Sunday 8 January 2023


WAZIMU WA MADEREVA WA BODABODA

Hivi Waendesha Pikipiki Maarufu kwa Jina la Bodaboda, Bongo zao ni Zile za Zinjanthropus!?
Safari ya Kutoka Kariakoo Mpaka Sinza, Kwa Siku Moja tu, Nilishuhudia Ajali Saba za Bodaboda. 

Nilipopata likizo yangu ya mwaka, nikafunga safari kwenda Bongo, baada ya kuondoka takriban miaka na miezi kadhaa, kwa kweli nilikuwa na hamu kubwa sana ya kukutana na ndugu, jamaa, marafiki na majirani zangu. Na haswa ukizingania ni miaka imepita na uku hamu yangu kubwa kuona jinsi gani usafiri wa Bodaboda na Bajaj ulivyo shamiri jijini Dar.

Mengi nilisimuliwa kuhusiana na madereva wa Bodaboda na jinsi wanavyoendesha biashara zao, nami nikawa na hamu ya kulinganua na pia kushuhudia kwa macho ni kipi haswa kina ukweli katika hayo masimulizi.

Nakumbuka kuwa Pikipiki zilianza kutumika nchini Ujerumani katika karne ya 19. Ulikuwa usafiri uliokuwa mpya lakini ulirahisisha kuabirisha hasa ukikumbuka watu wa huko wakati huo wengi waliwatumia hayawani kwa ajili ya usafiri.

Huku kwetu enzi ya Mkoloni Muingereza ndio pikipiki zilianza kusambaa sana na kati ya pikipiki zilizopendwa zilikuwa za aina ya BSA kutoka Uingereza, pikipiki hizi zilipata jina kutoka kampuni iliyokuwa inazitengeneza iliyoitwa Birmingham Small Arms Company.

Baada ya Uhuru pikipiki za Honda, Suzuki kutoka Japan na Yamaha, zilipata umaarufu sana, pia kulikuwa na pikipiki aina ya VESPA toka India na BATAVUS za Mdachi nazo zilikuwa maarufu sana hapa nchini.

Umaarufu wa pikipiki ulipelekea serikali kuwapatia Makatibu Tarafa, Mabwana Shamba na watumishi wengi wa serikali pikipiki aina ya Honda 90 na baadae zikaletwa Honda 125. 

Pikipiki hizi zilikuwa ni imara kweli kweli, haswa Honda 90, maana zina uwezo hata wa kufungiwa jembe ulaya (plau) na ukalima kwa kutumia pikipiki.

Miaka yote hiyo waendesha pikipiki walikuwa watu wastaarabu walioheshimika na kuheshimu sheria za barabarani. 

Miaka hii michache zimeingia pikipiki za Kichina, ambazo zimezagaa kwenye biashara inayoitwa Bodaboda.

Waendesha bodaboda wamekuwa watu wa ajabu sana, ni watu wenye kudhani kuwa wao wana haki ya barabara na hata pembeni ya barabara kuliko mtu mwingine yoyote, na kuwa wao sheria za barabara haziwahusu.

Hawa ni watu wanaoamini kuwa ukipiga honi tu inatosha kuyafanya magari, majengo na hata miti kuhama na kuwapisha wao wanapotaka kupita. Kiukweli kwa siku chache nilizokaa likizoni, nilishuhudi mamia ya vijana wakijeruhiwa na wengine kufariki kwa ajaili za kizembe za kila siku za usafiri huu.

Mie naiomba serikali ifanye uchunguzi wa kina kabisa, hivi kwanini watu wakiendesha hizi pikipiki za Kichina akili zao zinahama? Kwanini hizi Pikipiki za Kichina zimewekwa nini mpaka Bongo za waendeshao hizi pikipiki zinakuwa kama za Zinjanthropus!

Mimi na mashaka na sponji inayotumiwa kwenye viti vya Bodaboda, inawezekana ina madini ambayo yakimuingia anae iendesha akili inahama.

Serikali ifanye uchunguzi wa wasiwasi wangu huu. Kwa kuwa sioni sababu kwanini waendeshaji wa zamani walikuwa hawapotezi akili, ila hawa wa Bodaboda akili zao, zinakuwa sio kabisa, hisije kuwa Wachina wana mpango wa kando kutupunguza, ili wahamie Afrika maana... Mmmh!

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!