Tuesday, 26 May 2026

 JE, NI MASLAHI BINAFSI, UKOSEFU WA MSIMAMO AU 

KUPUUZA HISTORIA YA MAUAJI TANZANIA?

Kuhama chama si dhambi. Dhambi ni kuhama misimamo, kuhama ukweli, na kuhama dhamana kwa wananchi. Historia ya mauaji inatukumbusha: cheo ni dhamana, si kinga. Mwanasiasa anayepuuza historia hii, leo akisifia, kesho akilaani, huyo anapigania tumbo lake tu.

Wanasiasa wa Tanzania wanapaswa kutambua kuwa historia itawahukumu vikali. Kitendo cha kuweka mbele maslahi ya matumbo yao na kuwa tayari kugeuka geuka kiitikadi kinazidi kuchelewesha upatikanaji wa Katiba Mpya na Tume Huru ya Uchaguzi, vitu ambavyo vingemaliza kabisa mzunguko huu wa ukatili na mauaji kila msimu wa uchaguzi. Bila kuwa na viongozi wenye msimamo thabiti (kama ule wa uwajibikaji wa Ali Hassan Mwinyi wa mwaka 1976), siasa za Tanzania zitabaki kuwa biashara ya watu wachache, huku raia wa kawaida wakiendelea kuwa wahanga wa upepo wa kisiasa.

---

1. UTANGULIZI:

SIASA HAINA ADUI WA KUDUMU” – KAULI AU KISINGIZIO?

HAMAHAMA YA WANASIASA: Katika siasa za Tanzania hasa vyama vya siasa viliporuhusiwa au kurejeshwa tena, kumekuwa na wimbi la wanasiasa kuhama vyama, leo yupo chama fulani, kesho anarudi au kuhamia kingine. Swali kuu linabaki: je, hii ni ishara ya demokrasia yenye afya au ni dalili ya kukosekana kwa misingi, msimamo na uwajibikaji wa kisiasa?

Swali la Msingi: Wanatafuta Nini?

Ni kutafuta maslahi binafsi (matumbo), ukosefu wa msimamo thabiti, au kupuuza historia ya mauaji na ukandamizaji wa kiutawala nchini?

Mjadala huu hauwezi kukamilika bila kuangalia historia ya nchi, hasa matukio mazito ya kiusalama na mauaji ambayo yalipaswa kuwa somo kwa wanasiasa wa Tanzania ili kujenga misimamo thabiti.

SIASA ZA KUHAMAHAMA VYAMA: UHURU AU MASLAHI?

Kihalisia, katiba na sheria za vyama vya siasa zinamruhusu mwanasiasa kuchagua chama anachotaka. Hata hivyo, changamoto ipo kwenye nia na muda wa maamuzi hayo.

Kwa mujibu wa wachambuzi, wanasiasa wanaohama wamegawanyika makundi mawili:

  • WENYE MISINGI NA ITIKADI: Wanahamia chama chenye maadili wanayoamini. Ni Wanasiasa wachache sana, huhama kwa sababu za sera na mwelekeo.

  • WAPENDA MASLAHI BINAFSI: “Popote panapo maslahi watakwenda”. Hawa ndio waliozua msemo “Siasa Haina Adui wa Kudumu” kauli ambayo kwangu mimi naiona kama upuuzi na ulaghai.

Hawa ni wenye siasa za matumbo; hutanguliza maslahi binafsi kuliko maslahi ya wananchi. Hawa ndio wanaoleta mashaka makubwa kwa jamii. Wanapokuwa nje ya mfumo, huikosoa serikali kwa nguvu zote. Lakini wanapopata nafasi ndani ya mfumo huo huo:

  • Hawakatai uteuzi.

  • Wananyamaza au kubadilika ghafla.

  • Baada ya kuondolewa madarakani, hurudi kuwa wakosoaji wakubwa.

Tatizo linakuja pale mwanasiasa anapokuwa serikalini: anasifia mfumo. Akiondolewa au kumaliza muda, ghafla anakuwa mkosoaji mkubwa. Hii inazua maswali: je walikuwa wanaficha ukweli wakiwa madarakani? Au walikuwa wanakula keki kimyakimya?

2. HISTORIA YA MAUAJI YA KISIASA TANZANIA:

Na Athari Zake Kisiasa, Kwa Nini Inapaswa Kukumbukwa.

Kabla ya kumhukumu mwanasiasa anayehama, ni muhimu kuweka mizani ya historia ya damu iliyomwagika. Historia hii ndiyo inayopaswa kutengeneza misimamo ya viongozi.

2.1. Mauaji ya Shinyanga 1976 na Kujiuzulu kwa Ali Hassan Mwinyi.

Julai 1976, yalitokea mauaji mkoani Shinyanga. Ali Hassan Mwinyi, akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, alimuandikia Rais Mwalimu Nyerere barua ya kujiuzulu uwaziri. Alisema “Hakuna sababu ya kiongozi kujiuzulu baada ya kutokea mauaji” lakini yeye aliona ni wajibu kuwajibika.

Uamuzi huo ulimjengea heshima na baadaye mwaka 1985 akawa Rais wa Awamu ya Pili.

Somo hapa tunaona mfano wa uwajibikaji wa kisiasa, jambo ambalo siku hizi lhalipo. Leo, viongozi wangapi wako tayari kuwajibika mauaji yanapotokea?

2.2 Mauaji ya Mwembechai, 13 Februari 1998

Siku ya Ijumaa, 13 Februari 1998, polisi wa FFU walifyatua risasi kwa waumini wa Kiislamu Msikiti wa Mwembechai, Dar es Salaam. Angalau watu wanne waliuawa. Tukio lilitokana na mchungaji wa Kikatoliki kudai Waislamu walikuwa wakimkejeli Yesu, madai yaliyothibitika kuwa ya uongo.

Waziri wa wakati huo wa Mambo ya Ndani, Ali Ameir, alisema hali hiyo ilikuwa moja ya changamoto kubwa alizokumbana nayo.

Hili lilizua:

  • Maswali juu ya matumizi ya nguvu za dola

  • Hofu ya mgawanyiko wa kijamii

  • Wito wa uwajibikaji wa viongozi

Tukio hili liliibua maswali kuhusu uhuru wa dini na matumizi ya nguvu kupita kiasi na vyombo vya usalama.

Lakini, je, wanasiasa wa leo wanajifunza nini kutoka hapa? Au wanalitumia tu kama silaha ya kisiasa wanapokuwa nje ya madaraka?

Muda baadae, Msomi ambaye hapendi kuitwa Profesa, aliekuwa mhadhiri muandamizi Udsm, Professor Hamza Mustafa Njozi, akaandika kitabu "Mwembechai Killings and the Political Future of Tanzania" ni kazi inayochunguza mauaji ya Mwembechai ya mwaka 1998 jijini Dar es Salaam na kuangazia athari zake pana kwa haki, demokrasia, na utulivu wa kisiasa nchini Tanzania.

Kitabu kilipigwa marufuku kuingia nchini wakati wa Rais Mkapa.

Serikali ilikataa uchunguzi huru na ikapiga marufuku mkutano wa wanawake wa Kiislamu waliotaka kuzungumza unyanyasaji waliopata rumande. Mwembechai ikawa alama ya ubaguzi wa kidini na matumizi mabaya ya dola.

2.3 OPERESHENI MKIRU - (Mkuranga, Kibiti, Rufiji) 2013-2017

MKIRU ni kifupisho cha Mkuranga, Kibiti NA Rufiji. Hayo ni maeneo yaliyokumbwa na mauaji ya polisi na viongozi wa serikali kuanzia 2013.

Eneo la Pwani ya Tanzania, lilishuhudia mfululizo wa mauaji ya askari polisi na raia. Serikali ilianzisha Operesheni MKIRU ili kukabiliana na kile kilichoitwa ugaidi au uhalifu uliopangwa. Operesheni hii ilitumia ujasusi mkubwa na ilifanikiwa kupunguza matukio hayo.

Hata hivyo, ilizua madai ya ukiukaji wa haki za binadamu.

Chanzo kikuu kilichotajwa:

  1. Chuki za wananchi dhidi ya polisi: 23 Januari 2013, mkazi wa Kibiti alifariki Muhimbili kwa madai ya kupigwa na polisi. Wananchi walifunga Barabara ya Kilwa kwa zaidi ya saa 3 na kuchoma kituo cha polisi.

  2. Unyanyasaji wa kiuchumi: Ripoti ya Mwananchi Mei 26, 2017 ilieleza kuwa vijana wa MKIRU wanategemea mkaa, magogo, mazao, lakini wananyanyaswa na mamlaka, maliasili, mgambo na polisi.

Hadi leo, dhana 4 zinazunguka MKIRU: Ugaidi, Chuki za Kisiasa, Chuki Dhidi ya Polisi, au Uhalifu wa Kawaida.


Matukio haya:

  • Yalionesha changamoto za usalama.

  • Yalifichua mapungufu ya uwazi katika operesheni za dola.

Lakini bado, hakuna mjadala wa kina unaoongozwa na wanasiasa wenye msimamo, wengi huongea kwa msimu.

2.4 MAUAJI YA ZANZIBAR KILA UCHAGUZI.
(Kuanzia Mwaka 1995, 2000, 2005, Hadi 2021).

Zanzibar ina historia ndefu ya damu wakati wa uchaguzi:

  • 29 Oktoba 2000: Uchaguzi ulivurugwa. Waangalizi wa Jumuiya ya Madola, OAU, SADC walisema ulikuwa na dosari kiasi cha kutokuwa na hadhi ya kuitwa uchaguzi.

  • 27 Januari 2001: Polisi waliwaua waandamanaji wa CUF. Serikali ilisema waliuawa 23, CUF walisema 67. Human Rights Watch ilithibitisha angalau 35 na zaidi ya 600 kujeruhiwa. Zaidi ya 2000 walikimbilia Kenya kama wakimbizi.

  • 2020-2025: Vikundi vya “Janjawid” na vikosi kazi vimedaiwa kutumika kuumiza wapinzani. Haji Omar Kheir, Mshauri wa Rais tangu 2023, ametajwa majukwaani na Maalim Seif kuwa muasisi wa vikundi hivyo.

Historia ya chaguzi za Zanzibar imekuwa ikihusishwa na:

  • Vurugu.

  • Mauaji.

  • Migogoro ya kisiasa.

Haya si mambo mapya, lakini swali ni:

Kwa nini bado yanajirudia kila uchaguzi?

2.5 TUKIO LA 29 OKTOBA 2025.

Hadi kufikia nyakati za hivi karibuni, ikiwemo matukio mabaya ya mfululizo wa utekaji, upotezwaji wa watu, na vifo vya wanaharakati pamoja na viongozi wa kisiasa wa upinzani (kama vile mauaji ya wanasiasa wa Upinzani, na wengine), damu inaendelea kumwagika. Wananchi wanapoteza maisha wakiamini wanapigania mfumo bora wa maisha, huku wanasiasa wakichukulia harakati hizo kama mtaji wa biashara zao binafsi.

Uchaguzi Mkuu wa 29 Oktoba 2025 ulifuatiwa na ukandamizaji mkubwa. Ofisi ya Haki za Binadamu ya UN iliripoti:

  1. Mamia waliuawa, idadi isiyojulikana kujeruhiwa au kukamatwa.

  2. Zaidi ya 150 walikamatwa tangu siku ya kura, wengi wakiwa watoto, wakishtakiwa kwa uhaini.

  3. Inasemekana miili ilichukuliwa na vyombo vya dola na kupelekwa sehemu zisizojulikana ili kuficha ushahidi.

  4. Miundombinu na mali za watu binafsi ziliharibiwa, kupelekea wengi kupata hasara na hata kufirisika.

Mashahidi walisema askari walifyatua risasi za moto moja kwa moja. Viongozi wa upinzani na makundi ya haki wanasema vifo ni “mamia hadi zaidi ya elfu”, wengi wakiwa vijana, wanawake, watoto. Asilimia 95 ya waathirika walipigwa risasi kichwani au kifuani kwa karibu, kuashiria “nia ya kuua sio kutawanya”.

Mtandao ulizimwa, vyombo vya habari vikadhibitiwa. UN ilitaka uchunguzi huru na kuachiliwa kwa Tundu Lissu na wengine.

Hali hii imepelekea kujiuliza mambo haya matatu:

  • Uhuru wa kisiasa

  • Usalama wa raia na mali zao

  • Nafasi ya vyama vya upinzani

Lakini badala ya kujenga hoja za pamoja, wanasiasa wengi wamegawanyika kulingana na maslahi yao binafsi.

3. KWA NINI WANASIASA “NJE YA MFUMO” HAWAJUMLISHI KUPATA MAJIBU?

Wengi wanaopinga serikali wakati wako nje ya madaraka, wanapopata vyeo huwa kimya au wanashiriki katika mfumo huo huo.

  • Ukosefu wa Uwajibikaji wa Kitaasisi: Tangu Mwinyi ajiuzulu 1976, ni viongozi wachache wamewajibika. Mauaji ya Mwembechai 1998, MKIRU 2017, Zanzibar 2001 na 2025, hakuna ripoti ya wazi ya serikali wala hatua kwa wahusika. Hii inafanya “nje ya mfumo” wasiamini mfumo utatoa haki.

  • Matumizi ya Dola Kulinda Maslahi: Historia inaonyesha polisi na vyombo vya usalama vikitumika kukandamiza upinzani. Hivyo mwanasiasa akitoka nje, anakuwa hana ulinzi.

  • Maslahi ya Tumbo” vs Msimamo: Wapo wanaosubiri nafasi. Wakiwa nje wanasema serikali ni mbaya. Wakipewa uteuzi, wananyamaza. Hii ni “undumila kuwili na Ubarakala” – unafiki wa kisiasa. Lakini pia wapo wanaohofia uhai wao. Bila ulinzi wa kisheria, kusema ukweli ukiwa ndani ni hatari.

3.1. SIASA ZA KUHAMAHAMA VYAMA: UHURU AU MASLAHI?

Kihalisia, katiba na sheria za vyama vya siasa zinamruhusu mwanasiasa kuchagua chama anachotaka. Hata hivyo, changamoto ipo kwenye nia na muda wa maamuzi hayo.

Kwanini hawaunganishi dots (hawajumlishi, hawatoi wala kuzidisha, sembuse kugawanya) kupata majibu?

  • Wanasiasa wa Tanzania wanajua fika historia ya mauaji ya Shinyanga, Mwembechai, Zanzibar, na utekaji wa sasa. Wanajua kuwa tatizo ni mfumo wa kiutawala (Structural Problem) unaolinda madaraka ya chama kimoja na kuminya haki. Hata hivyo, hawataki kujumlisha matukio haya ili kujenga msimamo imara wa muda mrefu kwa sababu msimamo unagharimu. Kupigania mfumo wa haki kunahitaji kujitoa mhanga, jambo ambalo wanasiasa wengi hawapo tayari kulifanya pindi fursa ya "kula" inapojitokeza. Wanapigania maslahi ya matumbo yao na familia zao.

  • Unafiki wa kutosusia nyadhifa za kiserikaliHili ni swali la msingi sana: Kwanini mwanasiasa anayejinasibu kuwa upande wa wananchi akichaguliwa au kuteuliwa kwenye nafasi ya kiserikali (kama ubunge, uwaziri, au ubalozi) hawakatai?

  • Wanapokuwa ndani ya mfumo, wananyamaza kimya kabisa. Hawazungumzii mauaji, hawazungumzii utekaji, na wanatetea bajeti na sera mbovu.

  • Wanajifanya kuona serikali ni mbaya na ina ukatili pale tu wanapomaliza muda wao au wanapoondolewa kwenye vyeo vyao (Political Rejection). Huu ni uthibitisho tosha kwamba hawakuwa na uchungu na nchi, bali walikuwa na uchungu wa kupoteza fursa ya kufaidika na mfumo.

"Mwanasiasa anayelalamika kuwa mfumo ni mbaya baada ya kufukuzwa kazi, halalamikii mfumo, analalamikia kukatwa kwa mirija yake ya ugali."

3.2 AINA TATU ZINAZO PELEKEA WANASIASA KUHAMAHAMA VYAMA:

  • Wenye Misingi ya Kiitikadi: Wachache sana, huhama kwa sababu za sera na mwelekeo.

  • Wanaotafuta Nafasi: Uhama pale wanaponyimwa uteuzi au mamlaka. Hawa ndio wale siasa za tumbo (Mslahi Binafsi). Hutanguliza maslahi binafsi kuliko maslahi ya wananchi. Wengine hubadili vyama ili kupata nafasi za kiserikali, mikataba, au ulinzi.

  • Ukosefu wa Taasisi Thabiti za Vyama: Vyama vingi vinategemea watu binafsi badala ya msimamo wa kiitikadi.

  • Kupuuza Historia: Wanasiasa wachache hujenga misimamo thabiti kuhusu mauaji ya kihistoria (Shinyanga, Mwembechai, MKIRU, Zanzibar) ili kuzuia kurudiwa. Badala yake, wengi hujikita katika siasa za Matukio ya sasa kwa faida binafsi.

3.3 MIFANO HAI YA VIONGOZI WALIOHAMAHAMA.

Wabunge na madiwani wengi wametoka vyama vya upinzani (kama CHADEMA, CUF) na kujiunga na CCM wakati wa mabadiliko ya uongozi, wakidai “kuunga mkono maendeleo.”

Baadhi ya viongozi wa zamani wa upinzani wamechukua nyadhifa serikalini na kuacha kuikosoa serikali kwa ukali walioonyesha awali. Hii inaweza kuashiria undumilakuwili, kuwa na sura mbili kulingana na nafasi.

Hizi ndizo sababu nizionazo zinazoleta mashaka makubwa kwa jamii. Wanasiasa wanapokuwa nje ya mfumo, huikosoa serikali kwa nguvu zote. Lakini wanapopata nafasi ndani ya mfumo huo huo:

  • Hawakatai uteuzi.

  • Wananyamaza au kubadilika ghafla.

  • Baada ya kuondolewa madarakani, hurudi kuwa wakosoaji wakubwa.

Hii inazua swali:

Je, tatizo ni nini?

3.4 CHART


Jina la Kiongozi

Kuhama/Kubadili Msimamo

Muktadha na Sababu

Edward Lowassa

Kutoka CCM kwenda CHADEMA (2015), kisha kurudi CCM (2019).

Baada ya jina lake kukatwa CCM mwaka 2015, alihamia upinzani akidai mfumo wa CCM ni mbaya na haufai. Alikaribishwa na CHADEMA kama "shujaa". Baada ya uchaguzi kupita na upepo kubadilika chini ya Hayati Magufuli, alirejea tena CCM na kusifu kazi ya chama hicho.

Dr. Willibrod Slaa

Kutoka CHADEMA kwenda Diplomasia (CCM), kisha kurudi upinzani.

Alikuwa katibu mkuu wa CHADEMA na nembo ya mapambano dhidi ya ufisadi. Mwaka 2015 alijiondoa CHADEMA kupinga ujio wa Lowassa. Na hata kuongeza misumari na kuituhumu CHDEMA kuwa inateka wanachama wake wenyewe. Baadaye aliteuliwa na serikali ya CCM kuwa Balozi. Baada ya kustaafu ubalozi, amerudi tena kwenye msimamo wa kuikosoa vikali serikali kupitia majukwaa ya kiraia.

Lazaro Nyalandu

Kutoka CCM kwenda CHADEMA, kisha kurudi CCM.

Alikuwa Waziri ndani ya CCM, akahama na kwenda upinzani akidai mfumo unaminya demokrasia. Baada ya mambo kuwa magumu kisiasa, alirejea tena CCM akidai anaunga mkono juhudi za mwenyekiti.

Prof. Kitila Mkumbo

Kutoka ACT-Wazalendo kwenda CCM.

Alikuwa mmoja wa waasisi wa ACT-Wazalendo na mkosoaji mkubwa wa kiuchumi wa serikali ya CCM. Baada ya kuteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na Rais Magufuli, alihamia rasmi CCM na sasa ni Waziri na mtetezi mkubwa wa mfumo ule ule aliokuwa akiukosoa.

Mch. Peter Simon Msigwa

Kutoka CHADEMA kwenda CCM (Juni 2024), kisha kurudi CHADEMA (Mei 2026)

Baada ya kushindwa kwenye uchaguzi wa Kanda ya Nyasa ndani ya CHADEMA dhidi ya Tundu Lissu, alitangaza kukihama chama hicho kwa hasira na kujiunga na CCM, huku akimshambulia vikali Freeman Mbowe kwa madai ya udikteta. Hata hivyo, baada ya kukaa CCM kwa takriban miaka miwili na kuambulia patupu kwenye kura za maoni za kuelekea uchaguzi, mnamo Mei 2026 ametangaza rasmi kurejea CHADEMA akidai "nimechoka kuishi kwa huzuni" na kuwaomba radhi Watanzania.


Maneno ya Peter Msigwa Wakati wa Kuhama.

Uhamaji wa Mchungaji Peter Msigwa kwenda CCM uliambatana na kauli nzito zilizowaacha wananchi na maswali mengi kuhusu msimamo wake wa kiitikadi na "unabii" wa kisiasa aliokuwa akihubiri huko nyuma.

1. Kauli ya "Bata na Tai" (Kujitetea Kuhama CHADEMA)

Alipokuwa akihojiwa na vyombo vya habari kuelezea sababu ya kukimbilia CCM baada ya kushindwa uchaguzi wa ndani CHADEMA, Msigwa alitoa mfano wa ndege akisema:

"Mimi ni mtu wa kusema haki, mimi ni mtu wa kunyoosha maelezo, mtu wa kusema ukweli. Sasa kuna vitu ambavyo naona nikiwa upande huu [CHADEMA], ile umimi inashindwa. Naanza kuwa bata wakati natakiwa niwe eagle (tai). Sasa nikaona isiwe tabu..."

Kauli hii ilitumiwa na wakosoaji wake kuonyesha jinsi alivyokuwa akijitwika ukuu wa "Tai" (ndege anayeona mbali na mwenye nguvu), huku akidhalilisha taasisi na wanachama alioacha nyuma kama "Bata".

2. Kumlipua Freeman Mbowe na Kudai CHADEMA Hakuna Demokrasia

Wakati anapokelewa na Mwenyekiti wa CCM Taifa, Rais Samia Suluhu Hassan mnamo Juni 2024, Msigwa hakusita kurusha makombora kwa viongozi wake wa zamani. Alimshambulia waziwazi Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, kwa kumlinganisha na madikteta wa nchi za jirani:

Alidai kuwa CHADEMA imepoteza mwelekeo, haina demokrasia ya kweli, na inafanya "siasa za uongo". Alidai kuwa ndani ya chama hicho hakuna anayetakiwa kuhoji mamlaka ya Mwenyekiti na yeyote anayejaribu kufanya hivyo anakatwa mabawa.

3. Kugeuka na Kusifu Mfumo wa CCM

Ndani ya kipindi chake kifupi akiwa CCM, msimamo wa Msigwa ulibadilika kwa digrii 180. Yule Mchungaji aliyekuwa akipiga kelele majukwaani akilaani ukatili wa serikali ya CCM, mauaji ya Zanzibar, na ukandamizaji, alianza kusikika kwenye mikutano ya kampeni (kama kule Ismani mkoani Iringa) akisema:

"Tanzania ipo salama chini ya Chama Cha Mapinduzi. Upinzani hawana sera za ukombozi, CCM pekee ndicho chama chenye uwezo wa kuongoza na kuwaletea wananchi maendeleo."

Ukweli wa Siasa za "Matumbo": Msigwa Katupwa Kabatini na Kurudi CHADEMA (Mei 2026)

Mchezo huu wa kuigiza wa Mchungaji Msigwa umekuja kuthibitisha kwa vitendo hoja kuu ya makala yetu, kwamba wanasiasa wanatafuta maslahi ya matumbo yao na fursa za madaraka.

Baada ya kuhamia CCM kwa mbwembwe na kugeuka kuwa "chawa" wa kusifu kila kitu, Msigwa aliamini angetunziwa heshima yake na kupitishwa kugombea Ubunge wa Iringa Mjini kupitia tiketi ya CCM. Hata hivyo, mfumo wa CCM ulimtumia kama "karai" la kupigia propaganda na kisha kumtupa kando. Kwenye mchakato wa kura za maoni ndani ya CCM kuelekea Uchaguzi Mkuu, jina la Msigwa liliangukia pua na halikuwemo hata kwenye majina matatu ya juu ya wanachama waliopendekezwa na wajumbe.

Baada ya kuona amewekwa "kabatini" na kupoteza umaarufu wote wa kisiasa mbele ya jamii, mnamo Mei 2026, Mchungaji Msigwa ameamua "kulamba matapishi yake" na kutangaza kurejea CHADEMA kwa aibu, akitoa kauli mpya inayovunja moyo:

"Nimechoka kuishi kwa huzuni, Watanzania naomba mnisamehe..."

Huu ni uthibitisho mwingine hai kuwa wanasiasa hawa hawana chembe ya msimamo wa kiitikadi; upepo wa maslahi binafsi ukivuma upande wa mashariki wanakuwa "Tai wa kijani", upepo ukiwakataa wanarudi upande wa magharibi kuwa "Bata wa bluu", huku damu ya wananchi wanaouawa kwenye harakati za kulinda vyama hivyo ikiendelea kupuuzwa.

Wimbo huu wa Peter Msigwa atangaza kurudi CHADEMA unaonyesha video ya tukio la hivi karibuni ambapo mwanasiasa huyo anaomba radhi hadharani na kutangaza rasmi kurejea chama chake cha zamani baada ya safari yake ya kisiasa ndani ya CCM kukwama.

3.5 BILA KUWAHUKUMU, TUANGALIE MIFANO YA TABIA:

  • Kundi la “Waliokurupuka 2015-2020”: Wanasiasa kadhaa walihama kutoka upinzani kwenda CCM wakati wa utawala wa Rais Magufuli. Hoja yao: “utawala umekubalika”. Wakosoaji wanasema walitafuta ulinzi baada ya kubanwa.

  • Kundi la “Waliotoka CCM 2022-2024”: Baadhi ya wabunge na madiwani walihamia upinzani baada ya kukosa teuzi au kura za maoni. Walidai “wanataka mabadiliko”. Lakini walipokuwa ndani, hawakuyasema.

  • Zanzibar: Haji Omar Kheir alishindwa uchaguzi Tumbatu, akalia kwenye mtumbwi. Baadaye ZEC ikamtangaza mshindi. Akiwa Waziri wa vikosi, vikundi vya kihalifu vilishamiri. Leo ni Mshauri wa Rais. Mfano wa jinsi mfumo unavyoweza kutumika.

3.6 TATIZO KUBWA: Ukosefu wa Msimamo wa Kisiasa

Wanasiasa wengi:

  • Hawajengi misingi ya kudumu ya sera.

  • Wanabadilika kulingana na upepo wa kisiasa.

  • Wanashindwa kuunganisha nguvu wanapokuwa nje ya mfumo.

Badala ya:

  • Kujenga hoja za pamoja.

  • Kutoa mbadala wa kisera.

  • Kulinda maslahi ya wananchi.

Wanageuka kuwa:

Wapinzani wa muda na watawala wa muda”

4. JE, NI UNDUMILA KUWILI NA UBARAKALA?

Ndiyo, kama kigezo ni “unasema nini ukiwa ndani dhidi ya ukiwa nje”. Lakini pia ni swali la “mazingira”. Mfumo usio na uwajibikaji unazalisha wanafiki na wanasiasa tumbo, wenye kujipendekeza, kwani ukweli ni gharama.

Kwa kuangalia mienendo:

  • Mwanasiasa anapokuwa nje ya mfumo: Anaona mfumo ni mbaya.

  • Akiingia ndani ya mfumo: Anakwa karambishwa asali, Ananyamaza.

  • Akitoka/kufukuzwa: Anarudia ukosoaji ule ule.

Hii ni ishara ya:

  • Kukosa uadilifu wa kisiasa.

  • Kukosa ujasiri wa kusimamia ukweli.

  • Kuweka mbele maslahi binafsi kuliko taifa.

5. HITIMISHO: Nini Kifanyike?

Siasa za bendera kufuata upepo (Siasa Maslahi) ni usaliti mkubwa kwa damu ya Watanzania waliopoteza maisha huko Shinyanga, Mwembechai, Pemba, Unguja, na katika barabara za Dar es Salaam na Tanzania kwa ujumla, kupitia utekaji na mauaji ya kisiasa.

Wanasiasa wa Tanzania wanapaswa kutambua kuwa historia itawahukumu vikali. Kitendo cha kuweka mbele maslahi ya matumbo yao na kuwa tayari kugeuka geuka kiitikadi kinazidi kuchelewesha upatikanaji wa Katiba Mpya na Tume Huru ya Uchaguzi, vitu ambavyo vingemaliza kabisa mzunguko huu wa ukatili na mauaji kila msimu wa uchaguzi. Bila kuwa na viongozi wenye msimamo thabiti (kama ule wa uwajibikaji wa Ali Hassan Mwinyi wa mwaka 1976), siasa za Tanzania zitabaki kuwa biashara ya watu wachache, huku raia wa kawaida wakiendelea kuwa wahanga wa upepo wa kisiasa.

5.1 TUNAWAJIBIKA:

  1. KUKUMBUKA HISTORIA: Shinyanga, Mwembechai, MKIRU, Zanzibar, 29 Oktoba 2025 – damu hizi ni dira. Mwanasiasa asiyejifunza historia atairudia.

  2. UWAJIBIKAJI WA LAZIMA: Kama Mwinyi alivyojiuzulu 1976, tunahitaji utamaduni ambapo waziri, IGP, RPC anawajibika mauaji yakitokea.

  3. TUME HURU ZA UCHUNGUZI: UN imeitaka Tanzania kuchunguza mauaji ya 2025. Bunge linapaswa kuanzisha tume huru kwa Mwembechai, MKIRU, na Zanzibar.

  4. KATIBA MPYA: Ili kuzuia wanasiasa kutumia mianya ya “siasa haina adui wa kudumu”, tunahitaji katiba inayozuia wabunge kuhama vyama bila kurudi kwa wananchi.

  5. WANANCHI WAWE MAKINI: Wasiangalie maneno bali matendo.

  6. Vyama vijenge itikadi: Siasa isiwe ya mtu binafsi.

  7. Historia ya kweli ya Tanzania, ifundishwe, ili makosa yasirudiwe.


6. MWISHO:

Kuhama chama si dhambi. Dhambi ni kuhama misimamo, kuhama ukweli, na kuhama dhamana kwa wananchi. Historia ya mauaji inatukumbusha: cheo ni dhamana, si kinga. Mwanasiasa anayepuuza historia hii, leo akisifia, kesho akilaani, huyo anapigania tumbo lake tu.

Jamii iulize: Kiongozi wako alisema nini kuhusu MKIRU akiwa Mkuu wa Wilaya au mkoa au hata ubalozi? Alisema nini kuhusu mauwaji ya kule Zanzibar na 29 Oktoba 2025 akiwa na cheo? Majibu yake ndiyo kipimo cha msimamo wake.

Wajibu wetu kama raia ni kudai uwajibikaji na kuelimishana ili siasa ziwe za maendeleo, si za faida binafsi.

Na kama historia ya mauaji na matukio ya kiusalama haijawafanya raia na wanasiasa kujifunza, basi swali linabaki wazi:


JE, WANATUMIKIA NCHI… AU WANAITUMIA NCHI?


Monday, 15 May 2023

 HIVI KWELI NILIKUFA AU
NILIUWACHA TU UHAI KWA MUDA!?

  •          Naamini Kabisa, Nilikufa Kwa Dakika Kadhaa, Ilikuwa ni Hali ya Kushangaza na Kustaajabisha Mno!
  •       Ni Tukio Lililotokea Zaidi ya Miaka Kadhaa Nyuma, Kabla ya Mabasi ya Mwendokasi...

Siku hiyo ilikuwa kama siku zingine tu zisizo na majina, ile hamu ya katembea kwa miguu na ile taswira ya jiji la Dar, ilisawiri barabara kwenye bongo langu.

Kama kawaida ya mitaa mingi ya Kariakoo, kumejaa watu wa kila aina. Nikapita kwenye mitaa iliyosongamana watu nikishajika huku na kule, nikakumbuka kufuchama Rununu yangu, kwa kuchelea wivi, wasijeichukua bila ruhusa yangu, huku sauti za wabeba mizigo kwenye Rikwama, wakiyosayosa maneno ya kutiana nguvu.

Nikapishana na msukuma rikwama mmoja akanitolea maneno ya kuudhi, sikumjali! Upande mwingine kuna Bodaboda zinafukuzana, nikazikwepa nisipigwe dafrao...!

Huku nikijiwazia, "...hawa waendesha Bodaboda wamekuwa watu wa ajabu sana, ni watu wenye kudhania kuwa wao wana haki ya barabara na hata pembeni ya barabara kuliko mtu mwingine yoyote, na sheria za barabara haziwahusu..."

Ghafla bin vuu..! Nikajikuta napaa hewani, usawa wa futi kadhaa, nikabakia naelea hewani, huku makelele ya watu na kina mama wakiwa kwenye shake kubwa... "Mtumeee...! Kashauwa, Tobaaa yaillahi kijana wa watu..."

Sikumbuki ni nini kilitokea, ila nilicho kiona mpaka leo nikikikumbuka naingiwa na shakawa kubwa yenye kutetemesha mwili wangu na moyo kuingiwa na hofu, kiasi cha kuunyogesha.

Tahamaki nikaona watu kwenye tahanani, huku wametaharuki, wakijikusanya kumzunguka mtu aliyelala pembeni mwa barabara, nikamsikia mdada mmoja akisema, "…Kagongwa na Bodaboda...!"

Kitu cha kwanza kunistaajabisha, ambacho mpaka leo sijui jinsi ya kukielezea wala kuolelezesha, ni ile hali ya utulivu na amani niliyokuwa nayo muda ule. Nilikuwa namuonea huruma kila mtu, kama vile wanapoteza muda wao tu hapa duniani.

Kitu cha pili ambacho kilishtua roho yangu, ni pale nami nilipotaka kujisogeza kuelekea kwenye akhlaki ya ule mkusanyiko... Badala ya kutembea nilikuwa kama mtu anae elea na kujisogeza mzima mzima, sikuwa nakanyaga ardhi, nilihisi wepesi ambao sijawahi kuupata kwenye maisha yangu.

Kuna kitu kilinipelekea nione upande wa machweo ya jua, nikaona viumbe visivyo elezeka, kama vile vinaashiria nisiende huko walipo... Sawia wengine wakiniita nielekee walipo wao, wakiwa upande wa Kaskazini wakiwa na maumbo yenye kupitisha mwanga, mfano wa Jeli...!

Matendo yote hayo yalitokea sanjari...! Nikastaajabia uwezo ule wa kuona pande zote bila kugeukageuka!

Ile hali kwanza haikujisajili kwenye bongo langu, ni mpaka pale nilipojisogeza kwenye lile kusanyiko. Nikapitiliza bila kugusana na mtu yoyote yule, ndipo hapo sasa mshituko mkubwa ulipo nipata.

Nilishuhudia mwili wa mtu ukiwa umelala pembeni karibu na mtaro wa maji, huku mtu mmoja Shaibu mwenye mwili wa ajabu, akijitahidi kushajiishika kutoa huduma ya kwanza, huku akiwazuiya vijana sefule mashakili, wasipenyeze vidole vyao kwenye mifuko ya suruali iliyovaliwa na ule mwili.

Nikamkumbuka yule Shaibu, ni mmoja wa wazee wa mitaa ya kule Gerezani, ni katika jamaa zetu, ananifahamu nami namfahamu, lakini jinsi alivyo kama vile yupo tofauti na watu wengine (Nilikuja Kufahamu Baadae, Kwanini Nilimuona yupo Vile).

Yule Shaibu, alikuwa akinihita kwa jina langu na lababa yangu (Fulani Bin Fulani), huku akishahiri watu wasimamishe gari waupeleke mwili hospitali. "...Simamisheni gari tumpeleke hospitali haraka, huyu bado mzima, mwili ungali moto, si wa ahera huyu..."

Nadhani watu wengine walimuona ni wa kawaida tu, la sivyo, asingesogea mtu karibu yake…!

Nikataka kumwambia kuwa nipo hapa, pembeni lakini sauti haikutoka, maana hata hao watu wengine, wakinipita bila kunikwepa, kama vile mtu anapishana na upepo...!

Ule Mwili Pale Chini, Ulikuwa Ni Mwili Wangu...!

Wakaunyanyua ule mwili na kuupakia kwenye gari la mizigo, Toyota Pickup, ajabu nyingine ni pale nilipo ona ule mwili umeunganishwa na nafsi yangu au sijui niseme ndio roho yenyewe (Wallahi hata sijui ni kitu gani), kimefanana na kama uzi mwembamba hivi wa ajabu, wenye rangi niseme kama nyeupe au rangi ya fedha pamoja na rangi ya Zambarau hivi lakini yenye kupitisha mwanga, kiufupi niseme kama uzi wa kioo wenye kumetameta, wenye kufanana na mwanga au umeme wa radi.

Uzi au kamba ile nyembamba sana ilikuwa imeniunganisha mimi na mwili ule, kupitia kwenye kitovu... Nikajikuta nipo sawia na mwendo wa gari. 

Kupitia barabara ya Msimbazi, kisha barabara ya Uhuru, kuelekea hospitali ya Amana.

Yule Shaibu akaweka mkono wake mmoja kwenye kichwa cha ule mwili kwenye utosi, na mkono mwingine akashika vikidole gumba vya miguu wa kulia na kushoto, kisha akatamka shahada (la 'ilaha 'illa-llahu akitaja na majina mengine ya MwenyeziMungu, Ar-Rahmaan, Ar-Rahiim, Al-Aziiz, As-Samii, Al-Basiir, Al-Wahhaab, Al-Baasit, Al-Ghafuur, Al-Hafiidh, Al-Mujiib, Al-Waduud, Al-Ba’ith, Al-Mu’id, Al-Muhyii, Al-Hayy, An-Nur, Al-Barr, At-Tawwab, Al-‘Afuww, Dhul-Jalaali Wal-Ikraam, Mrejeshe… ).

Akabonyeza kwenye chembemoyo, kwenye mbonyeo ulio baina ya gegedu la mifupa ya mbavu, katikati ya kifua cha mwili ule (mwili wangu), kwa kidole gumba chake, kwa lengo la kusisimua mapavu na moyo wa ule mwili, viweze kurejea kwenye kazi yake...!

Kila alipokuwa akikandamiza kifua cha mwili ule baina ya gegedu na utosi, huku nami nikajikuta naukaribia ule mwili...!

Ni kama vile alikuwa anavuta ule uzi ulioniunganisha mimi na ule mwili...!

Ghafla polepole nikaanza kuhisi kupotelewa na uwezo wa kuona na kusikia, sikusikia chochote, kama vile ninayepoteza fahamu na kuzama kwenye rima, lisilo na mwisho, macho hayakuona kitu... Huku ule uzi ukinivuta na mimi kwa haraka sana kama mtu anayevutwa na nguvu kubwa kelekea ulipo mwili wangu…!

Nilikuja kushituka nipo Hospitali ya Muhimbili, nilikuja kuambiwa kuwa, baada ya ile ajali, wasamalia wema, walinipeleka Hospitali ya Amana, kisha kuhamishiwa hospitali ya Muhimbili.

Uzuri vipimo vilionyesha kuwa sikuathirika sana, kule kupoteza fahamu ni baada ya kujipigiza kichwa kwenye lami.

Kumbe nilipoteza fahamu kwa siku mbili.

Siku ya tatu, baada ya kutoka hospitali, nilimuulizia yule mzee aliyenisadia (Nikamtaja kwa jina), nikaambiwa kuwa, uwenda nimemfananisha tu, maana huyo mzee mbona, alisha fariki siku nyingi sana, ni zaidi ya miaka kumi sasa tangia amefariki...! Kidogo nizimie tena...!

Ndugu zangu, kweli roho zipo, maana zile dakika kadhaa, niliona mengi sana, niliyaona yasioweza kuonekana kwa macho ya kawaida, MwenyeziMungu alifungua pazia la macho yangu ya rohoni, nikaona yasiyo onekana kwa macho ya kawaida.

Kiukweli wala sijui ni kwa jinsi gani naweza kuyahadithia mambo yale yote...!

Nilipotoka hospitali, nilikuja kutafuta kufahamu maana ya yale maneno ya Shaibu yule... Nikayaelewa...!

Wednesday, 15 February 2023

TETEMEKO LA ARDHI NCHINI UTURUKI NA SYRIA

Kahramanmaras Lasababisha Watu Zaidi ya Elfu Ishirini na Nane Kufariki Dunia.

Maisha ya Dunia sio Chochote Mbele ya Muumba na Yaweza Kukatika Ghafla Bila ya Kuletewa Taarifa. Tuna Amka Tukilala Tukiwa ni Wenye Kusindikiza Vijana kwa Wazee Kwenye Makazi ya Milele Wakipitia Ndani ya Barzakh.
Zipo njia nyingi za kukatika maisha haya kama vile ajali, maradhi na mauaji.
Hata hivyo, kuna aina nyingine ambayo kwa karne mbili hizi zilizopita, imepamba moto. Ni hii ardhi yetu tunayoringa nayo kushindwa kabisa kuhimili mambo. Hapo tunaona kimbunga, mitetemeko ya ardhi ya kiwango cha juu, joto na baridi kali na balaa kadha wa kadhalika.
Ardhi ya Nchi ya Uturuki na Syria imetikisika, na huu ni mfano mzuri wa kuwazinduana ndugu zengu Waislam. Hakika kuna mengi ya kujifunza kwa sisi Waislam kutokana na matetemeko haya ya ardhi, na haswa matetemeko yaliyotokea tarehe za hivi karibuni, mwezi huu wa February 2023, ni tetemeko lenye ukubwa wa Kiwango cha 7.8 magnitude katika nchi hizo mbili.
Maisha ya watu wasiopungua watu elfu 28 yamepotea ghafla bila ya matarajio.
Na maelfu ya watu wamejeruhiwa na majumba na mali kadhaa zimeharibika. Ile siha na neema aliyowapa Allah imeondoka kwa wepesi kabisa.
Maelfu ya maisha ya watu yamebadilika ghafla ndani ya kipindi kisichozidi nusu saa...!
ALLAHU AKBAR!
Yapo wapi macho ya Waislam kutanabahi kiumbe hichi kinachoitwa ardhi kushindwa kuhimili mambo ya wanaadamu!?
Hali ya huzuni, majonzi na masikitiko imewezwa kupugua kidogo na faraja kupatikana kwa waanga wa tetemeko ilo, pale ubinaadamu na moyo wa kusaidia haraka, ulipojitokeza aidha kupitia serikali zao na serikali za nchi nyingine na mashirika binafsi ya kujitolea.
Hata kwa wale waliokuwa hawana uwezo, nao wanajitolea kusaidia ndugu zao.
Sisi Waislam leo uwezo tunao, badala ya kusaidiana tunaleta jeuri ya neema tuliopewa.
Ni funzo kwa Waislam kuwa Maneno ya Allah (Subhaanahu wa Ta’ala) hayaanguki abadan, kuwa siku za mwisho kutakuwa na majanga mengi, vifo vitatokea vingi kwa pamoja na mengineyo:
Uharibifu umedhihiri barani na baharini kwa sababu ya yale iliyofanya mikono ya watu, ili Awaonjeshe (adhabu ya) baadhi ya mambo waliyoyafanya, huenda wakarudi (wakatubia kwa MwenyenziMungu).
Ar-Ruum 30: 41
Naye Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amekwisha bainisha kuwa maafa yatakuwa ni mengi karibu na Qiyaamah:
“Saa (Qiyaamah) haitosimama hadi elimu ifutwe, wakati kukimbia kwa kasi, mitetemeko kuzidi kwa sana, fitna kutokea na al-Harj kuengezeka.” Akaulizwa, “Ewe Mjumbe wa Allah, nini hiyo al-Harj?” Akasema, “Al-Qatl, al-Qatl (Mauaji, Mauwaji)”.
Imepokewa na Imaam Ahmad
Na kwa vile maneno ya Allah (Subhaanahu wa Ta’ala) pamoja na Mtume Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa salam) ni mazima; tujue kuwa mitihani hii ipo, na bila ya shaka kila tuliloahidiwa litatokea, ikiwemo Qiyaamah chenyewe.
Kwa mantiki hiyo; tunatakiwa tustaghfiru na tujiweke tayari na kifo wakati wowote.
Hakuna mwenye mihadi na Malakul-Mawt. Anakuja ule wakati anaopangiwa na Mola wake aje kuzichukua roho zetu. Waturuki na Wasyria wale waliokufa kwa mpigo hakuna hata mmoja aliyejuwa kama siku ile angekufa, ya kwamba angekwenda nchi jirani kwa kukimbia mauti. Laiti ghayb ingejulikana na viumbe, Serikali ya Uturuki na Syria zingekuwa na uwezo wa kuwahamisha watu wake kutoka kwenye eneo la hatari kabla maharibiko hayajatokea.
Hili jambo liwaguse wanaosema: "acha ni-injoi, mie kijana, bado damu inachemka kotekote". Waliokufa katika maafa wamo vijana waliochemkwa na damu mpaka zikatokota kwa afya njema na uzuri.
Na wale walionekana na maumbo madogo, hawakuwa ni vibete au mbilikimo, bali ni watoto wadogo. Hii ni kuonesha kwamba kifo au maafa hayachagui umri.
Hili jambo pia liwaguse wenye uwezo wanaogoma kwenda Hijja, wakisema kuwa mambo bado, ipo siku nitakwenda ilihali uwezo anao.
Nadhani, pengine katika maelfu ya watu wale kuna ambao walikuwa na mawazo kama hayo japo mmoja na hakufanikisha malengo. Na hiyo ni khiyana kwa Allah mtakatifu tunamfanyia, kuwa katupa uwezo na tunautumia kinyume na malengo ya Uislamu.
Liwaguse hili jambo, wale wanaosema watajistiri... tusubiri... tusubiri kwanza...!
Ni vyema nikakomaa hapa, kwani ni mengi tunayojifunza kutokana na mitetemeko hii ya ardhi na maafa mengine ya kiasili.
Mimi moyo wangu umeingiwa na khofu kubwa juu ya mauti na amali zetu, nimeingiwa na imani na watu waliopoteza viungo ambavo sisi tunavyo na badala ya kumshukuru Mola Mlezi wetu, hatuinami (hatusali) mpaka tuanguke (tufariki).
Nimeingiwa na imani kuona vitoto vichanga, wazee na wanawake na wengine wakikosa malazi na sehemu za kijihifadhi.
Nimesikitika kwa kila hali na nikalia ndani ya moyo wangu.
Wa billahit Tawfiyq.

Monday, 6 February 2023

 GANDA LA HARAGWE KWENYE JINO

Huku kazini, tulikuwa na mkutano wa kuongelea ufanisi utakaopelekea natija kwenye kazi zetu za Kila siku. Nilikuwa ni mtakadamu kwa siku ile, kwa wanao wasilisha mada...

Kabla sijaingia kwenye chumba Cha mkutano, nikapitia maliwatoni, nikachua na udhu Ili nipate faradhi kabla ya mkutano kuanza. Wakati najiangalia kwenye kioo nikipaka mafuta kupunguza ukavu wa ngozi na baridi, wakati nafanya mkaguo, tahamaki nakenua kinywa, nakutana na twasira ya Ganda la Haragwe limeganda kwenye jino.

Kumbukumbu zangu, zilichelewa kidogo kusajili tukio la mimi kula maharagwe. Ni baada ya sekunde kadhaa, nikakumbuka kuwa nilikula maharagwe na tambi, takriban siku tatu nyuma.

Lile ganda lilinitafakarisha sana, kwanza nashukuru nililiona mapema kabla ya mkutano, maana ningekuwa kituko cha siku kama si wiki nzima, Alhamdulillah tahayuri iliniepuka.

Fikiria mtu unaweza kula chapati na MAHARAGE majira ya asubuhi, ukasindikiza na chai vikombe kadhaa... Ukasukutua kinywa mara tatu...

Mchana ukala ugali na nyama, Ukasindikiza na maji ya matunda, Usiku ukala zako boflo na chai tu...

Kabla ya kwenda kulala, ukapiga mswaki, meno umeyasugua vizuri, bila kusahau ulimi, ukausugua mpaka kwenye koromeo, kisha ukasukutua tena na tena...!

Asubuhi, kabla ya kuwahi kazini unasafisha kinywa kwa kusugua meno vizuri na kusukutua mara tatu, unafika kazini, unacheka na jamaa zako, ghafla tu, wanaona Ganda la Harage kwenye Jino lako la mbele, tena harage lenyewe ni la juzi...!

Kwenye tafakuri yangu, nikagundua mfanano wa sisi viumbe binadamu na Ganda la Harage kuganda kwenye jino.

Na ndivyo binadamu tulivyo, waweza kutendewa wema, ihsani na kila zuri, lakini si sababu ya wewe kutosengenywa, wala si sababu ya wewe kutochukiwa, fanya ufanyalo, utaingia midomoni mwa waja kwa njia hisiyo pendeza kwenye masikio yako.

Ndio, Kuna Viumbe Hapa Duniani, Wapo Kama Ganda la Haragwe...!

Hakika tumefanikiwa katika ili la kutopendana na kuhishimiana, tumefanikiwa kueneza chuki miongoni mwa jamii zetu, si Waislam, si Wakristo, si Wapagani, na huko kwenye siasa za Kisekula ndio kabisa kumeoza, kiasi tumekuwa mbilikimo wa kifikra, tumefanikiwa katika kugawanyika miongoni mwetu na sasa tupo zaidi kimakundi, na wale ambao hawapo kwenye makundi au jumuiya yetu basi huyo si mwenzetu.

Tutamtia midomoni kwa maneno ya uongo na kashfa, mpaka apate shinikizo la moyo na jirani yake mapafu, kama si la figo na maini yake...

Tabia hizi kwa kweli zimemea kwenye nafsi zetu na zimendoa mafungamano ya kirafiki na kindugu na kusababisha majadiliano yetu hukosa busara na hikma kiasi cha kupelekea kwenye utengano na uhasama ambao tunaweza kuuepuka.

Mnisamehe tu, uzee huu, yote haya sababu majuzi nilikula maharagwe, ganda likabakia siku nne kinywani, kweli jitihada haishindi kudura, na takadiri huwezi epuka.

Sunday, 8 January 2023


WAZIMU WA MADEREVA WA BODABODA

Hivi Waendesha Pikipiki Maarufu kwa Jina la Bodaboda, Bongo zao ni Zile za Zinjanthropus!?
Safari ya Kutoka Kariakoo Mpaka Sinza, Kwa Siku Moja tu, Nilishuhudia Ajali Saba za Bodaboda. 

Nilipopata likizo yangu ya mwaka, nikafunga safari kwenda Bongo, baada ya kuondoka takriban miaka na miezi kadhaa, kwa kweli nilikuwa na hamu kubwa sana ya kukutana na ndugu, jamaa, marafiki na majirani zangu. Na haswa ukizingania ni miaka imepita na uku hamu yangu kubwa kuona jinsi gani usafiri wa Bodaboda na Bajaj ulivyo shamiri jijini Dar.

Mengi nilisimuliwa kuhusiana na madereva wa Bodaboda na jinsi wanavyoendesha biashara zao, nami nikawa na hamu ya kulinganua na pia kushuhudia kwa macho ni kipi haswa kina ukweli katika hayo masimulizi.

Nakumbuka kuwa Pikipiki zilianza kutumika nchini Ujerumani katika karne ya 19. Ulikuwa usafiri uliokuwa mpya lakini ulirahisisha kuabirisha hasa ukikumbuka watu wa huko wakati huo wengi waliwatumia hayawani kwa ajili ya usafiri.

Huku kwetu enzi ya Mkoloni Muingereza ndio pikipiki zilianza kusambaa sana na kati ya pikipiki zilizopendwa zilikuwa za aina ya BSA kutoka Uingereza, pikipiki hizi zilipata jina kutoka kampuni iliyokuwa inazitengeneza iliyoitwa Birmingham Small Arms Company.

Baada ya Uhuru pikipiki za Honda, Suzuki kutoka Japan na Yamaha, zilipata umaarufu sana, pia kulikuwa na pikipiki aina ya VESPA toka India na BATAVUS za Mdachi nazo zilikuwa maarufu sana hapa nchini.

Umaarufu wa pikipiki ulipelekea serikali kuwapatia Makatibu Tarafa, Mabwana Shamba na watumishi wengi wa serikali pikipiki aina ya Honda 90 na baadae zikaletwa Honda 125. 

Pikipiki hizi zilikuwa ni imara kweli kweli, haswa Honda 90, maana zina uwezo hata wa kufungiwa jembe ulaya (plau) na ukalima kwa kutumia pikipiki.

Miaka yote hiyo waendesha pikipiki walikuwa watu wastaarabu walioheshimika na kuheshimu sheria za barabarani. 

Miaka hii michache zimeingia pikipiki za Kichina, ambazo zimezagaa kwenye biashara inayoitwa Bodaboda.

Waendesha bodaboda wamekuwa watu wa ajabu sana, ni watu wenye kudhani kuwa wao wana haki ya barabara na hata pembeni ya barabara kuliko mtu mwingine yoyote, na kuwa wao sheria za barabara haziwahusu.

Hawa ni watu wanaoamini kuwa ukipiga honi tu inatosha kuyafanya magari, majengo na hata miti kuhama na kuwapisha wao wanapotaka kupita. Kiukweli kwa siku chache nilizokaa likizoni, nilishuhudi mamia ya vijana wakijeruhiwa na wengine kufariki kwa ajaili za kizembe za kila siku za usafiri huu.

Mie naiomba serikali ifanye uchunguzi wa kina kabisa, hivi kwanini watu wakiendesha hizi pikipiki za Kichina akili zao zinahama? Kwanini hizi Pikipiki za Kichina zimewekwa nini mpaka Bongo za waendeshao hizi pikipiki zinakuwa kama za Zinjanthropus!

Mimi na mashaka na sponji inayotumiwa kwenye viti vya Bodaboda, inawezekana ina madini ambayo yakimuingia anae iendesha akili inahama.

Serikali ifanye uchunguzi wa wasiwasi wangu huu. Kwa kuwa sioni sababu kwanini waendeshaji wa zamani walikuwa hawapotezi akili, ila hawa wa Bodaboda akili zao, zinakuwa sio kabisa, hisije kuwa Wachina wana mpango wa kando kutupunguza, ili wahamie Afrika maana... Mmmh!

Wednesday, 4 January 2023

MBIOMBIO NIKAJIKUTA NALIKIMBILIA GARI LA KUZOA TAKA

Nilikutana Naye Kwa Kinyozi... Akauliza, Kwa Unyenyekevu Kabisa..!
Basi bhana, Nipo Zangu Varandani, Mida ya Saa Tatu Hivi ya Asubuhi, Ghafala Huko Nje Nikasikia mlio wa Gari ya Kuzoa Takataka. Nikakumbuka Kuwa Nilipaswa Kutoa Pipa la Taka Tangia Jana Usiku... Nikakurupuka kama Swala aliyekoswa koswa na Simba.
Mbiombio nikapitiza uwani, nikakutana na rasharasha za mvua, uku nikijikwaa kizingitini, sikujali sana, nikakamata kishikio cha pipa, nakaliburuza mpaka nje.
Natoka gari lishapita, lipo takribani nyumba ya Tatu toka kwangu.
Sikukata tamaa, nikapiga mbinja, huyo mbiombio nakimbiza gari wanguwangu, kandambili imenichomoka mguuni wala sina habari, kufika ni hoi, nahema kama Mjombakaka aliyekoswa koswa kunyakuliwa na Kipungu.
Nilipo wafikia mmoja wa mzoa taka, akanambia kuwa si gari hili, wao ni wa kampuni nyingine... Nikajikuta nimechoka mara dufu.
Mbio za mita kumi na tano kama si ishirini, zilinifanya niwe hoi taabani, polepole nikajirudia zangu nyumbani, nikaokota ndara yangu iliyonichomoka wakati wa kukimbiza gari la taka, nikajigundua kumbe nimelowana...!
Nikajifuta maji, nikakaa zangu sebuleni, nikajitafakari, nikakumbuka ni siku tatu tu, tangia watu washeherekee mwaka mpya.
Nikakumbuka mengi, yaliopita kwenye maisha yangu, mtu mie niliyekuwa hodari wa mbio, leo hii mita ishirini zimenitoa kamasi...!
Mawazo yakanichukuwa, yakanipeleka siku ya mwaka mpya...
Ilikuwa baada ya kumaliza Faradhi ya salah ya insha, nimekaa na Memsapu wangu, tukiongea na kucheka na huku tukitafakari jinsi Mwaka ulivyopita. Kwa mbali tukasikia sauti za Fashfashi, huku mwanga ukimemetuka. Tukakumbuka kuwa kumbe mwaka umeisha, watu wanashereheka huko nje kwa kumaliza mwaka.
Vijana wangu wakatoka hapo nje, kuangalia fashfashi, zikimemetuka angani. Dakika hazikwisha, nikakatizwa na mlio wa simu ya mkononi. Triiii! Triiii! Triiii...! Kuangali kumbe zilikuwa ni meseji zikiingia mfurulizo. Nikawa najiuliza kuna nini tena mbona meseji nyingi kiasi hiki!?
Nikaamua kuzisoma moja baada ya moja, na meseji zote zikinitakia salamu za mwaka mpya, wenye amani na maisha mema.
Nikajikuta nakumbuka kisa kimoja kilichonipata kabla ya ule mwaliko toka kwa Sahibu yangu, takribani siku sita zilizopita.
Siku hiyo nilipitia kwa Kinyozi kwa dhumuni la kupunguza kidogo nywele na kukata sharubu zangu, maana nazo zilikuwa ndefu, kama Gari Moshi la kuelekea Kigoma.
Baada ya kuchakachua mwendo nikafika kwa Kinyozi, mitaa ya Kariakoo, kumekusanyika vijana kadhaa, wapo wanaosubiri kunyolewa na wapo wenye kupiga ndaro na ndarire za hapa na pale.
Wakati nasubiri zamu yangu, macho yangu yakagongana na mzee mmoja wa makamu hivi, kakonga kiasi chake. Kumtazama vizuri na kuchakata sura yake, nikahisi kumkumbuka.
Ndio Huyu huyu, alikuwa mmoja wa vijana niliosoma nao sekondari, nikamkumbuka kijana mmoja maungo makakamavu, rangi maji ya kunde, nakumbuka nikimtania kwa jina la Andunje. Tulikuwa wote darasa moja ni zaidi ya miongo mitatu sasa imepita!
Ila sasa ndani ya nafsi yangu nilikuwa bado najiuliza, ndio huyu, kijana aliyekuwa akisumbua sana kwenye masomo ya Hisabati pamoja na yale ya sayansi!?
Nikamtazama tena na tena, hakuonyesha kunikumbuka hata kidogo nikataka kumpotezea, lakini upande mmoja wa bongo langu, likanishauri  vingine. Nikatizama kichwa chake, kilichokuwa kimejaa mvi za hapa na pale, uso wake wenye makunyanzi.
Kwa jinsi alivyozeeka, asingeweza kabisa kuwa ni yule kijana niliyesoma naye darasa moja, nikajiliwaza kwa kujisemea moyoni, labda uwenda ni baba yake mdogo au ni watu tu wanarandana!
Zamu yangu ikawadia, nikajisogeza na kukalia kiti cha kinyozi, nikamuelekea jinsi gani nataka... Baada ya kumaliza na kulipa, nikapiga moyo konde na kujipa ujasiri, nikamsogelea na kumuuliza kama aliwahi kusoma shule niliyosomal?
Huku nikimkazia macho nikamuuliza, "Samahani ndungu, wewe ulisoma shule fulani hapa jijini Dasalama!?" Naye akanitazama kwa umakini bila ya kupepesa macho kisha akanijibu "Ndio, nilisoma pale..."
"Ulimaliza mwaka gani?" Nikamuuliza kwa mashaka kidogo!
Akajibu, "Mwaka 1990. Vipi kwani?" Naye akaniuliza!
Nikamakwa, "1990? Ulikuwa kwenye darasa langu!" Nikatamka, na huku mshangao wangu nikiuonyesha wazi kabisa, kwa yeye kutonikumbuka.
Akanitazama kwa muda, kama vile haamini ninachosema... Kisha sasa, Hapo ndipo nilipochoka kabisa, yaani yule babu wa watu akaniuliza, kwa unyenyekevu kabisa, "Samahani, hivi wewe ulikuwa Mwalimu wangu wa somo gani!? Maana mpaka sasa sijakukumbuka bado..."
Nikataka kumjibu kuwa mimi ni Classmate wake, ila kuna kitu kikanizuiya, akili ikafanyakazi kwa haraka sana, nikajisemea kimoyomoyo...
"Mungu wangu! Kumbe Nimechakaa Zaidi Yake, Kiasi cha Yeye Kuhisi Kuwa Miye Nilikuwa Mwalimu Wake... Nikabakia Mdomo Wazi Ukitetema, Huku Kinywani Nikihisi Tewengu, Nadhani Nyongo Ilitema Ghafla!"

Hivi Mwaka Mpya Huwa Tunasheherekea Nini Haswa, Kuzeeka!? 

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!