Monday 6 February 2023

 GANDA LA HARAGWE KWENYE JINO

Huku kazini, tulikuwa na mkutano wa kuongelea ufanisi utakaopelekea natija kwenye kazi zetu za Kila siku. Nilikuwa ni mtakadamu kwa siku ile, kwa wanao wasilisha mada...

Kabla sijaingia kwenye chumba Cha mkutano, nikapitia maliwatoni, nikachua na udhu Ili nipate faradhi kabla ya mkutano kuanza. Wakati najiangalia kwenye kioo nikipaka mafuta kupunguza ukavu wa ngozi na baridi, wakati nafanya mkaguo, tahamaki nakenua kinywa, nakutana na twasira ya Ganda la Haragwe limeganda kwenye jino.

Kumbukumbu zangu, zilichelewa kidogo kusajili tukio la mimi kula maharagwe. Ni baada ya sekunde kadhaa, nikakumbuka kuwa nilikula maharagwe na tambi, takriban siku tatu nyuma.

Lile ganda lilinitafakarisha sana, kwanza nashukuru nililiona mapema kabla ya mkutano, maana ningekuwa kituko cha siku kama si wiki nzima, Alhamdulillah tahayuri iliniepuka.

Fikiria mtu unaweza kula chapati na MAHARAGE majira ya asubuhi, ukasindikiza na chai vikombe kadhaa... Ukasukutua kinywa mara tatu...

Mchana ukala ugali na nyama, Ukasindikiza na maji ya matunda, Usiku ukala zako boflo na chai tu...

Kabla ya kwenda kulala, ukapiga mswaki, meno umeyasugua vizuri, bila kusahau ulimi, ukausugua mpaka kwenye koromeo, kisha ukasukutua tena na tena...!

Asubuhi, kabla ya kuwahi kazini unasafisha kinywa kwa kusugua meno vizuri na kusukutua mara tatu, unafika kazini, unacheka na jamaa zako, ghafla tu, wanaona Ganda la Harage kwenye Jino lako la mbele, tena harage lenyewe ni la juzi...!

Kwenye tafakuri yangu, nikagundua mfanano wa sisi viumbe binadamu na Ganda la Harage kuganda kwenye jino.

Na ndivyo binadamu tulivyo, waweza kutendewa wema, ihsani na kila zuri, lakini si sababu ya wewe kutosengenywa, wala si sababu ya wewe kutochukiwa, fanya ufanyalo, utaingia midomoni mwa waja kwa njia hisiyo pendeza kwenye masikio yako.

Ndio, Kuna Viumbe Hapa Duniani, Wapo Kama Ganda la Haragwe...!

Hakika tumefanikiwa katika ili la kutopendana na kuhishimiana, tumefanikiwa kueneza chuki miongoni mwa jamii zetu, si Waislam, si Wakristo, si Wapagani, na huko kwenye siasa za Kisekula ndio kabisa kumeoza, kiasi tumekuwa mbilikimo wa kifikra, tumefanikiwa katika kugawanyika miongoni mwetu na sasa tupo zaidi kimakundi, na wale ambao hawapo kwenye makundi au jumuiya yetu basi huyo si mwenzetu.

Tutamtia midomoni kwa maneno ya uongo na kashfa, mpaka apate shinikizo la moyo na jirani yake mapafu, kama si la figo na maini yake...

Tabia hizi kwa kweli zimemea kwenye nafsi zetu na zimendoa mafungamano ya kirafiki na kindugu na kusababisha majadiliano yetu hukosa busara na hikma kiasi cha kupelekea kwenye utengano na uhasama ambao tunaweza kuuepuka.

Mnisamehe tu, uzee huu, yote haya sababu majuzi nilikula maharagwe, ganda likabakia siku nne kinywani, kweli jitihada haishindi kudura, na takadiri huwezi epuka.

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!