Wednesday, 15 February 2023
Monday, 6 February 2023
GANDA LA HARAGWE KWENYE JINO
Huku kazini, tulikuwa na mkutano wa kuongelea ufanisi utakaopelekea natija kwenye kazi zetu za Kila siku. Nilikuwa ni mtakadamu kwa siku ile, kwa wanao wasilisha mada...
Kabla sijaingia kwenye chumba Cha mkutano, nikapitia maliwatoni, nikachua na udhu Ili nipate faradhi kabla ya mkutano kuanza. Wakati najiangalia kwenye kioo nikipaka mafuta kupunguza ukavu wa ngozi na baridi, wakati nafanya mkaguo, tahamaki nakenua kinywa, nakutana na twasira ya Ganda la Haragwe limeganda kwenye jino.
Kumbukumbu zangu, zilichelewa kidogo kusajili tukio la mimi kula maharagwe. Ni baada ya sekunde kadhaa, nikakumbuka kuwa nilikula maharagwe na tambi, takriban siku tatu nyuma.
Lile ganda lilinitafakarisha sana, kwanza nashukuru nililiona mapema kabla ya mkutano, maana ningekuwa kituko cha siku kama si wiki nzima, Alhamdulillah tahayuri iliniepuka.
Fikiria mtu unaweza kula chapati na MAHARAGE majira ya asubuhi, ukasindikiza na chai vikombe kadhaa... Ukasukutua kinywa mara tatu...
Mchana ukala ugali na nyama, Ukasindikiza na maji ya matunda, Usiku ukala zako boflo na chai tu...
Kabla ya kwenda kulala, ukapiga mswaki, meno umeyasugua vizuri, bila kusahau ulimi, ukausugua mpaka kwenye koromeo, kisha ukasukutua tena na tena...!
Asubuhi, kabla ya kuwahi kazini unasafisha kinywa kwa kusugua meno vizuri na kusukutua mara tatu, unafika kazini, unacheka na jamaa zako, ghafla tu, wanaona Ganda la Harage kwenye Jino lako la mbele, tena harage lenyewe ni la juzi...!
Kwenye tafakuri yangu, nikagundua mfanano wa sisi viumbe binadamu na Ganda la Harage kuganda kwenye jino.
Na ndivyo binadamu tulivyo, waweza kutendewa wema, ihsani na kila zuri, lakini si sababu ya wewe kutosengenywa, wala si sababu ya wewe kutochukiwa, fanya ufanyalo, utaingia midomoni mwa waja kwa njia hisiyo pendeza kwenye masikio yako.
Ndio, Kuna Viumbe Hapa Duniani, Wapo Kama Ganda la Haragwe...!
Hakika tumefanikiwa katika ili la kutopendana na kuhishimiana, tumefanikiwa kueneza chuki miongoni mwa jamii zetu, si Waislam, si Wakristo, si Wapagani, na huko kwenye siasa za Kisekula ndio kabisa kumeoza, kiasi tumekuwa mbilikimo wa kifikra, tumefanikiwa katika kugawanyika miongoni mwetu na sasa tupo zaidi kimakundi, na wale ambao hawapo kwenye makundi au jumuiya yetu basi huyo si mwenzetu.
Tutamtia midomoni kwa maneno ya uongo na kashfa, mpaka apate shinikizo la moyo na jirani yake mapafu, kama si la figo na maini yake...
Tabia hizi kwa kweli zimemea kwenye nafsi zetu na zimendoa mafungamano ya kirafiki na kindugu na kusababisha majadiliano yetu hukosa busara na hikma kiasi cha kupelekea kwenye utengano na uhasama ambao tunaweza kuuepuka.
Mnisamehe tu, uzee huu, yote haya sababu majuzi nilikula maharagwe, ganda likabakia siku nne kinywani, kweli jitihada haishindi kudura, na takadiri huwezi epuka.
Sunday, 8 January 2023

WAZIMU WA MADEREVA WA BODABODA
Wednesday, 4 January 2023
MBIOMBIO NIKAJIKUTA NALIKIMBILIA GARI LA KUZOA TAKA
Hivi Mwaka Mpya Huwa Tunasheherekea Nini Haswa, Kuzeeka!?
Saturday, 24 December 2022
WEWE UNGEFANYA NINI
NA UNGEJISIKIAJE!?

Hatoki Mtu Hapa... Mpaka Niupate...!
Sikukuu hii, nilipata mwaliko toka kwa sahibu yangu mmoja, hayati ya ujana wetu tulikuwa wanagenzi katika moja ya shule ya awali, jijini Dar, Gerezani, Kariakoo.
Sahibu yangu huyu imepita miaka mingi hatujaonana, kuonana kwetu ilikuwa kwa nasibu, wiki moja nyuma, nikiwa zangu kwenye harakati za hapa na pale, nikasikia sauti ya mtu anasalimia.
"Kakaa salamaa," akamalizia kwa kuniita jina langu... Kugeuka nakutana na sura ya mtu ninayo ijuwa, ijapo wajihi wake amebadirika, kiribatumbo cha haja, kama kabaila shamba. Lakini sura yake ingali ileile.
Tukasalimiana kwa bashasha, tukakumbushana mengi enzi tukiwa darasani, tukawakumbuka wanagenzi wenzetu waliokuwa watundu, na wale walimu visirani.
Tukaagana kwa yeye kunipa muhaliko, sikukuu hii, niende kwake kumtembelea, ili nami nipate nafasi ya kuiona familia yake, ana mke na watoto watatu.
Siku ikafika, nikachapa lapa, kiguu na njia, nikikatiza mitaa, ni mida ya adhuhuri, baada ya mshuko, jua si kali, ila fukuto la joto, lililotokana na wingu la mvua iliyogoma kunya, lilisababisha kero kidogo kwa wengi wetu tuliokuwa tukitembea kwa miguu, sako kwa bako kuelekea maeneo tofauti.
Baada ya kusubiri kwa dakika kadhaa kituo cha basi, nikapanda moja ya mabasi, maarufu kwa jina la Daladala, abiria ni wengi, siku kama hizi za sikukuu, wengi upendelea kwenda kwenye fukwe za bahari, kuvinjari, nadhani ndio sababu iliyopelekea wingi wa watu kwenye basi na haswa vichugandevu na watoto. Baada ya mwendo wa dakika zisizopungua 25, nikafika safari yangu.
Jamaa yangu ni mtu na familia yake, anaishi na mkewe na watoto zake kadhaa, pamoja na ndugu zake na wafanyakazi wa ndani.
Ma shaa Allah, nyumba yake nzuri, imezungushiwa ukuta mrefu wa futi saba na ushee, mbele kuna geti na kibaraza cha mlinzi. Nyumba imependeza na ina watu kiasi wasiopungua 8 kwa ujumla.
Rafiki yangu ni mtu mwenye uwezo wake kifedha nadhani kutokana na cheo chake serikalini...
Nimefika kwake nikakaribishwa vizuri kwa bashasha, baada ya salamu za hapa na pale, na mazungumzo haya na yale ya enzi tukiwa shule, huku tukijiburudisha kwa sharubati, nikaomba ruhusa niende msalani.
Uzuri wa hizi nyumba, vyoo, Maliwato na Mekoni ni humo humo ndani, wakati nipo msalani nikasikia sauti ya mkewe akilalamika kupotelewa kwa Mkufu Wake wa Dhahabu.
Sikujali sana, nikamaliza haja zangu, baada ya kujisafi, nikatoka zangu na kurudi varandani nilipokuwa nimeketi na mwenyeji wangu, nikawakuta wakazi wa nyumba ile wote wamekusanywa pamoja. Na mara mke wa sahibu yangu anawauliza kwa sauti alio wakusanya, nani kauchukua mkufu wake.
Kila mmoja anakataa, wanasema kuwa hawajui mahala wapi mkufu ulipo, naye bila ajizi akasema kwa ukali tena kwa sauti iliyobeba msisitizo wa herufi kubwa "HUMU NDANI HAKUJAWAHI KUPOTELEWA NA KITU HATA SIKU MOJA, MTANIELEZA LEO MKUFU WANGU HUPO WAPI! Na HATOKI MTU HAPA, MPAKA NIUPATE MKUFU WANGU!"
Nikaona baadhi ya macho yananitazama, ilihali mwenyewe najijua kuwa sina tabia za udokozi wala wivi...!
Nikajikuta nimepigwa na ganzi, mwili ukanisisimka kama mtu aliyeona mzimu wa mtu wa kale.
Nikawatazama na wao wakanitazama, nikamgeukia kumtazama mwenyeweji wangu, akakimbiza macho na kutazama pembeni, kukapita kimya cha sekunde kadhaa...
Nikajiuliza maswali mawazoni, nikakosa majibu, kisha nikakumbuka kuwa dunia ya leo, watu hawakosi majibu, Sasa Basi Kama Ndio Wewe Yamekukuta Haya, Ungefanya Nini?
Monday, 5 December 2022
NILIKWENDA KUNUNUA MWENYEWE DUKANI

Hivi Siku Hizi Bado Kuna Wanao Tafuna Tambuu!?

Hivi Siku Hizi Bado Kuna Wanao Tafuna Tambuu!?
Nipo Zangu Likizo, Ndani ya Jijila la Dar, Nakatiza Mitaa ya 'Uhindini' Karibu na Palipokuwa na Jumba la Sinema la Cameo, Lengo ni Kuelekea Walipokuwa Wakiishi Wakwe Zangu, Mtaa ya Kisutu.
Nikaikumbuka hii mitaa enzi hizo nikiishi mtaa wa Livingstone, walikuwa wakiuza sana Tambuu, ila ni ayami sasa sijaona 'Wahindi' wala 'Waswahili' wakitafuna Tambuu.
Zamani ukipita hii mitaa unakuta watu wanatafuna tu. Sasa usiombe jamaa awe anatafuna akiwa ghorofani halafu 'aipunguze' mdomoni wakati wewe unapita chini. Utasimulia.
Nikakumbuka kisa kilichonipata, miaka kadhaa nyuma. Nipo zangu nyumbani, mtaa wa Livingstone, Kariakoo. Miaka ile ya 80, bado kinda hata ubwabwa wa shingo bado kunitoka, sina hili wala lile. Hata sijui lile wazo lilikuja vipi, ila mpaka leo naamini kabisa, yaani haki ya Mungu tena, ndani ya mtima wangu kuwa; siku ile nilitembelewa na ibilisi wa Kibaniyani.
Tena atakuwa ni Mgujarati tu afiriti yule ayari, maana si kwa ushawishi ule ulionikamata, kiasi cha kushindwa kufikiria vizuri. Wala sikuwa na uraibu wa kula Tambuu, ila siku ile nilikamatika, nikajikuta nipo kiguu na njia kuelekea maeneo ya Kisutu, Uhindini.
Nikakatiza zangu Mnazi Mmoja, huyoo kiguu na njia, nikapita Mtaa wa Libya, mpaka makutano ya mtaa wa Libya na Zanaki, kisha nikachepuka kidogo kuingia mtaa wa Mtendeni, kisha nikaingia mtaa wa Mlima, kabla ya kukanyaga mtaa niliokusudia, mtaa wa Kisutu, dukani kwa Muhindi, Makaputura.
Ni baba wa Makamu, mnene haswa, kakaa dukani kwake, akipenda kuvaa kaputura akiishikiza kwa anjali, na ndio ikawa rakabu yake, Mzee/Babu Makaputura.
Duka limesheheni vitu kadhaa wa kadha, vimewekwa bila mpangilio maalum. Harufu ya Agarbatti inachomeka iliyowashwa mbele ya Ganesha na Lakshmiina, ina hanikiza kiasi cha kukera kwenye pua, harufu badala ya kuanisi ikawa inakera kiasi.
Akanitazama, bila ya kutabasamu, anafungua kinywa chake kunisemesha, huku nikishuhudia meno yake, yaliyobadirika rangi na kupata rangi ya Kahawia, iliyochanganyika na Chanikiwiti na mdomo wake uliojaa mate Mekundu kama damu kwa kula tambuu.
Kisha anatema mate mekundu yasiyopendeza, "Nini nataka veve", akaniuliza kwa rafidhi yake ya Kihindi, nami nikajikuta namjibu bila kufikiria, nataka tambuu, akanitazama kisha akaniuliza, "Nani Natuma veve tambuu" Kaka, nikamjibu, "Nambari gani iko nataka" nikamjibu, namba kumi na tatu, "Nambari Kumi na tatu, Taveja yeye" ndio babu, we nipe tu, ataiweza, nikamjibu. "Nataka gapi, bili, tatu inne" Moja tu inatosha.
"Haya subiri kidogo nategeza wewe, ile spesho kabisa, Tikee" uku akitingisha kichwa chake... Nikaitikia Tikee. Kulikuwa na majani ya Tambuu mezani, akachukua jani moja akalipangusa kidogo, kisha akaweka Popoo pamoja na chokaa kidogo juu ya jani la mtambuu, akaongeza na Tumbaku, Kungu Manga kidogo, Jagir gur na vikorokoro vingine wala sivikumbuki tena.
Akachana gazeti na kunifungia, "haya lete shiligi bili", nikampatia, kisha huyoo nikaongoza kurudi zangu, nyumbani. Nikapita mtaa wa Mrima, nikafungua kifurushi changu cha tambuu, nikabugia yote kinywani.
Sikumbuki kutema mate, kila yakijaa kinywani, nayameza kwa ule utamu wa ile sukari guru... Dakika si nyingi, nikaanza kuhisi Andasa ikipanda kidogo kidogo.
Afanaleki! Nikaanza kuhisi ubongo wangu haujatulia, harabu ya ile tambuu, yaani chugachugia, nilitia akili siku hiyo, dunia yote niliona kama inakwenda upande upande, nami nikaifatisha.
Kumbe walio niona siku ile wakastaajabu, wakapatwa na mpagao, mtu mfupi mie kwa jinsi nilivyokuwa nikitembea, kama mtu mwenye milonjo, maana si kwa miondoko ile ya mikogo.
Wakaja kuniuliza, siku ya pili yake, kumbe nilivyokuwa naangaika na andasi kichwani, na mwendo nikabadirisha, nikihisi barabara zimeinamia upande mmoja wa kushoto, nami ili nisidondoke nikajikuta natembea kuinamia upande wa kuume, natembea kama mtu aliyepigwa dafurao na lori la Jay Fong la mwaka 74.
Nilikuwa natembea kama Kaa au Ngadu, yaani nikitembea upande upande, siku hiyo niliongea lugha zote za Kihindi, Kibengali, Kigujarati, Kitelugu, Kiurdu, mpaka Kibanyani nilikijua siku hiyo... Kudadeki.
Hata nyumbani sikumbuki nilifikaje, nilijikuta tu nimepitiliza mpaka uwani, huku nimeshika kibatari nilichokiwasha, tena ni saa kumi jioni, mie naona giza.
Siku hiyo nilitapika mpaka nyongo... Nikanyororeka kama Kinyonga aliyelishwa ugoro...
Kuanzia siku hiyo nilikoma, sikutia mdomoni si Tambuu wala Kubeli au nduguye Pariki...
Friday, 2 December 2022
NILISHIKWA KWA TUHUMA ZA KUSAFIRISHA MADAWA YA KULEVYA.
Nilipo Ruhusiwa tu, Breki ya Kwanza Ilikuwa Maliwatoni...
Nipo Ndani ya Ndege, Aina ya Airbus, Tumehabiri Watu Wengi Sana, Hii ni Moja Kati ya Ndege Kubwa Sana za Abiria, Ndege Inamilikiwa na Shirika la Ndege la Falme za Kiarabu la Imarati (Emirates).
Nikitokea zangu ughaibuni moja kati ya nchi za Ulaya, naelekea zangu Afrika Mashariki kwa likizo fupi.
Nitakaa Dubai kwa siku kama tatu hivi, kisha baada ya hapo nitaunganisha ndege kuelekea kwenye nchi ambayo ndio kuna kitovu changu.
Ndio kwanza nimemaliza kuweka mzigo wangu kwenye Saraka (Dambra) ya kwenye ndege.
Kitu ambacho binafsi sikipendi sana na hii ni kwa sababu ya kimo changu, maana mimi si mrefu wa sifa wala si mfupi wa kuchusha.
Ghafla nikashikwa bega la kushoto, mshiko ule uliandamana na sauti kavu kidogo, ya mwanamke wa Kiafrika, mtu mzima, amekonga kiasi chake, kwa haraka haraka, nikakadiria umri wake, anapata miaka 60 au 65 hivi. Na kwa ile rafudhi yake, nikahisi kuwa anatokea Afrika Magharibi, na kama sikosei atakuwa tu ni Mpopo na kama si Mnaijeria basi ni Mghana.
Akaniomba nimsaidie kuweka begi lake kwenye saraka, yaani sehemu ya juu ya kuhifadhia mizigo.
Lakini ghafla kabla sijainama kuchukua mzigo wa yule bibi, mtu mmoja mrefu kiasi aliyekaa karibu nasi akajitokeza na kumsaidia yule mama mtu mzima.
Kila mtu akakaa kwenye kiti chake, wakati tupo angani, yule bibi akaanzisha mazungumzo. Alikuwa ni mzungumzaji mzuri, mwenye kujua mengi.
Nami kama kawaida yangu, napenda mazungumzo na haswa ninapogundua ninaweza kuelimika kwa namna moja au nyingine.
Tuliongea wakati wote, kiasi cha kuifanya safari ya saa tisa ya kwenda Dubai kuhisi imekuwa fupi sana.
Mara, sauti ya rubani ikasikikia kupitia kipaza sauti akitangaza kwamba tumeingia kwenye anga ya Dubai na muda si mrefu ndege itatua kwenye kiwanja cha ndege cha Dubai.
Ghafla yule bibi ambaye amefanya urafiki nami akanza kulalamika maumivu ya tumbo.
Nami kwa uungwana niliokua nao nikiongozwa na moyo wangu uliojaa huruma kwa yule ajuza, nilibonyeza kitufe cha msaada, na muhudumu wa kwenye ndege akaja kutusikiliza, akataka kujua shida ni nini.
Nikamwambia kuwa jirani yangu hakuwa anajisikia vizuri.
Lakini cha ajabu yule bibi, ghafla alianza kuniita mimi kuwa ni kijana wake (My son, my son...), na uku akiwa amenikamata mkono, hakutaka kuniachia.
Msimamizi akaniambia kuwa hakuna kitu wangeweza kufanya zaidi ya kumpa dawa za kupunguza maumivu na tusubiri hadi tutakapotua.
Yule muhudumu akamtaarifu rubani, naye rubani akatangaza kwamba tumepatwa na dharura ya mgonwa ndani ya ndege na akatushauri sote tutulie na tusiwe na wasiwasi kwani yule mgonjwa atahudumiwa.
Yule bibi alikuwa akilia na kutokwa na jasho kama vile aliyemwagiwa ndoo nzima ya maji.
Nikajaribu kuuachanisha mkono wake na wangu, lakini yule bibi alikataa kuniachia mkono wangu... Kila mtu alidhani kuwa mimi na yule bibi wa Kipopo ni mtu na mwanae.
Ndege ilipokwisha tua na kusimama, yule kijana aliyesaidia kuweka mzigo wa yule bibi kwenye Saraka, aliondoa mzigo wake, kisha akasaidia tena kushusha sanduku la Bibi Mpopo na kuliweka kwenye kiti.
Yule jamaa kabla ya kuondoka alininong’oneza kwa kunishauri nijitenge mbali na huyu bibi na niwaambie wahudumu wa ndani ya ndege kuwa mimi na yule bibi hatukusafiri pamoja.
Wafanyikazi wa kwenye ndege waliniuliza kama tuna uhusiano na bibi yule, niliwaambia kuwa tumekutana kwenye ndege. Sikumjua kabisa kabla...
Wakati naondoka nikamuaga na kumtakia kila la kheri, lakini yule bibi aliniomba nimsaidie kumbebea mkoba wake.
Lakini yule jamaa aliyemsaidia kuuweka mzigo kwenye saraka ya kwenye ndege aliniangalia, tukatazamana machoni, nikamuona akitikisa kichwa kwa msisitizo. Nikamuelewa!
Tukawaachia wahudumu wamsaidie.
Basi mimi na abiria wengine tukatoka ndani ya ndege na kumwacha bibi wa Kipopo anasubiri kiti cha magurudumu.
Nashuru niliweza kujikongoa kutoka kwa yule bibi, baada ya waudumu kufika na kumsaidia mizigo yake na yeye akawekwa kwenye kiti cha matairi.
Tulipokuwa tukingoja mizigo yetu, tukasikia sauti kali ikiamuru "... Stop, Stop! You are Under Arrest...!"
Nageuka kuangalia kumbe anayeambiwa asimame na kuwa amewekwa chini ya ulinzi ni yule bibi wa Kipopo alikuwa akikimbia, akijaribu kuwatoroka Askari na wafanyakazi wa kwenye ndege.
Kumbe walipo mshusha tu, tumbo lilipona ghafla na mara moja na akasimama na kuanza kukimbia uku akimuachia mkoba mmoja wa wafanyakazi wa kwenye ndege, na kukimbia kuelekea nje...!
Kwa bahati nzuri polisi wa uwanja wa ndege walikuwa na kasi kuliko yeye. Walimshika na kumrudisha uku wamemvisha pingu za mikono.
Bibi wa Kipopo bila haya wala soni usoni akaanza kuniita tena... "My son... My son, ooh! How could you do this to me, ooh...!"
Mwanangu ... Mwanangu! Unawezaje kunifanyia hivi...!
Ndio sasa nikaelewa na fahamu kunirudia uzuri, kumbe bibi alikuwa amebeba dawa za kulevya na alikuwa akijaribu kunihusisha na mimi, ili yeye apate upenyo wa kutoroka!
Kwa bahati nzuri, yule bwana ambaye alikuwa amemsaidia kushusha mzigo wake toka kwenye saraka, alijitokeza na kuwaambia polisi wa uwanja wa ndege kuwa mimi na yeye (Bibi wa Kipopo) tumekutana tu kwenye ndege.
Polisi walichukua pasipoti yangu na kumwuliza yule bibi ataje majina yangu kamili ikiwa ni kweli mimi ni mwanae na tulikuwa tukisafiri pamoja.
Kwa neema ya Mungu, sikuwa nimemwambia hata jina langu la kwanza, bibi wa Kipopo akabakia tu anag’aa ng’aa macho! Uku akiendelea tu kusema "...he is my son, ...he is my son, ooh!"
Hata hivyo Polisi wakanitaka nifuatane nao kwenye chumba kidogo ambapo nilihojiwa sana.
"Nilikutana naye wapi? ...Nilipanda wapi...? Huyo bibi alipanda wapi...!?" Na maswali mengine mengi ya kimtego.
Na mizigo yangu yote ilipekuliwa na kuchambuliwa sana, wakachukua alama za vidole vyangu ili wakaangalie kama nilisha wahi kukamatwa...!
Taarifa za kipolisi zilipokuja, alama zangu za vidole hazikupatikana popote, si kwenye mizigo ya yule bibi wala kwenye kazidata za Kipolisi!
Niliruhusiwa kuondoa baada ya takribani saa tatu za mahojiano, maana hata mwenyeji wangu alisha anza kukata tamaa.
Hakuna siku nilijawa na hofu kama hii siku, na haswa kama ujazoea maswala ya kukamatwa na polisi, tena basi nikiwa nchi ngeni, nchi ambayo kesi za dawa za kulevya hukumu yake ni kifungo cha muda mrefu kama si cha maisha, kwa kweli nilichanganyikiwa...
Nilipo ruhusiwa tu, breki ya kwanza ilikuwa ni maliwatoni, uko niliharisha kweli kweli, nadhani ni ule woga na fikra zilizonizonga kuwa sasa ndio basi tena, naiwacha dunia kizembe...!
Tangia siku ile nikajifunza jambo moja, la kutogusa mzigo wa mtu yoyote yule. Labda mzigo uwe wa familia yangu na nimeupakia na kuufunga mwenyewe...
Zaidi ya hapo hata sijali, tena nimeapa kabisa, Haki ya Mungu tena, sikusaidii, nimekukuta uwanja wa ndege na mizigo yako hata ikiwa unayo mizigo iliyo kuelemea au umekongeka ukakongoroka utaibeba na kuishughulikia wewe mwenyewe.
Sitakupa hata toroli ya kuweka mzigo wako!
Mizigo yako... shida yako... Hiyo ndio sera yangu mpya safarini.
Na kama ni ndani ya ndege na ikiwa huwezi kuifikia sehemu ya kuwekea mizigo, kwenye saraka, na ikatokea kuwa mimi ndiye mtu wa karibu zaidi, nitakachoweza kukusaidia ni kukuambia umwite muhudumu wa kwenye ndege akusaidie...!
Maana Nazi Mbovu Harabu ya Nzima.
Nawatakia Wasafiri, Safari Njema...!
Tuesday, 29 November 2022
NILIKESHA NIKIMTAFUTA
Tukio Linalo Fanana na Ukweli!
Friday, 11 November 2022
BIRIKA BATI, KIKOMBE BATI,
NA HATUKUKOMA.

Hivi wakulaumiwa walikuwa watengenezaji au wanunuaji au watumiaji!?
Yaani hata sielewi, vikombe gani vinaunguza namna ile? Au walikuwa wanatukomesha tukivunja vikombe vya udongo!?
Halafu kikombe cha chai, ila kinapicha ya nyanya. Sikuvipenda, sivipendi, sitavipenda.
Na kwa nini nivipende, uwenda hivi vikombe ndio vimetukomaza midomo tukiwa bado makinda.
Nahisi ndio maana Watanzania tumekuwa watu wa kupiga sana stori... Sasa wewe fikiria chai ya moto, kuiwacha huwezi, hapo sasa ni stori tu, kumbe janja yako unavizia ipowe, hapo ni stori plus umbea na mikingamo.
Basi nikwambie, siku hiyo nikamtembelea binamu yangu wa kike maeneo ya Magomeni, nikitokea zangu maeneo ya Gerezani, Kariakoo, chini nimevalia viatu vyangu vya Kung Fu shuzi, medini Chaina. Shati langu la Juliana, picha ya ndege, kubwa kiasi na chini nimevalia suruali yangu ya kodrai.
Mtu mimi na ufupi huu, ukiniona kwa mbali, utafikiria nguo zatembea zenyewe. Huyoo kiguu na njia, nikakatiza zangu Jangwani, na jua lile la saa tisa alasili. Kufika home kwake, kanikaribisha uwani, nyumba nzima yupo peke yake, wapangaji wapo mitaani, awajarudi bado.
Kanikaribisha kwenye Kigoda, baada ya salamu na kujuliana hali akanikaribisha chai ya mkandaa, akanitilia kwenye kombe la bati, chai imekolea viungo, inawasha kwa karafuu na tangawizi, ikakolezwa na pilipili mtama, chai kama uji wa mgonjwa na mie ujanja ikawa ni kupiga stori za kupoza chai, fu fu fuuu, nyiingi!
Japo tupo uwani, lakini joto la saa tisa, jiji Dar nalo halikuniwacha, utafikiri nimemwagiwa maji, mara akanyanyuka na kuniita niende chumbani kwake...!
"Binamu njoo chumbani nikuonyeshe mambo, ila nakuonya usimwambie mtu..."
Ghafla nikajikuta nameza mate machungu, nahisi nilitaka kutema nyongo, ikaishia kohoni, chai kidogo inipalie, nilajikuta naimeza bila kujua kuwa naunguza kolomeo.
Nami bila ajizi nikajikuta nipo chumbani, hata sijui nimefikaje, maana fahamu zikikuwa zinaingia na kutoka...
Hakuna pa kukaa ila kwenye kitanda, mwenyewe katandika mashuka yake ya kufuma kwa mkono, maua ya rozi (mawaridi), kafanya seti kamili, mapazia ya dirishani na mlangoni. Vingine kafunikia radio yake, kaseti aina ya National na kitambaa kingine kakitandika kwenye meza.
Pembeni ya chumba kuna mtungi wa maji, umefunikwa na sahani ya bati na kata yake imewekwa pembeni kidogo, picha za wanamuziki wa Boney M na ABBA group zilizokatwa kutoka kwenye magazeti ya Sunday News zimebandikwa ukutani, pamoja na picha ya Buraku, kafanana na mwanamke wa Kihindi.
Kwenye meza kuna viboksi viwili vitupu vya sabauni ya Lux na lifebuoy pamoja na kibox cha dawa ya kusugulia meno ya Colgate. Pembeni kidogo, kuna kabati la vyombo lenye wavu, na kabati la nguo lenye kioo.
"Kaa basi hapo we nawe wima wima tu, kama mgambo wa site" sauti yake ikakatiza mawazo yangu yaliokwenda mbali ya hapo, maana mawazo yalikuwa mbingu ya sabaaa nacheka na kufurahi na malaika wa peponi.
Nikakaa kitandani, moyo unakwenda kasi kama wa Mbayuwayu... Akanitazama kisha akanambia, huku kaweka umakini usoni, yaani yupo siriasi kabisa... "binamu hii iwe siri yetu, ukimwambia mtu, mi na wewe basi tena sitakushirikisha kwenye mambo mazuri haya."
Nikahisi masikio ghafla yamenisimama wima kama mbwa wa msasi kaona windo, nikanyoosha na shingo kama Njiwa Manga...
Nikahitikia kwa kutingisha kichwa, akanambia "Apiya binamu, kuwa hutotoa siri, sema Hakiyamngu..." nikajikuta natamka, kwa kigugumizi, kilicho nikamata, hata kilipotokea sijui...
"Ha-ki ya M-ngu tttena, si-si-mwambii m-mtu mi mi-ye, Waalaahi Nakuapia, mmmh na mchanga huu naramba." Huku nikiinama na kwa kutumia kidole cha shahada, nikapangusa sakafu na kuramba...
Moyo ukaongeza kasi kama garimoshi la Mjerumani kwenye vita kuu ya kwanza ya dunia sanjari na tumbo likapata kusema, gruuuh.
Akanitazama kisha akanambia: "Haya mie nakuamini voo binamu yangu, najuwa we mambo yako ya kizungu, ndio mana nakupendaga..." Akatamka huku anaelekea kabatini kwake na kufungua kabati...
Hamadi, katoa doti tatu za vitenge vya wax na kuvirembea pale nilipo kaa, kitandani. Enzi hizo tukuvihita vitenge vya Burundi.
"Nimeletewa jana na shemejio..." Sauti yake ikaanikiza pale chumbani.
Nikamuuliza, Mmm! Shemeji yupi huyo...!? Yule mjeshi wa Ngerengere!?
Akanijibu: "Uwachi na wewe, wa Ngerengere wapi!? Yule nishamtosa siku nyingi... Huyu humjuhi wewe, mwenyewe anafanyakazi bandarini, hivyo vitenge vya Magamu (Magendo), vilikuwa vinapelekwa Burundi kontena nzima, yeye ndio kavinyakua hivi vitatu, kaniletea nimuuzie."
"Kimoja shilingi 25, ila kwa wewe binamu yangu, nitakuuzia kwa shilingi 22, na wewe ukauze upate faida japo kidogo."
Nikamtazama, kisha nikapiga fundo moja la chai ya moto, yaani hata sikuhisi kuunguzwa, hiyo midomo na koromeo nilikuja kuhisi nimebabuka, usiku wake nisharudi nyumbani.
Ghafla nikajihisi kama biskuti ndani ya chai ya moto au kiowevu, nikawaza mfukoni nina shilingi Moja ya Mwenge na sumni tu ile ya sungura...
Enewi, yalikuwa tu maisha yenye changamoto zake, furaha, uzuni, vicheko vyote vilikamilisha uhalisia wa maisha yetu, hatukuacha kutembeleana, japo bidhaa muhimu zilikuwa adimu... kula kwa kaya...
😉ðŸ¤ðŸ¤£
Tuesday, 8 November 2022
LIKIZO YANGU, JIJINI DSM (DIZIM)

Na Kumbukumbu Iliyopotea
Nilipokuwa likizo jijini Dar es salaam, nikajikuta tu nimepata hamu ya katembelea kwa miguu, mitaa ya Gerezani, Kariakoo. Nikapitapita mitaa iliyosongamana watu wa kila aina, nikakumbuka kufuchama Rununu yangu, kwa kuchelea wivi, wasijeichukua bila ruhusa yangu, huku sauti za wabeba mizigo wakiyosayosa maneno ya kutiana nguvu, nikapishana na wenyeji wachache sana, wakihisabika kwa vidole vya mkono, wengi wao ni wageni.
Huyo nikayoyomeka zangu, nikajikuta natokea mtaa wa Nkrumah, taratibu nikashuka zangu mwelekeo wa Mnara wa saa, nikatupa macho upande wa kushoto nikasoma kibao, kilichofubaa kwa rangi baada ya kutelekezwa miaka dahari, neno NEW CHOX bado likisomeka, kumbukumbu ikarejea miaka mingi nyuma, nikatabasamu sanjari na kusikitika, maana umuhimu wa jengo hilo kwa sasa haupo tena, nani anakwenda sinema siku hizi!?
Hata ile hoteli ya Continental sina uhakika kama bado inatoa huduma, nakumbuka tulikuwa tukienda kucheza Disco na vijana wenzangu.
Nikakumbuka hata wale wakaazi wa vitongojini, nao hawakuachwa nyuma, serikali iliwafungulia vituo vya burudani vya kijamii, kwa wakazi wa jiji la Dar, watakuwa wanakumbuka majumba ya DDC, kama vile Amana Social Hall, DDC Kariakoo, Keko na pale Magomeni.
Pale Ilala awali ilikuwa pia ni mahali ambapo wengi wakienda kungalia sinema siku za mwisho wa wiki na siku za sikukuu. Kiufupi majumba haya ya jamii, yalikuwa nchi nzima.
Nikakumbuka kuna jumba moja lilikuja mwishoni, katika miaka ya 80, jumba ambalo ndio lilikuwa jumba lenye uwezo wa kuingiza watu wengi sana, likijulikana kwa jina la Star Light Cinema.
Kiukweli hii ni kumbukumbu nzuri na ya kuuzunisha, maana enzi hizo kweli ilikuwa jambo la tunu sana kwa mtoto au hata mtu mzima kupelekwa sinema.
Kwanza halikuwa jambo rahisi kwa mtu tu asiye na ubavu kupata tiketi, haswa filamu ikiwa ni mpya na waigizaji wakiwa ni maarufu.
Nakumbuka walanguzi wa tikiti za sinema, vijana kwa watu wazima, wenye nguvu zao, wengi wao weshatangulia mbele za haki, walikuwa wakimaliza kulangua pale New Chox sinema, walikuwa wakikimbilia Avalon sinema, alafu sasa pale kidirishani, tikiti zilikuwa zikiuzwa nusu, kisha zilizobakia wale Wahindi wakiwapa watu wao na kuziuza kwa bei ya juu.
Nikajikuta natabasamu, kumbukumbu iliyokuja baada ya hapo, nikatamani kucheka, maana siku hiyo pale Chox niliwahi kidirishani kabla ya dirisha la kununulia tikiti halijafunguliwa, nikajuwa leo napata tikiti tena zile siti za nyuma kabisa, kama si mstari A basi D.
Ghafla lango likafunguliwa kuruhusu watu waingie kununua tikikiti, sanjari na dirisha la kuuzia tikiti, hamadi nikajikuta hewani kama Sapatu, nimepigwa kibega kimoja tu, nikajikuta nimetupwa huko karibia na vyoo, chali kama mtoto wa Komba kaanguka mtini.
Nikajizoazoa zangu, nikabakia nimetumbua zangu macho kama mtu aliyekabwa na nguto, kumeza siwezi wala kutema ziwezi.
Enewei, pale jumba la sinema la Empire nako wakimaliza kuuza, walikuwa wakienda zao Empress, Ila jumba ambalo vijana wengi wakilipenda ni jumba la Empire kwa sababu walikuwa wakionyesha sinema nyingi za hollywood, na waendeshaji walikuwa na tabia ya kuongeza sauti haswa wakati wa mapigano, ili kuwakoleza watizamaji.
Majumba ya Cameo (Mtaa wa Jamhuri,) na Odeon (Mtaa wa Zaramo na Jamhuri) haswa yalikuwa maarufu kwa sinema za Kihindi, wakifuatiwa na New Chox Cinema (Mtaa wa Nkuruma) na Avalon (Mtaa wa Zanaki) na Empress (Mtaa wa Samora) alafu ndio Empire (Mtaa wa Azikiwe).
Kule Msasani, kulikuwa na jumba la sinema, likitwa Drive-Inn, wakiingia na magari yao, ila wakazi wa Msasani wengi walikuwa wakijazana nje ya ukuta na kutazama sinema, japokuwa hawakuweza kusikia sauti lakini wengi wakiridhika na hiyo hali.
Nakumbuka kumtembelea Marehemu, ndugu yake na baba, mitaa ya Msasani, sasa ndugu yangu mmoja (yeye ni mkubwa kuliko mimi, naye pia ni marehemu), akanipa ofa bubu ya kwenda kutazama sinema, ah ah ah ah, akanipeleka Drive inn, kufika tukakaa nje ya ukuta na kununu zetu karanga na maji ya sharubati, tukatafuta tofali na box chakavu kisha tukaa kuangalia movie, tukisumbuliwa na mbu hapa na pale.
Sikumwambia kitu maana nilikuwa nikimuheshimu, mwenyewe nilishazoe kwenye majumba yetu ya kawaida, kama ukishindwa kununua tikiti basi unafanya kila njia kupenya au unampa pesa kidogo mwangalizi wa tikiti na kukuingiza ndani, ila kama jumba limejaa, basi unakaa kwenye ngazi za kutokea nje... Ah ah ah ah, ama kweli siku hazigandi.
Vijana wa leo wanaweza kushangaa wakisikia kuwa hata wimbo wa Taifa ulikuwa ukipigwa kabla ya onyesho, ila baadae sana ikaja kuondolewa kwa sababu ilisemekana kuwa hakukuwa na heshima, sababu wengine walikuwa ni walevi na hawakuwa wakisimama wima pale wimbo wa Taifa unapopigwa.
Hii biashara ya sinema ilikuja kuanza kudorora vilipoanza vituo vya Runinga na kushamili kwa biashara ya kuazimana kanda za video, na maktaba za kukodisha kanda za video, hizo zilikuwa enzi za Mzee Ruhsa.
Wengi walikuja kupendelea kukodisha kanda za video kuliko kwenda kwenye majumba ya sinema kwa sababu kwanza ilikuwa ghali kwa mtu mwenye familia, kugharamia watu zaidi ya wanne, pili filamu zenyewe nyingi zilikuwa baadae zikirudiwa rudiwa, nadhani shirika la filamu Tanzania lilikuja kufirisika na kushindwa tena kuagiza filamu mpya.
Haya majumba ya sinema, siku za mwisho mwisho walikuwa wakionyesha filamu mbili mpaka tatu kwa malipo ya kutazama filam moja, yaani ilikuwa ni kukesha, maana zilikuwa zikianza usiku.
Nakumbuka filam moja ya kihindi ilitamba sana katikati ya miaka ya 70 na mwanzoni mwa miaka ya 80, filam yenyewe ilitoka mwaka 1975. Ilitwa Sholay, hii filam Wahindi wa bongo walichapisha mpaka fulana zake na kuziuza!