Sunday, 8 January 2023
Wednesday, 4 January 2023
MBIOMBIO NIKAJIKUTA NALIKIMBILIA GARI LA KUZOA TAKA
Hivi Mwaka Mpya Huwa Tunasheherekea Nini Haswa, Kuzeeka!?
Saturday, 24 December 2022
WEWE UNGEFANYA NINI
NA UNGEJISIKIAJE!?

Hatoki Mtu Hapa... Mpaka Niupate...!
Sikukuu hii, nilipata mwaliko toka kwa sahibu yangu mmoja, hayati ya ujana wetu tulikuwa wanagenzi katika moja ya shule ya awali, jijini Dar, Gerezani, Kariakoo.
Sahibu yangu huyu imepita miaka mingi hatujaonana, kuonana kwetu ilikuwa kwa nasibu, wiki moja nyuma, nikiwa zangu kwenye harakati za hapa na pale, nikasikia sauti ya mtu anasalimia.
"Kakaa salamaa," akamalizia kwa kuniita jina langu... Kugeuka nakutana na sura ya mtu ninayo ijuwa, ijapo wajihi wake amebadirika, kiribatumbo cha haja, kama kabaila shamba. Lakini sura yake ingali ileile.
Tukasalimiana kwa bashasha, tukakumbushana mengi enzi tukiwa darasani, tukawakumbuka wanagenzi wenzetu waliokuwa watundu, na wale walimu visirani.
Tukaagana kwa yeye kunipa muhaliko, sikukuu hii, niende kwake kumtembelea, ili nami nipate nafasi ya kuiona familia yake, ana mke na watoto watatu.
Siku ikafika, nikachapa lapa, kiguu na njia, nikikatiza mitaa, ni mida ya adhuhuri, baada ya mshuko, jua si kali, ila fukuto la joto, lililotokana na wingu la mvua iliyogoma kunya, lilisababisha kero kidogo kwa wengi wetu tuliokuwa tukitembea kwa miguu, sako kwa bako kuelekea maeneo tofauti.
Baada ya kusubiri kwa dakika kadhaa kituo cha basi, nikapanda moja ya mabasi, maarufu kwa jina la Daladala, abiria ni wengi, siku kama hizi za sikukuu, wengi upendelea kwenda kwenye fukwe za bahari, kuvinjari, nadhani ndio sababu iliyopelekea wingi wa watu kwenye basi na haswa vichugandevu na watoto. Baada ya mwendo wa dakika zisizopungua 25, nikafika safari yangu.
Jamaa yangu ni mtu na familia yake, anaishi na mkewe na watoto zake kadhaa, pamoja na ndugu zake na wafanyakazi wa ndani.
Ma shaa Allah, nyumba yake nzuri, imezungushiwa ukuta mrefu wa futi saba na ushee, mbele kuna geti na kibaraza cha mlinzi. Nyumba imependeza na ina watu kiasi wasiopungua 8 kwa ujumla.
Rafiki yangu ni mtu mwenye uwezo wake kifedha nadhani kutokana na cheo chake serikalini...
Nimefika kwake nikakaribishwa vizuri kwa bashasha, baada ya salamu za hapa na pale, na mazungumzo haya na yale ya enzi tukiwa shule, huku tukijiburudisha kwa sharubati, nikaomba ruhusa niende msalani.
Uzuri wa hizi nyumba, vyoo, Maliwato na Mekoni ni humo humo ndani, wakati nipo msalani nikasikia sauti ya mkewe akilalamika kupotelewa kwa Mkufu Wake wa Dhahabu.
Sikujali sana, nikamaliza haja zangu, baada ya kujisafi, nikatoka zangu na kurudi varandani nilipokuwa nimeketi na mwenyeji wangu, nikawakuta wakazi wa nyumba ile wote wamekusanywa pamoja. Na mara mke wa sahibu yangu anawauliza kwa sauti alio wakusanya, nani kauchukua mkufu wake.
Kila mmoja anakataa, wanasema kuwa hawajui mahala wapi mkufu ulipo, naye bila ajizi akasema kwa ukali tena kwa sauti iliyobeba msisitizo wa herufi kubwa "HUMU NDANI HAKUJAWAHI KUPOTELEWA NA KITU HATA SIKU MOJA, MTANIELEZA LEO MKUFU WANGU HUPO WAPI! Na HATOKI MTU HAPA, MPAKA NIUPATE MKUFU WANGU!"
Nikaona baadhi ya macho yananitazama, ilihali mwenyewe najijua kuwa sina tabia za udokozi wala wivi...!
Nikajikuta nimepigwa na ganzi, mwili ukanisisimka kama mtu aliyeona mzimu wa mtu wa kale.
Nikawatazama na wao wakanitazama, nikamgeukia kumtazama mwenyeweji wangu, akakimbiza macho na kutazama pembeni, kukapita kimya cha sekunde kadhaa...
Nikajiuliza maswali mawazoni, nikakosa majibu, kisha nikakumbuka kuwa dunia ya leo, watu hawakosi majibu, Sasa Basi Kama Ndio Wewe Yamekukuta Haya, Ungefanya Nini?
Monday, 5 December 2022
NILIKWENDA KUNUNUA MWENYEWE DUKANI

Hivi Siku Hizi Bado Kuna Wanao Tafuna Tambuu!?

Hivi Siku Hizi Bado Kuna Wanao Tafuna Tambuu!?
Nipo Zangu Likizo, Ndani ya Jijila la Dar, Nakatiza Mitaa ya 'Uhindini' Karibu na Palipokuwa na Jumba la Sinema la Cameo, Lengo ni Kuelekea Walipokuwa Wakiishi Wakwe Zangu, Mtaa ya Kisutu.
Nikaikumbuka hii mitaa enzi hizo nikiishi mtaa wa Livingstone, walikuwa wakiuza sana Tambuu, ila ni ayami sasa sijaona 'Wahindi' wala 'Waswahili' wakitafuna Tambuu.
Zamani ukipita hii mitaa unakuta watu wanatafuna tu. Sasa usiombe jamaa awe anatafuna akiwa ghorofani halafu 'aipunguze' mdomoni wakati wewe unapita chini. Utasimulia.
Nikakumbuka kisa kilichonipata, miaka kadhaa nyuma. Nipo zangu nyumbani, mtaa wa Livingstone, Kariakoo. Miaka ile ya 80, bado kinda hata ubwabwa wa shingo bado kunitoka, sina hili wala lile. Hata sijui lile wazo lilikuja vipi, ila mpaka leo naamini kabisa, yaani haki ya Mungu tena, ndani ya mtima wangu kuwa; siku ile nilitembelewa na ibilisi wa Kibaniyani.
Tena atakuwa ni Mgujarati tu afiriti yule ayari, maana si kwa ushawishi ule ulionikamata, kiasi cha kushindwa kufikiria vizuri. Wala sikuwa na uraibu wa kula Tambuu, ila siku ile nilikamatika, nikajikuta nipo kiguu na njia kuelekea maeneo ya Kisutu, Uhindini.
Nikakatiza zangu Mnazi Mmoja, huyoo kiguu na njia, nikapita Mtaa wa Libya, mpaka makutano ya mtaa wa Libya na Zanaki, kisha nikachepuka kidogo kuingia mtaa wa Mtendeni, kisha nikaingia mtaa wa Mlima, kabla ya kukanyaga mtaa niliokusudia, mtaa wa Kisutu, dukani kwa Muhindi, Makaputura.
Ni baba wa Makamu, mnene haswa, kakaa dukani kwake, akipenda kuvaa kaputura akiishikiza kwa anjali, na ndio ikawa rakabu yake, Mzee/Babu Makaputura.
Duka limesheheni vitu kadhaa wa kadha, vimewekwa bila mpangilio maalum. Harufu ya Agarbatti inachomeka iliyowashwa mbele ya Ganesha na Lakshmiina, ina hanikiza kiasi cha kukera kwenye pua, harufu badala ya kuanisi ikawa inakera kiasi.
Akanitazama, bila ya kutabasamu, anafungua kinywa chake kunisemesha, huku nikishuhudia meno yake, yaliyobadirika rangi na kupata rangi ya Kahawia, iliyochanganyika na Chanikiwiti na mdomo wake uliojaa mate Mekundu kama damu kwa kula tambuu.
Kisha anatema mate mekundu yasiyopendeza, "Nini nataka veve", akaniuliza kwa rafidhi yake ya Kihindi, nami nikajikuta namjibu bila kufikiria, nataka tambuu, akanitazama kisha akaniuliza, "Nani Natuma veve tambuu" Kaka, nikamjibu, "Nambari gani iko nataka" nikamjibu, namba kumi na tatu, "Nambari Kumi na tatu, Taveja yeye" ndio babu, we nipe tu, ataiweza, nikamjibu. "Nataka gapi, bili, tatu inne" Moja tu inatosha.
"Haya subiri kidogo nategeza wewe, ile spesho kabisa, Tikee" uku akitingisha kichwa chake... Nikaitikia Tikee. Kulikuwa na majani ya Tambuu mezani, akachukua jani moja akalipangusa kidogo, kisha akaweka Popoo pamoja na chokaa kidogo juu ya jani la mtambuu, akaongeza na Tumbaku, Kungu Manga kidogo, Jagir gur na vikorokoro vingine wala sivikumbuki tena.
Akachana gazeti na kunifungia, "haya lete shiligi bili", nikampatia, kisha huyoo nikaongoza kurudi zangu, nyumbani. Nikapita mtaa wa Mrima, nikafungua kifurushi changu cha tambuu, nikabugia yote kinywani.
Sikumbuki kutema mate, kila yakijaa kinywani, nayameza kwa ule utamu wa ile sukari guru... Dakika si nyingi, nikaanza kuhisi Andasa ikipanda kidogo kidogo.
Afanaleki! Nikaanza kuhisi ubongo wangu haujatulia, harabu ya ile tambuu, yaani chugachugia, nilitia akili siku hiyo, dunia yote niliona kama inakwenda upande upande, nami nikaifatisha.
Kumbe walio niona siku ile wakastaajabu, wakapatwa na mpagao, mtu mfupi mie kwa jinsi nilivyokuwa nikitembea, kama mtu mwenye milonjo, maana si kwa miondoko ile ya mikogo.
Wakaja kuniuliza, siku ya pili yake, kumbe nilivyokuwa naangaika na andasi kichwani, na mwendo nikabadirisha, nikihisi barabara zimeinamia upande mmoja wa kushoto, nami ili nisidondoke nikajikuta natembea kuinamia upande wa kuume, natembea kama mtu aliyepigwa dafurao na lori la Jay Fong la mwaka 74.
Nilikuwa natembea kama Kaa au Ngadu, yaani nikitembea upande upande, siku hiyo niliongea lugha zote za Kihindi, Kibengali, Kigujarati, Kitelugu, Kiurdu, mpaka Kibanyani nilikijua siku hiyo... Kudadeki.
Hata nyumbani sikumbuki nilifikaje, nilijikuta tu nimepitiliza mpaka uwani, huku nimeshika kibatari nilichokiwasha, tena ni saa kumi jioni, mie naona giza.
Siku hiyo nilitapika mpaka nyongo... Nikanyororeka kama Kinyonga aliyelishwa ugoro...
Kuanzia siku hiyo nilikoma, sikutia mdomoni si Tambuu wala Kubeli au nduguye Pariki...
Friday, 2 December 2022
NILISHIKWA KWA TUHUMA ZA KUSAFIRISHA MADAWA YA KULEVYA.
Nilipo Ruhusiwa tu, Breki ya Kwanza Ilikuwa Maliwatoni...
Nipo Ndani ya Ndege, Aina ya Airbus, Tumehabiri Watu Wengi Sana, Hii ni Moja Kati ya Ndege Kubwa Sana za Abiria, Ndege Inamilikiwa na Shirika la Ndege la Falme za Kiarabu la Imarati (Emirates).
Nikitokea zangu ughaibuni moja kati ya nchi za Ulaya, naelekea zangu Afrika Mashariki kwa likizo fupi.
Nitakaa Dubai kwa siku kama tatu hivi, kisha baada ya hapo nitaunganisha ndege kuelekea kwenye nchi ambayo ndio kuna kitovu changu.
Ndio kwanza nimemaliza kuweka mzigo wangu kwenye Saraka (Dambra) ya kwenye ndege.
Kitu ambacho binafsi sikipendi sana na hii ni kwa sababu ya kimo changu, maana mimi si mrefu wa sifa wala si mfupi wa kuchusha.
Ghafla nikashikwa bega la kushoto, mshiko ule uliandamana na sauti kavu kidogo, ya mwanamke wa Kiafrika, mtu mzima, amekonga kiasi chake, kwa haraka haraka, nikakadiria umri wake, anapata miaka 60 au 65 hivi. Na kwa ile rafudhi yake, nikahisi kuwa anatokea Afrika Magharibi, na kama sikosei atakuwa tu ni Mpopo na kama si Mnaijeria basi ni Mghana.
Akaniomba nimsaidie kuweka begi lake kwenye saraka, yaani sehemu ya juu ya kuhifadhia mizigo.
Lakini ghafla kabla sijainama kuchukua mzigo wa yule bibi, mtu mmoja mrefu kiasi aliyekaa karibu nasi akajitokeza na kumsaidia yule mama mtu mzima.
Kila mtu akakaa kwenye kiti chake, wakati tupo angani, yule bibi akaanzisha mazungumzo. Alikuwa ni mzungumzaji mzuri, mwenye kujua mengi.
Nami kama kawaida yangu, napenda mazungumzo na haswa ninapogundua ninaweza kuelimika kwa namna moja au nyingine.
Tuliongea wakati wote, kiasi cha kuifanya safari ya saa tisa ya kwenda Dubai kuhisi imekuwa fupi sana.
Mara, sauti ya rubani ikasikikia kupitia kipaza sauti akitangaza kwamba tumeingia kwenye anga ya Dubai na muda si mrefu ndege itatua kwenye kiwanja cha ndege cha Dubai.
Ghafla yule bibi ambaye amefanya urafiki nami akanza kulalamika maumivu ya tumbo.
Nami kwa uungwana niliokua nao nikiongozwa na moyo wangu uliojaa huruma kwa yule ajuza, nilibonyeza kitufe cha msaada, na muhudumu wa kwenye ndege akaja kutusikiliza, akataka kujua shida ni nini.
Nikamwambia kuwa jirani yangu hakuwa anajisikia vizuri.
Lakini cha ajabu yule bibi, ghafla alianza kuniita mimi kuwa ni kijana wake (My son, my son...), na uku akiwa amenikamata mkono, hakutaka kuniachia.
Msimamizi akaniambia kuwa hakuna kitu wangeweza kufanya zaidi ya kumpa dawa za kupunguza maumivu na tusubiri hadi tutakapotua.
Yule muhudumu akamtaarifu rubani, naye rubani akatangaza kwamba tumepatwa na dharura ya mgonwa ndani ya ndege na akatushauri sote tutulie na tusiwe na wasiwasi kwani yule mgonjwa atahudumiwa.
Yule bibi alikuwa akilia na kutokwa na jasho kama vile aliyemwagiwa ndoo nzima ya maji.
Nikajaribu kuuachanisha mkono wake na wangu, lakini yule bibi alikataa kuniachia mkono wangu... Kila mtu alidhani kuwa mimi na yule bibi wa Kipopo ni mtu na mwanae.
Ndege ilipokwisha tua na kusimama, yule kijana aliyesaidia kuweka mzigo wa yule bibi kwenye Saraka, aliondoa mzigo wake, kisha akasaidia tena kushusha sanduku la Bibi Mpopo na kuliweka kwenye kiti.
Yule jamaa kabla ya kuondoka alininong’oneza kwa kunishauri nijitenge mbali na huyu bibi na niwaambie wahudumu wa ndani ya ndege kuwa mimi na yule bibi hatukusafiri pamoja.
Wafanyikazi wa kwenye ndege waliniuliza kama tuna uhusiano na bibi yule, niliwaambia kuwa tumekutana kwenye ndege. Sikumjua kabisa kabla...
Wakati naondoka nikamuaga na kumtakia kila la kheri, lakini yule bibi aliniomba nimsaidie kumbebea mkoba wake.
Lakini yule jamaa aliyemsaidia kuuweka mzigo kwenye saraka ya kwenye ndege aliniangalia, tukatazamana machoni, nikamuona akitikisa kichwa kwa msisitizo. Nikamuelewa!
Tukawaachia wahudumu wamsaidie.
Basi mimi na abiria wengine tukatoka ndani ya ndege na kumwacha bibi wa Kipopo anasubiri kiti cha magurudumu.
Nashuru niliweza kujikongoa kutoka kwa yule bibi, baada ya waudumu kufika na kumsaidia mizigo yake na yeye akawekwa kwenye kiti cha matairi.
Tulipokuwa tukingoja mizigo yetu, tukasikia sauti kali ikiamuru "... Stop, Stop! You are Under Arrest...!"
Nageuka kuangalia kumbe anayeambiwa asimame na kuwa amewekwa chini ya ulinzi ni yule bibi wa Kipopo alikuwa akikimbia, akijaribu kuwatoroka Askari na wafanyakazi wa kwenye ndege.
Kumbe walipo mshusha tu, tumbo lilipona ghafla na mara moja na akasimama na kuanza kukimbia uku akimuachia mkoba mmoja wa wafanyakazi wa kwenye ndege, na kukimbia kuelekea nje...!
Kwa bahati nzuri polisi wa uwanja wa ndege walikuwa na kasi kuliko yeye. Walimshika na kumrudisha uku wamemvisha pingu za mikono.
Bibi wa Kipopo bila haya wala soni usoni akaanza kuniita tena... "My son... My son, ooh! How could you do this to me, ooh...!"
Mwanangu ... Mwanangu! Unawezaje kunifanyia hivi...!
Ndio sasa nikaelewa na fahamu kunirudia uzuri, kumbe bibi alikuwa amebeba dawa za kulevya na alikuwa akijaribu kunihusisha na mimi, ili yeye apate upenyo wa kutoroka!
Kwa bahati nzuri, yule bwana ambaye alikuwa amemsaidia kushusha mzigo wake toka kwenye saraka, alijitokeza na kuwaambia polisi wa uwanja wa ndege kuwa mimi na yeye (Bibi wa Kipopo) tumekutana tu kwenye ndege.
Polisi walichukua pasipoti yangu na kumwuliza yule bibi ataje majina yangu kamili ikiwa ni kweli mimi ni mwanae na tulikuwa tukisafiri pamoja.
Kwa neema ya Mungu, sikuwa nimemwambia hata jina langu la kwanza, bibi wa Kipopo akabakia tu anag’aa ng’aa macho! Uku akiendelea tu kusema "...he is my son, ...he is my son, ooh!"
Hata hivyo Polisi wakanitaka nifuatane nao kwenye chumba kidogo ambapo nilihojiwa sana.
"Nilikutana naye wapi? ...Nilipanda wapi...? Huyo bibi alipanda wapi...!?" Na maswali mengine mengi ya kimtego.
Na mizigo yangu yote ilipekuliwa na kuchambuliwa sana, wakachukua alama za vidole vyangu ili wakaangalie kama nilisha wahi kukamatwa...!
Taarifa za kipolisi zilipokuja, alama zangu za vidole hazikupatikana popote, si kwenye mizigo ya yule bibi wala kwenye kazidata za Kipolisi!
Niliruhusiwa kuondoa baada ya takribani saa tatu za mahojiano, maana hata mwenyeji wangu alisha anza kukata tamaa.
Hakuna siku nilijawa na hofu kama hii siku, na haswa kama ujazoea maswala ya kukamatwa na polisi, tena basi nikiwa nchi ngeni, nchi ambayo kesi za dawa za kulevya hukumu yake ni kifungo cha muda mrefu kama si cha maisha, kwa kweli nilichanganyikiwa...
Nilipo ruhusiwa tu, breki ya kwanza ilikuwa ni maliwatoni, uko niliharisha kweli kweli, nadhani ni ule woga na fikra zilizonizonga kuwa sasa ndio basi tena, naiwacha dunia kizembe...!
Tangia siku ile nikajifunza jambo moja, la kutogusa mzigo wa mtu yoyote yule. Labda mzigo uwe wa familia yangu na nimeupakia na kuufunga mwenyewe...
Zaidi ya hapo hata sijali, tena nimeapa kabisa, Haki ya Mungu tena, sikusaidii, nimekukuta uwanja wa ndege na mizigo yako hata ikiwa unayo mizigo iliyo kuelemea au umekongeka ukakongoroka utaibeba na kuishughulikia wewe mwenyewe.
Sitakupa hata toroli ya kuweka mzigo wako!
Mizigo yako... shida yako... Hiyo ndio sera yangu mpya safarini.
Na kama ni ndani ya ndege na ikiwa huwezi kuifikia sehemu ya kuwekea mizigo, kwenye saraka, na ikatokea kuwa mimi ndiye mtu wa karibu zaidi, nitakachoweza kukusaidia ni kukuambia umwite muhudumu wa kwenye ndege akusaidie...!
Maana Nazi Mbovu Harabu ya Nzima.
Nawatakia Wasafiri, Safari Njema...!
Tuesday, 29 November 2022
NILIKESHA NIKIMTAFUTA
Tukio Linalo Fanana na Ukweli!
Friday, 11 November 2022
BIRIKA BATI, KIKOMBE BATI,
NA HATUKUKOMA.

Hivi wakulaumiwa walikuwa watengenezaji au wanunuaji au watumiaji!?
Yaani hata sielewi, vikombe gani vinaunguza namna ile? Au walikuwa wanatukomesha tukivunja vikombe vya udongo!?
Halafu kikombe cha chai, ila kinapicha ya nyanya. Sikuvipenda, sivipendi, sitavipenda.
Na kwa nini nivipende, uwenda hivi vikombe ndio vimetukomaza midomo tukiwa bado makinda.
Nahisi ndio maana Watanzania tumekuwa watu wa kupiga sana stori... Sasa wewe fikiria chai ya moto, kuiwacha huwezi, hapo sasa ni stori tu, kumbe janja yako unavizia ipowe, hapo ni stori plus umbea na mikingamo.
Basi nikwambie, siku hiyo nikamtembelea binamu yangu wa kike maeneo ya Magomeni, nikitokea zangu maeneo ya Gerezani, Kariakoo, chini nimevalia viatu vyangu vya Kung Fu shuzi, medini Chaina. Shati langu la Juliana, picha ya ndege, kubwa kiasi na chini nimevalia suruali yangu ya kodrai.
Mtu mimi na ufupi huu, ukiniona kwa mbali, utafikiria nguo zatembea zenyewe. Huyoo kiguu na njia, nikakatiza zangu Jangwani, na jua lile la saa tisa alasili. Kufika home kwake, kanikaribisha uwani, nyumba nzima yupo peke yake, wapangaji wapo mitaani, awajarudi bado.
Kanikaribisha kwenye Kigoda, baada ya salamu na kujuliana hali akanikaribisha chai ya mkandaa, akanitilia kwenye kombe la bati, chai imekolea viungo, inawasha kwa karafuu na tangawizi, ikakolezwa na pilipili mtama, chai kama uji wa mgonjwa na mie ujanja ikawa ni kupiga stori za kupoza chai, fu fu fuuu, nyiingi!
Japo tupo uwani, lakini joto la saa tisa, jiji Dar nalo halikuniwacha, utafikiri nimemwagiwa maji, mara akanyanyuka na kuniita niende chumbani kwake...!
"Binamu njoo chumbani nikuonyeshe mambo, ila nakuonya usimwambie mtu..."
Ghafla nikajikuta nameza mate machungu, nahisi nilitaka kutema nyongo, ikaishia kohoni, chai kidogo inipalie, nilajikuta naimeza bila kujua kuwa naunguza kolomeo.
Nami bila ajizi nikajikuta nipo chumbani, hata sijui nimefikaje, maana fahamu zikikuwa zinaingia na kutoka...
Hakuna pa kukaa ila kwenye kitanda, mwenyewe katandika mashuka yake ya kufuma kwa mkono, maua ya rozi (mawaridi), kafanya seti kamili, mapazia ya dirishani na mlangoni. Vingine kafunikia radio yake, kaseti aina ya National na kitambaa kingine kakitandika kwenye meza.
Pembeni ya chumba kuna mtungi wa maji, umefunikwa na sahani ya bati na kata yake imewekwa pembeni kidogo, picha za wanamuziki wa Boney M na ABBA group zilizokatwa kutoka kwenye magazeti ya Sunday News zimebandikwa ukutani, pamoja na picha ya Buraku, kafanana na mwanamke wa Kihindi.
Kwenye meza kuna viboksi viwili vitupu vya sabauni ya Lux na lifebuoy pamoja na kibox cha dawa ya kusugulia meno ya Colgate. Pembeni kidogo, kuna kabati la vyombo lenye wavu, na kabati la nguo lenye kioo.
"Kaa basi hapo we nawe wima wima tu, kama mgambo wa site" sauti yake ikakatiza mawazo yangu yaliokwenda mbali ya hapo, maana mawazo yalikuwa mbingu ya sabaaa nacheka na kufurahi na malaika wa peponi.
Nikakaa kitandani, moyo unakwenda kasi kama wa Mbayuwayu... Akanitazama kisha akanambia, huku kaweka umakini usoni, yaani yupo siriasi kabisa... "binamu hii iwe siri yetu, ukimwambia mtu, mi na wewe basi tena sitakushirikisha kwenye mambo mazuri haya."
Nikahisi masikio ghafla yamenisimama wima kama mbwa wa msasi kaona windo, nikanyoosha na shingo kama Njiwa Manga...
Nikahitikia kwa kutingisha kichwa, akanambia "Apiya binamu, kuwa hutotoa siri, sema Hakiyamngu..." nikajikuta natamka, kwa kigugumizi, kilicho nikamata, hata kilipotokea sijui...
"Ha-ki ya M-ngu tttena, si-si-mwambii m-mtu mi mi-ye, Waalaahi Nakuapia, mmmh na mchanga huu naramba." Huku nikiinama na kwa kutumia kidole cha shahada, nikapangusa sakafu na kuramba...
Moyo ukaongeza kasi kama garimoshi la Mjerumani kwenye vita kuu ya kwanza ya dunia sanjari na tumbo likapata kusema, gruuuh.
Akanitazama kisha akanambia: "Haya mie nakuamini voo binamu yangu, najuwa we mambo yako ya kizungu, ndio mana nakupendaga..." Akatamka huku anaelekea kabatini kwake na kufungua kabati...
Hamadi, katoa doti tatu za vitenge vya wax na kuvirembea pale nilipo kaa, kitandani. Enzi hizo tukuvihita vitenge vya Burundi.
"Nimeletewa jana na shemejio..." Sauti yake ikaanikiza pale chumbani.
Nikamuuliza, Mmm! Shemeji yupi huyo...!? Yule mjeshi wa Ngerengere!?
Akanijibu: "Uwachi na wewe, wa Ngerengere wapi!? Yule nishamtosa siku nyingi... Huyu humjuhi wewe, mwenyewe anafanyakazi bandarini, hivyo vitenge vya Magamu (Magendo), vilikuwa vinapelekwa Burundi kontena nzima, yeye ndio kavinyakua hivi vitatu, kaniletea nimuuzie."
"Kimoja shilingi 25, ila kwa wewe binamu yangu, nitakuuzia kwa shilingi 22, na wewe ukauze upate faida japo kidogo."
Nikamtazama, kisha nikapiga fundo moja la chai ya moto, yaani hata sikuhisi kuunguzwa, hiyo midomo na koromeo nilikuja kuhisi nimebabuka, usiku wake nisharudi nyumbani.
Ghafla nikajihisi kama biskuti ndani ya chai ya moto au kiowevu, nikawaza mfukoni nina shilingi Moja ya Mwenge na sumni tu ile ya sungura...
Enewi, yalikuwa tu maisha yenye changamoto zake, furaha, uzuni, vicheko vyote vilikamilisha uhalisia wa maisha yetu, hatukuacha kutembeleana, japo bidhaa muhimu zilikuwa adimu... kula kwa kaya...
😉🤭🤣
Tuesday, 8 November 2022
LIKIZO YANGU, JIJINI DSM (DIZIM)

Na Kumbukumbu Iliyopotea
Nilipokuwa likizo jijini Dar es salaam, nikajikuta tu nimepata hamu ya katembelea kwa miguu, mitaa ya Gerezani, Kariakoo. Nikapitapita mitaa iliyosongamana watu wa kila aina, nikakumbuka kufuchama Rununu yangu, kwa kuchelea wivi, wasijeichukua bila ruhusa yangu, huku sauti za wabeba mizigo wakiyosayosa maneno ya kutiana nguvu, nikapishana na wenyeji wachache sana, wakihisabika kwa vidole vya mkono, wengi wao ni wageni.
Huyo nikayoyomeka zangu, nikajikuta natokea mtaa wa Nkrumah, taratibu nikashuka zangu mwelekeo wa Mnara wa saa, nikatupa macho upande wa kushoto nikasoma kibao, kilichofubaa kwa rangi baada ya kutelekezwa miaka dahari, neno NEW CHOX bado likisomeka, kumbukumbu ikarejea miaka mingi nyuma, nikatabasamu sanjari na kusikitika, maana umuhimu wa jengo hilo kwa sasa haupo tena, nani anakwenda sinema siku hizi!?
Hata ile hoteli ya Continental sina uhakika kama bado inatoa huduma, nakumbuka tulikuwa tukienda kucheza Disco na vijana wenzangu.
Nikakumbuka hata wale wakaazi wa vitongojini, nao hawakuachwa nyuma, serikali iliwafungulia vituo vya burudani vya kijamii, kwa wakazi wa jiji la Dar, watakuwa wanakumbuka majumba ya DDC, kama vile Amana Social Hall, DDC Kariakoo, Keko na pale Magomeni.
Pale Ilala awali ilikuwa pia ni mahali ambapo wengi wakienda kungalia sinema siku za mwisho wa wiki na siku za sikukuu. Kiufupi majumba haya ya jamii, yalikuwa nchi nzima.
Nikakumbuka kuna jumba moja lilikuja mwishoni, katika miaka ya 80, jumba ambalo ndio lilikuwa jumba lenye uwezo wa kuingiza watu wengi sana, likijulikana kwa jina la Star Light Cinema.
Kiukweli hii ni kumbukumbu nzuri na ya kuuzunisha, maana enzi hizo kweli ilikuwa jambo la tunu sana kwa mtoto au hata mtu mzima kupelekwa sinema.
Kwanza halikuwa jambo rahisi kwa mtu tu asiye na ubavu kupata tiketi, haswa filamu ikiwa ni mpya na waigizaji wakiwa ni maarufu.
Nakumbuka walanguzi wa tikiti za sinema, vijana kwa watu wazima, wenye nguvu zao, wengi wao weshatangulia mbele za haki, walikuwa wakimaliza kulangua pale New Chox sinema, walikuwa wakikimbilia Avalon sinema, alafu sasa pale kidirishani, tikiti zilikuwa zikiuzwa nusu, kisha zilizobakia wale Wahindi wakiwapa watu wao na kuziuza kwa bei ya juu.
Nikajikuta natabasamu, kumbukumbu iliyokuja baada ya hapo, nikatamani kucheka, maana siku hiyo pale Chox niliwahi kidirishani kabla ya dirisha la kununulia tikiti halijafunguliwa, nikajuwa leo napata tikiti tena zile siti za nyuma kabisa, kama si mstari A basi D.
Ghafla lango likafunguliwa kuruhusu watu waingie kununua tikikiti, sanjari na dirisha la kuuzia tikiti, hamadi nikajikuta hewani kama Sapatu, nimepigwa kibega kimoja tu, nikajikuta nimetupwa huko karibia na vyoo, chali kama mtoto wa Komba kaanguka mtini.
Nikajizoazoa zangu, nikabakia nimetumbua zangu macho kama mtu aliyekabwa na nguto, kumeza siwezi wala kutema ziwezi.
Enewei, pale jumba la sinema la Empire nako wakimaliza kuuza, walikuwa wakienda zao Empress, Ila jumba ambalo vijana wengi wakilipenda ni jumba la Empire kwa sababu walikuwa wakionyesha sinema nyingi za hollywood, na waendeshaji walikuwa na tabia ya kuongeza sauti haswa wakati wa mapigano, ili kuwakoleza watizamaji.
Majumba ya Cameo (Mtaa wa Jamhuri,) na Odeon (Mtaa wa Zaramo na Jamhuri) haswa yalikuwa maarufu kwa sinema za Kihindi, wakifuatiwa na New Chox Cinema (Mtaa wa Nkuruma) na Avalon (Mtaa wa Zanaki) na Empress (Mtaa wa Samora) alafu ndio Empire (Mtaa wa Azikiwe).
Kule Msasani, kulikuwa na jumba la sinema, likitwa Drive-Inn, wakiingia na magari yao, ila wakazi wa Msasani wengi walikuwa wakijazana nje ya ukuta na kutazama sinema, japokuwa hawakuweza kusikia sauti lakini wengi wakiridhika na hiyo hali.
Nakumbuka kumtembelea Marehemu, ndugu yake na baba, mitaa ya Msasani, sasa ndugu yangu mmoja (yeye ni mkubwa kuliko mimi, naye pia ni marehemu), akanipa ofa bubu ya kwenda kutazama sinema, ah ah ah ah, akanipeleka Drive inn, kufika tukakaa nje ya ukuta na kununu zetu karanga na maji ya sharubati, tukatafuta tofali na box chakavu kisha tukaa kuangalia movie, tukisumbuliwa na mbu hapa na pale.
Sikumwambia kitu maana nilikuwa nikimuheshimu, mwenyewe nilishazoe kwenye majumba yetu ya kawaida, kama ukishindwa kununua tikiti basi unafanya kila njia kupenya au unampa pesa kidogo mwangalizi wa tikiti na kukuingiza ndani, ila kama jumba limejaa, basi unakaa kwenye ngazi za kutokea nje... Ah ah ah ah, ama kweli siku hazigandi.
Vijana wa leo wanaweza kushangaa wakisikia kuwa hata wimbo wa Taifa ulikuwa ukipigwa kabla ya onyesho, ila baadae sana ikaja kuondolewa kwa sababu ilisemekana kuwa hakukuwa na heshima, sababu wengine walikuwa ni walevi na hawakuwa wakisimama wima pale wimbo wa Taifa unapopigwa.
Hii biashara ya sinema ilikuja kuanza kudorora vilipoanza vituo vya Runinga na kushamili kwa biashara ya kuazimana kanda za video, na maktaba za kukodisha kanda za video, hizo zilikuwa enzi za Mzee Ruhsa.
Wengi walikuja kupendelea kukodisha kanda za video kuliko kwenda kwenye majumba ya sinema kwa sababu kwanza ilikuwa ghali kwa mtu mwenye familia, kugharamia watu zaidi ya wanne, pili filamu zenyewe nyingi zilikuwa baadae zikirudiwa rudiwa, nadhani shirika la filamu Tanzania lilikuja kufirisika na kushindwa tena kuagiza filamu mpya.
Haya majumba ya sinema, siku za mwisho mwisho walikuwa wakionyesha filamu mbili mpaka tatu kwa malipo ya kutazama filam moja, yaani ilikuwa ni kukesha, maana zilikuwa zikianza usiku.
Nakumbuka filam moja ya kihindi ilitamba sana katikati ya miaka ya 70 na mwanzoni mwa miaka ya 80, filam yenyewe ilitoka mwaka 1975. Ilitwa Sholay, hii filam Wahindi wa bongo walichapisha mpaka fulana zake na kuziuza!
Monday, 7 November 2022
WANAWAKE NA DAWA YA MAPENZI

Visa na Vituko Mitaani.
Wednesday, 5 October 2022
JIJI
LA DAR US SALAAMA
DAR ES SALAAM TANZANIA
Kabla ya mwaka 1868, Jiji
linalofahamika kwa jina la Dar es Salaam, halikuwepo kabisa. Badala yake
kulikuwa na mji ulioundwa na miji mitatu maarufu, ambayo ni Kunduchi, Mbwamaji
na Tindwa. Kila mji ulijitegemea, huku idadi ya wakazi wake wote kwa jumla
haikuzidi watu 2,000.
Kati ya miji hiyo mitatu, miji
miwili ya Kunduchi na Mbwamaji bado ipo hadi leo huku mji wa Tindwa, uliokuwa
na eneo kubwa zaidi, ulimezwa na nguvu za matukio ya kihistoria
yaliyosababishwa na mabadiliko na mpangilio mji mzima wa jiji.
Tukio kubwa la kihistoria
lililobadili mpangilio wa miji hiyo mitatu na kuzaliwa kwa Jiji ambalo leo hii
linalofahamika kama Dar es Salaam lilitokea mwaka 1865 pale Sultani Majid,
aliyekuwa mtawala wa Zanzibar, kununua eneo kubwa la ardhi ya mji wa Tindwa,
iliyomilikiwa na Sharif abdushakur Salim Al Attas na Jumbe Tambaza (machifu wa Kimashomvi), eneo
hilo lilianzia Bustani ya Mnazi Mmoja karibu na Mnara wa Saa (Clock Tower)
mpaka Magogoni (Ferri) mpaka kuelekea Daraja la Selender kutokezea Upanga
lilikuwa ni Shamba la Jumbe Tambaza.
Lengo la Sultani huyo la kununua
ardhi hiyo inayoanzia eneo la Magogoni hadi eneo la Hospitali ya Osheni Rodi
(Ocean Road), eneo ambalo lilikuwa pori linalotazama Bahari ya Hindi na ambalo
lilikuwa na ukimya, kiasi cha wakazi wa eneo la Tindwa kulipa jina la Mzizima,
kwa sababu kila aliyepita eneo hilo alihisi mwili wake kusisimka na kuzizima
kwa hofu ya kuwaogopa Wanyama pori.
Alinunua hilo eneo na kujenga
majengo makubwa kwa ajili ya kufungua chuo/shule ya kufundisha dini ya Kiislamu
kwa lengo la kueneza Uislamu kutokea hapo kuelekea maeneo mengine ya Mrima,
Pwani na Bara hadi Kongo na Burundi na kwa watu wa nchi za ukanda wa Afrika
Mashariki, Afrika ya Kusini na Afrika ya Kati.
Baada ya kununua eneo hilo, mwaka
1865 Sultani Majid aliingiza manuari kubwa za mizigo, zinazokadiriwa kuwa kati
ya tatu hadi saba, zikiwa zimesheheni vifaa vya ujenzi na wataalamu wa ujenzi
wa majengo ya chokaa na mawe, toka nchi za Bara Hindi na Uajemi. Na ndipo
ujenzi wa majengo hayo ulipoanza kwenye eneo hilo la Mzizima mkabala na pwani
ya Magogoni, huku majengo mengi yakijengwa eneo la Ocean Road.
Pamoja na Ikulu ile ya Magogoni,
Seyyid Majid pia alijenga lile jumba la ‘Ocean Road Cancer Institute’ (ORCI)
kwa sasa, ambalo mwanzoni lilikuwa ni Msikiti Mkubwa wa Ijumaa.
Ujenzi wa majengo hayo ulichukua
takribani miaka mitatu na kukamilika mwaka 1868 na Sultani Majid mwenyewe
alilipa jengo moja kubwa lilipo Magogoni hadi leo, jina la Dar us Salaama
(tamka Daru Salaam), maneno ya Kiarabu yenye maana ya Nyumba ya Utulivu au
Nyumba ya Amani. Na katika lango kuu pameandikwa maneno kutoka kwenye Qur’an
Suuratul Hijr Ayah ya 46 isemayo (ٱدْخُلُوهَا بِسَلَـٰمٍ ءَامِنِينَ)
Udkhuluuhaa Bisalaamin Aaminiin (Ingieni kwa salama na amani).
Wakoloni wa Kizungu walipokuja
Tanganyika, mahala hapo ambapo palikuwa ni Msikiti Mkubwa wa Ijumaa, pakafanywa
hospitali iliyojulikana kama ‘Ocean Road European Hospital’, iliyokuwa
ikiwatibia Wazungu peke yao.
Na ndio utaona vijana wengi jiji
la Dar es Salaam waliozaliwa baada ya uhuru kati ya miaka ya 60 - 70,
wamezaliwa kwenye hospitali ya Ocean Road, ambayo sasa ni maalum wa kutibu
saratani (Ocean Road Cancer Hospital), na kabla ya hapo yalikuwa ni majengo ya
msikiti na mabweni ya vijana na wazee waliokuja kusoma Dar Us Salaam na bado
mpaka leo muonekano wake ni ule ule.
Ikulu ile ya Magogoni wakati huo,
ilikuwa imezungukwa na misikiti kadhaa ambayo yote, katika Utawala wa
Kijarumani, ilibadilishwa matumizi na kufanywa taasisi nyengine.
Misikiti mingine iliyobaki
ikasambaratishwa na kutumiwa kwa shughuli nyengine, ukiwamo Msikiti mkubwa
uliokuwa baharini pale Forodhani, jijini Dar es Salaam, ulipogeuzwa kutoka
msikiti na kuwa Kanisa la Mtakatifu Joseph mpaka hivi leo.
Kuanzia hapo, wakazi wote wa miji
mitatu ya Kunduchi, Mbwamaji na Tindwa, wakabadili jina la Mji wa Tindwa na
kuubatiza jina la jumba hilo kubwa kuwa Dar us Salaama, jina ambalo baadae
lilimeza hata majina ya miji ya Kunduchi na Mbwamaji na kuifanya iwe vitongoji
tu katika mji wa Dar us Salaam.
Kwa takribani miaka kumi tangu
kufunguliwa kwa jengo hilo, raia toka nchi mbalimbali kuanzia Tanganyika,
Msumbiji, Zaire, Burundi, Rwanda, Kenya na Uganda, walimiminika katika jumba
hilo na kupata elimu ya Uislamu iliyotolewa na masheikh wakubwa toka nchi za
Uarabuni, Lamu na Mombasa Kenya na Zanzibar.
Kati ya mwaka 1875 na 1878,
Wajerumani walivamia Tanganyika na kuiweka katika himaya ya utawala wao, na
jengo hilo lilibadilishwa matumizi yake toka kuwa kitivo cha elimu ya Kiislamu
na kuwa makao makuu ya serikali ya Kijerumani na baadae kuwa makazi ya Mtawala
wa Kiingereza na leo hii ni Ikulu ya Taifa.
Mbali ya kubadilishwa jina kwa
jengo hilo, toka Dar ul Salaam na kuwa Ikulu, hata jina lilipewa mji wake
kutokana na jengo hilo pia limebadilishwa toka Dar us Salaama (Nyumba ya
Utulivu/Amani) na kuwa Dar es Salaam (Bandari ya Amani) ambayo wajuzi wa lugha
ya Kiarabu wanakata kuwa neno hilo Dar es Salaam halina maana ya Bandari ya
Salama.
NB:
Maelezo Kutoka kwa Mjuu wa Sharif Abdushakur Salim Al Attas
Sharif Abdushakur Salim Al Attas hakuuza eneo lake la Shamba lake tokea Clock Tower mpaka Magogoni, sababu Sharif Attas hakuwa na watoto zaidi ya mdogo wake sharif Omar Al attas aliezikwa uani ndani ya Msikiti wa Kitumbini, na sababu ya Wajerumani (Deutsch-Ostafrika) kupora Shamba la sharif abdushakur Salim, walisema Shamba la diwani wao ndio sababu wakapora na alieuza eneo ni Tambaza.
Tuesday, 27 September 2022
FAIDA YA KUNYONYESHA
KATIKA miaka ya sitini na sabini, serikali mbali mbali duniani
ziliwahamasisha kina mama kuacha kuwanyonyesha watoto wao maziwa ya mama. Na
badala yake watumie maziwa ya kopo.
Juhudi hizo zilizaa matunda yaliyokusudiwa. Yaani kina mama wengi
waliacha kuwanyonyesha watoto wao maziwa ya mama, na badala yake
waliwanyonyesha maziwa ya kopo (bottle feeding).
Hata hivyo teknolojia hiyo mpya ilileta maafa ya maelfu ya watoto
wadogo katika nchi mbali mbali. Hii ni kwa sababu, maziwa ya kopo hayana kinga,
yanagharama kubwa, yanahitaji muda wa kuyaanda na usafi wa hali ya juu. Pia
maziwa ya kopo hayana virutubisho vyote anavyovihitaji mtoto mchanga.
Baada ya maafa hayo, katika miaka ya hivi karibuni serikali kadhaa
duniani zimeanza kuwahimiza kinama kuirudia teknolojia asilia. Yaani kuwanyonyesha
watoto maziwa ya mama.
Hata hivyo, maisha yetu ya kila siku yanatuonyesha kwamba, kuna
kinamama kadhaa hasa katika mji ambao hawajawa tayari kuirejea teknolojia hiyo
ya asili, licha ya faida zake nyingi kama zinavyowekwa wazi sasa na elimu ya
sayansi.
Baadhi ya kina mama hao wasiotaka kuwanyonyesha watoto wao maziwa
ya mama wanaona jambo hilo ni kero na lina wanyima muda na uhuru wa ‘kustarehe’
(kwenda Bar, ufukweni, kwenye kumbi za muziki, kwenye makasino, kwenye pati,
n.k.
Pia wapo wale wanao ona kwamba ‘kero’ ya kunyonyesha maziwa ya
mama itawazeesha mapema na pia wataonekana kuwa hawaendi na wakati!
Kwa kuzingatia kasoro hiyo, iko haja kwa vyombo vya habari
kuongeza juhudi za kuwahamasisha kina mama na jamii kwa jumla ili kuirejea
teknolojia ya kuwanyonyesha watoto maziwa ya mama. Makala hii inalenga katika
azma hiyo. Kwa kuielimisha jamii faida zinazopatikana katika maziwa ya mama
yanapotumika kwa unyonyeshaji watoto wadogo.
Awali ya yote maziwa ya mama ni mlo kamili wenye mchanganyiko wa
virutubisho vyote inavyoweza kumpa mtoto afya kwa kipindi cha miezi minne ya
kwanza bila ya kuihitaji nyongeza ya chakula kingine.
Maziwa ya mama pia ni chakula na kinywaji kilicho safi na salama.
Vilevile maziwa ya mama yanakinga kwa mtoto na vilevile tayari muda wote.
Pamoja na faida hizo, maziwa ya mama yana gharama nafuu
yakilinganishwa na yale ya kopo. Vilevile maziwa ya mama hayachafui mazingira.
Kwa maneneo mengine maziwa ya kopo (makopo na mifuko iliyowekwa maziwa)
yanachafua mazingira.
Zaidi ya hayo, teknolojia ya kumnyonyesha mtoto maizwa ya mama
inaongeza mapenzi baina ya mtoto na mama. Pia utafiti wa kisayansi ulioripotiwa
hivi karibuni na jarida la American Academy of Pediatrics", umeonyesha
kwamba unyonyeshaji wa maziwa ya mama hasa kwa muda mrefu unaongeza uwezo wa
utambuzi kwa mtoto.
HAYATI ZA UJANA WETU
SIKU YA IDD
Baada
ya Mfungo Na Vile Vigoma vya Kula Daku, Jioni Tulielekea Viwanjani
Nimejikuta tu, Naandika, Kumbukumbu Chache Zilizobakia
Miaka ya 70 Mpaka 80.
Nakumbuka
Nilipokuwa Bado Kinda, Mwezi Kama Huu Ulioisha, Mwezi wa Ramadhani, Ilikuwa
Baada tu ya Kumaliza Kufuturu, Basi Wale Matineja, Walikuwa Wakipitapita
Majumbani Usiku Wakiimba na Wengine Hata Kucheza, Wakitumbuiza kwa Kupiga
Vigoma vya Kula Daku.
Kwa
Sie Tulikulia Dizim, yaani Dar Es Salaam Ilikuwa Jambo la Kawaida sana Kuwaona
Vijana Wadogo Mida ya Saa Mbili Mpaka Nne Usiku, Wakipita Majumbani na Vigoma
Vyao. Wakiwaimbia Watu Mitaani, "Kula Daku, Kula".
Wakati
Mwingine Hata Vijana wa Makamo Pia Walitutumbuiza, Ila Hawa Ilikuwa ni Tofauti
Kidogo, Wao Walikuwa Wakipita Kuanzia Mida ya Saa Nne Usiku
Hizo
ni enzi ambayo Waislamu walikuwa na Imani, ilikuwa ikifika muda wa kufuturu,
basi utaona wakitandika Mikeka na Majamvi, nje ya majumba yao. Kiufupi Wanaume
Walikuwa Wakifuturu barazani, na kila mpita njia ukaribishwa, japo anywe nusu
kikombe cha uji, uji uliokolezwa pilipili Manga (Pilipili Mtama). Na wanawake
waliokuwa wakifuturu uwani. Kama ilikuwa ni nyumba yakupanga, basi wote wakaazi
wa hiyo nyumba ujumuika na kupata futari kwa pamoja, kila mmoja akileta futari
yake aliyopika siku hiyo.
Nimekumbuka
baadhi ya maneno ya nyimbo zilizokuwa zikiimbwa.
Muulizeni
mzungu alietoka angani bwana x2.
Babu
kaungua ndevu kwa uji wa ramazani bwanaa...
Kula
daku maneno yangu, kula eeh daku wee, daku kulaaa...
Huyu
na huyu kama mtu na nduguye bwana...
Nasema
huyu na huyu kama mtu na nduguye bwanaaa...
Ukiwaangalia
sana mapua kama nguruwe bwana...
Kula
daku maneno yangu, kula eeh daku eeh, daku kulaaa...
Kwa
wale tineja, wakimaliza kuburudisha aidha wapewe pesa kidogo, Kuanzia senti 10,
20 au senti Hamsini, (Sumni), nyumba nyingine wakitoa Makoko na Matandu ya wali
na maisha yaliendelea kwa furaha na amani tele.
Utoto
ule waliweza kuaminiana, senti kidogo zilizokusanywa, masiku ya Ramadhani,
waligawana siku ya sikukuu ya Idd Fitri, hazikuwa pesa nyingi, kiasi cha
shilingi 10 au 15 au 20 kama mna bahati.
Ilikuwa
ikifika jioni kila mmoja alielekea kwenye viwanja vya sikukuu. Na wachache wetu
tulibahatika kununuliwa nguo mpya na viatu kwa ajili ya sikukuu.
Haikuwa
ajabu ukanunuliwa shati na suruali, ukakosa viatu, au ukanunuliwa viatu ukakosa
aidha suluwali au shati.
Tuliobahatika
tulipewa na pesa kidogo, nadra sana ukapewa shilingi tano, ni mwendo wa
shilingi kuja chini.
Sie
tuliolelewa kwenye vitongoji vya Kariakoo na Gerezani, Kisutu, Upanga, Ilala,
Magomeni na Buguruni kiwanja chetu Maarufu cha kushehereka, kilikuwa pale
Kidongo Chekundu (sasa ni Jakaya M. Kikwete Youth Park - JMK), kiwanja kilicho
kati ya mitaa ya Livingstone, Kiungani, Kisarawe na Lumumba, mbele ya shule ya
msingi Gerezani.
Hapo
Kidongo Chekundu, kulikuwa na Mabanda kadhaa wa kadha ya muda, yaliozungushiwa
magunia, mabanda maarufu yalikuwa yale ya vikaragosi, ngoma ya Nachi, (mfano
wa chakacha), mieleka na kadha wa kadha.
Nje
kulikuwa na uchezeshaji wa korokoro (Kamari) na michezo mingine ya kubahatisha.
Kulikuwa
na wachuuzi wa bidhaa wa kila aina, mihogo ya kukaanga na kuchoma, viazi vitamu
na mbatata vilivyopondwa na kuwekwa pilipili ya unga kwa juu, vikiliwa na
machicha ya nazi, mbwimbwi, ubuyu, juice za ukwaji, togwa, embe za kuchepa,
karanga shikirimu za vijiti na kadharika.
Sherehe
zilikuwa za siku tatu mfululizo, mabanda yakifunguliwa saa 10 jioni mpaka usiku
wa saa nne.
Sie
tulikuwa tukikaa karibu na viwanja, ilikuwa burudani tosha, kuona watu wa rika
mbalimbali, wakitoka vitongoji vya mbali wakijumuika pamoja wakubwa kwa wadogo,
kusheherekea sikukuu ya iddi.
Wengine
wetu tulikwenda kutazama sinema kwenye majumba ya kuonyeshea filamu.
Kwa
Dar es Salaam Kulikuwa New Chox, Odeon, Cameo, Avalon, Empress, Empire na
Drive-inn Cinema kule Msasani, ambayo unaingia na gari lako.
Enzi
hizo tulikuwa tukitumiana salamu kwa njia ya Redio, kulikuwa na watu maarufu wa
kutuma salamu, yaani karibia vipindi vyote hawakosi hao watu na mwisho wa
salamu unaandika ujumbe maalum, kama vile Salamu ni nusu ya kuonana n.k.
Ukibahatika,
basi waweza kukutana na gari la RTD, likipita mitaani, na kuwapa watu nafasi za
kutuma salamu zao za sikukuu, hapo utatakiwa utume salamu kwa watu watatu na
kisha utatakiwa uchaguwe wimbo wa kusindikiza salamu zako.
Kule
maeneo ya Posta ya zamani, pembeni ya jiji la Dizim, mkabala na shule ya
Forodhani, kulikuwa na eneo ambalo sasa nahisi kumegeuzwa kituo cha feri,
tukipaita Bombei. Hapo paliuzwa vitu vya Ubuge ubuge na ilikuwa kila Jumapili
utawakuta watu ufukwemi, wakipunga upepo uku wakiangalia Meli na Majahazi
yaliyotia nanga.
Kiza
kikiingia, wale vijana wadogo wadogo waliokwenda kwenye viwanja vya michezo,
wanajikusanya na kurudi majumbani mwao, kuanzia saa moja jioni.
Wale
wa nje ya mji, wanasogelea vituo vya mabasi ya UDA hapo utakutana na foleni
ndefu ya wasafi wakiwa kwenye foleni za kupanda mabasi. Hakukuwa na fujo za
kugombea mabasi kama hivi sasa, watu wakieshimiana na uku pembeni kuna mgambo akichunga
usalama wa abiria.
Ndani
ya basi hata kama umewahi kukalia kiti, kama kulikuwa na mzee au mama mjamzito,
basi alipishwa ili akalie siti ya basi. Ilikuwa kawaida kusikia mtu au watu
wakisema, "...Jama Hakuna Muislamu wa Kumpisha Huyo Mama Mjamzito siti!"