage direction, Ukosefu wa band coordination na Ukosefu wa technical leadership.
Hili ni tatizo la mfumo, si mtu mmoja. Ikiwa wasanii wataendelea kutegemea playback badala ya kukuza uwezo wa live performance, hadhira ya kimataifa itaendelea kuwapiga pande kwenye matamasha Mubashara, ukilinganisha na Afrobeats, Amapiano na Rhumba ambazo mara nyingi huwekeza zaidi katika live shows.
Thamani ya matamasha ya moja kwa moja inaweza kupungua kwa mashabiki wanaotarajia ubora wa sauti na uimbaji. Wasanii wapunguze sana (Kama si kuacha kabisa) kutegemea beat ya studio.
MAANDALIZI YA TAMASHA HAYAKUWA NA “CREATIVE DIRECTION” YA KUTOSHA.
CREATIVE DIRECTION INAHITAJI: Storyline ya tamasha, Mood board ya jukwaa, Visual identity, Flow ya performances na Emotional arc ya tukio.
Kukosekana kwa hayo yote, kumepelekea Tamasha lilionekana kama mkusanyiko wa wanafunzi, wanaojifunza mziki.
MUSTAKABALI: Tunahitaji Mapinduzi ya Live Performance.
Ili Bongo Fleva iende kimataifa Zaidi Mubashara, Vocal training lazima iwe sehemu ya tasnia. Live arrangement lazima iwe standard. Sound engineering lazima iboreshwe. Wasanii lazima wajenge “live persona”. Tamasha lazima liwe kazi ya sanaa, si tukio tu la kukusanya wasanii na hadhira.
JAMBO MUHIMU
Miaka 30 ya Bongo Fleva si sherehe ya mafanikio tu, lakini pia ni mwaliko wa kujitafakari. Tamasha la Mlimani City limeonyesha uzuri na udhaifu wetu.
Lakini kama taifa lenye vipaji, tuna nafasi ya kuandika sura mpya, sura ya ubora, utamaduni, na ubunifu wa kiwango cha dunia.
Onyesho la “Miaka 30 ya Bongo Fleva” lilikuwa ni nafasi ya dhahabu iliyopotea. Lilifanikiwa kukusanya watu, lakini lilishindwa kusimulia hadithi. Lilifanikiwa kuwa sherehe, lakini lilishindwa kuwa tamasha. Kama kioo cha tasnia, lilituonyesha upeo wa huduma zetu za kiufundi na upeo wa uwezo wetu wa kisanii unapokuja kwenye utendaji wa moja kwa moja. Changamoto iliyojitokeza si tu kwa wasanii, bali kwa waandaaji: Je, tunaweza kuacha kusherehekea umaarufu na kuanza kuwekeza katika ufundi?
Je, kumbukumbu ya miaka 40 itakuwa ni ushuhuda wa ubora, au mwingilio mwingine wa huzuni?
Hii ni kazi ya ubunifu ambayo lazima ianze sasa, kwa kufufua heshima ya jukwaa na kumfanya msanii kuelewa kuwa jasho la mazoezini ni muhimu.
KURASIMISHA NA KUHESHIMU MUZIKI WA BONGO FLEVA
Tamasha hili lilikuwa uthibitisho kuwa Bongo Fleva si burudani ya kupita tu, bali ni sehemu ya urithi wa taifa (national heritage). Kupata sapoti ya viongozi na wadau wakubwa (kama tuzo zilizotolewa kwa Profesa Jay na Ruge Mutahaba) inaashiria utambuzi rasmi wa mchango wa sanaa hii kijamii na kiuchumi.
KUTUNZA KUMBUKUMBU ZA KIHISTORIA (Archiving History)
Katika nchi ambayo haina desturi kubwa ya kuandika historia ya muziki, kukusanya wasanii hawa Mlimani City kulisaidia kuwakumbusha vijana wa sasa asili ya midundo wanayoifurahia leo (kutoka Ragga, Rap, hadi Afro-Bongo ya sasa).
TIBA NA MARIDHIANO YA KIJAMII
Muziki wa Bongo Fleva unaleta watu pamoja bila kujali tofauti zao za kitabaka au kisiasa. Kuona jukwaa linawaunganisha maadui wa zamani au washindani wa muda mrefu kulionyesha nguvu ya sanaa katika kuunganisha jamii.
TATHMINI YA KISANII
1. MUUNDO WA JUKWAA NA MWANGA (Stage Design & Lighting)
Jukwaa lilikuwa na ukubwa mzuri (grand scale) kuendana na hadhi ya "Miaka 30." Hata hivyo, muundo wa picha za nyuma (LED visual backdrops) ulikosa usimulizi wa hadithi (storytelling). Kwa tamasha la kihistoria kama hili, kila msanii alipopanda, skrini kubwa zilitakiwa kuonyesha safari yake (picha za kumbukumbu, video za zamani) ili kuongeza thamani ya kihisia (emotional connection). Mwanga ulikuwa mzuri lakini ulikosa mabadiliko ya kishairi (thematic transitions) kuendana na midundo ya nyimbo za huzuni au furaha.
2. MTIRIRIKO WA SHOO (Show Flow & Pacing)
Hili lilikuwa anguko kubwa kiubunifu. Shoo ilichukua muda mrefu sana bila sababu za msingi na kulikuwa na "muda mfu" (dead air) mwingi kati ya msanii mmoja na mwingine. Kazi ya DJ na MC haikuwa imepangiliwa vizuri kiscript (scripted cues). Shoo ya kiwango cha kimataifa inatakiwa kuwa na mtiririko usiopumzika (seamless transitions) msanii mmoja anapoondoka, mwingine anaingia kwa mdundo wa kushitukiza (surprise entrance) bila kuharibu mzuka wa mashabiki.
3. UTENGENEZAJI WA SAUTI NA MAANDALIZI (Sound Engineering & Vocal Performance)
Sauti (Audio Mix) iliyosikika kwenye livestream haikubaliki kwa hadhi ya Mlimani City. Kulikuwa na mikwaruzo, sauti za vyombo kuzidi sauti ya msanii (instrumental drowning vocals), na vipaza sauti kukata mara kwa mara. Wasanii walitakiwa kulazimishwa kufanya mazoezi ya "vocal coaching" na kupimwa sauti (sound check) saa 48 kabla ya shoo. Kuruhusu msanii kupanda jukwaani na kuimba nje ya ufunguo (off-key) ni kuharibu chapa (brand identity) ya muziki wetu mbele ya watazamaji wa kimataifa waliokuwa wakifuatilia mtandaoni.
MAPENDEKEZO (Recommendation):
Ili kuleta heshima ya kweli kwenye shoo zijazo za mikoa:
Lazima kuwe na "Creative Scriptwriter" wa shoo nzima.
Kila msanii apewe muda maalum wa kutumbuiza (kwa mfano wa tuzo za Grammy au BET).
Kupiga marufuku matumizi ya sauti kamili ya CD jukwaani (Full Vocal Playback) wasanii lazima waimbe live kwa kutumia vyombo au "semi-live (backing vocals tu)."
HITIMISHO
Maadhimisho ya Miaka 30 ya Bongo Fleva ni alama muhimu katika historia ya muziki wa Tanzania na yameonyesha jinsi Bongo Fleva ilivyokua kutoka muziki wa mitaani hadi kuwa utambulisho wa kitaifa.
Hata hivyo, mjadala kuhusu ubora wa uimbaji wa Kimubashara (live) unapaswa kuangaliwa kwa tahadhari. Kwanini maonyesho mengi ya mubashara yalionekana kukosa ubora?
Sababu zinaweza kuwa mtambuka, yaani mchanganyiko wa maandalizi, teknolojia ya sauti, afya ya sauti, uzoefu wa live, na namna nyimbo zilivyotengenezwa studio na si kweli kwamba wasanii hao hawawezi kuimba.
Wasanii wafanye mazoezi ya kuimba Mubashara (Live) kwa sauti zao halisi, kama vile wafnyavyo waimbaji wa nyimbo za Taarabu na Mziki wa Dansi, wazalishaji (Ma Producer) wawekeze katika maonyesho halisi, na tasnia ijenge miundombinu bora.
Tamasha kama lingepata mkurugenzi mzuri wa ubunifu, na wakatumia muda mrefu wa maandalizi, basi lingeifanya tamasha liwe tukio la kimataifa, ili Bongo Fleva iweze kushindana kimataifa bila kupoteza asili yake. Hii ni fursa ya kukuza utamaduni wetu na kuwaachia vijana urithi wenye thamani.
Tulipoona wakongwe wakipanda jukwaani, tulitarajia machozi ya furaha. Tulipata ukweli mchungu. Bongo Fleva imekuwa na miaka 30 ya mafanikio ya kibiashara, lakini miaka 30 ya kushindwa kujenga shule ya mziki.
Tulijenga majina, hatukujenga misingi. Tulijenga hit songs, hatukujenga sauti. Ndio maana msanii anashindwa kuimba wimbo wake mwenyewe, kwa sababu wimbo huo haujawahi kuwa wake, ulikuwa wa producer.
Miaka 30 ya Bongo Fleva isitufanye tujipongeze tu. Itufanye tuulize, je, mtoto atakayezaliwa leo, akitaka kuwa mwimbaji mkubwa wa Tanzania miaka 10 ijayo, ataenda kujifunza wapi kuimba live? Jibu bado ni, kwa YouTube na bahati imwangukie.
Heshima kwa wakongwe wote waliofungua njia. Lakini heshima ya kweli sio kuwapigia makofi jukwaani, ni kuhakikisha kizazi kijacho hakiaibiki kama sisi tulivyoaibika kwenye live hii.
Bongo Fleva inahitaji sasa operesheni, sio kufunga bendeji kwenye uvimbe ulio ndani ya tumbo.
Ni matumaini yetu kuwa, Tamasha hili halita kuwa la mwisho, bali mwanzo wa sura mpya ya furaha na maendeleo katika muziki wa Bongo Fleva.
Bongo Fleva imefika mbali. Lakini safari bado inaendelea.
Thirty years was not a bad innings. It would be a terrible pity to lose the scorecard.





