Monday 22 August 2022

JASUSI ALIYEITUMIKIA NAFASI YAKE VEMA

Augustino Lyatonga Mrema 1944 - 2022

Augustino Lyatonga Mrema alizaliwa Desemba 31, 1944 katika kijiji cha Kilaracha huko Moshi vijijini mkoani Kilimanjaro, kaskazini Mashariki mwa Tanzania.

Alisoma shule ya msingi huko huko kijijini na baada mwaka 1968 alifanya mtihani wa sekondari kidato cha nne iliyoandaliwa na chuo kikuu cha Cambridge cha nchini Uingereza.

Mrema alianza kazi mwaka 1966-69 kama mwalimu akifundisha shule mbalimbali za mkoa wa Kilimajaro, ilopofika mwaka 1972 na 1973 aliteuliwa kuwa mratibu wa elimu wa Kata.

Mwanzoni mwa miaka ya 70 alijiunga kwenye mafunzo maalumu ya siasa na uongozi, kwenye chuo cha siasa cha Kivukoni jijini Dar es Salaam na alichaguliwa kuwa mwalimu wa siasa katika wilaya mbalimbali kwa niaba ya Chama cha Mapinduzi na baadae kwenye miaka ya 80 alipelekwa Bulgaria, huko alisoma masuhala ya sayansi ya Ustawi wa jamii na Utawala.

Na akaja kuchaguliwa kuwa Mwalimu wa Chuo kikuu cha usalama wa Taifa na mwaka 1982 hadi 1984 bwana Mrema aliteuliwa kuwa Kaimu mkuu wa usalama wa Taifa kwa mkoa wa Dodoma, mwaka 1983 hadi 1984 na baadae aliteuliwa tena kuwa Katibu wa Kikosi cha Ulinzi na Usalama makao makuu Dodoma.

Mrema alikuja na kuhamasisha kuanzishwa kwa vikundi vya ulinzi wa jadi, nje ya mikoa ya Shinyanga na Mwanza vilivyoundwa na wananchi, maarufu Sungunsungu.

Jina la Sungusungu pamoja na asili yake ni vikundi vyao lilitokea katika jamii za Wasukuma. Jina hilo la Sungusungu lilianza kupata umaarufu tangu miaka ya 1980 kati ya Wasukuma walioona matatizo ya wizi wa mifugo na ujambazi kwenye barabara baada ya vita vya Kagera na kurudi kwa wanajeshi wengi nchini kutoka Uganda.

Hata hivyo, vikundi hivyo vya sungusungu mara kadhaa vilishutumiwa kwa kutumia nguvu kupita kiasi na kujichukulia sheria mkononi kwa kuwatesa baadhi ya watuhumiwa wa uhalifu.

Mwanzoni mwa miaka ya 1990 mpaka 1994, kabla ya kupelekwa kwenye vyama vya siasa na kuwa mmoja wa wagombea wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, alikuwa waziri wa mambo ya ndani ya nchi katika serikali ya awamu ya pili ya Rais Ali Hassan Mwinyi.

Na baadae aliongezewa cheo cha Naibu waziri Mkuu cheo ambacho hata hivyo hakikuwepo kwenye Katiba ya nchi ili kumpa nguvu zaidi ya utendani.

Itakumbukwa pia mwaka huo wa 1992 kulipotokea fujo za kuvunja Mabucha ya kuuza Nyma ya Nguruwe na ndio mwaka ambao Augustine Mrema alikuwa Waziri wa Mambo ya Ndani na Makamu Waziri Mkuu.

Waislamu wataukumbuka mwaka 1992 kwamba siku hiyo waliyolazimika kuvunja baadhi ya mabucha ya Nguruwe, ilikuwa ni baada ya watoto wa Kiislamu kuhuziwa nyama ya Nguruwe kwa makusudi.

Hatua hiyo ilifikiwa baada ya Waislamu kutoa taarifa Serikalini, juu ya hatari na athari ya uwepo wa mabucha ya Nguruwe katika makazi ya imani za watu mchanganyiko, lakini Serikali ilipuuzia. Siku ambayo watoto wa Kiislamu walipouziwa nyama hiyo, iliwalazimu Waislamu kuvunja mabucha hayo.

Ndipo Rais Mwinyi kwa hofu akasema wale waliovunja mabucha ya nguruwe "nguvu za dola ziwaangukie" na ndipo Mrema akiwa ndio Waziri wa Mambo ya Ndani na Makamu Waziri Mkuu, akalitimiza hilo kwa vitendo.

Ilipofika mwaka 1994 alibadilishwa Wizara hiyo na kuhamishiwa katika Wizara ya Kazi, Maendeleo ya Vijana na Michezo, mabadiriko haya hayakumpendeza, ilimpelekea Mrema kuhamaki akidai mabadiliko hayo yalilenga kumnyamazisha asiendelee kupamba na rushwa na wizi wa mali ya umma, akitolea mfano wa dhahabu iliyokamatwa uwanja wa ndege wa Dar es Salaam lakini wahusika hawakuchukuliwa hatua yoyote.

Mwaka 1992, mwaka ambao utakumbukwa sana na wale wanaofuatilia siasa za vyama kisiasa, kwa sababu ndio mwaka ambao vyama vya siasa viliruhusiwa rasmi nchini Tanzania kutokana na shinikizo la nchi wahisani.

Hapo ndipo sasa serikali ya Tanzania, ilipoamua kuwapa ruhusa majasusi maalum waliokubuhu kwenye siasa kwenda kuanzisha vyama vya upinzani, hili ionekane kwamba nchi ya Tanzania ina vyama huru vya kisiasa.

Augustino Lyatonga Mrema kwenye macho ya raia alionekana kama ni mpiganaji wa kweli wa wananchi, akajiunga rasmi kwenye kambi ya upinzani, wakapatikana na wengine wengi tu kama kina Mabere Marando, Makongoro Nyerere, Doktari Masumbuko Lamwai, Edwin Mtei, gavana wa zamani wa benki kuu ya Tanzania na aliyekuwa naibu wake Mzee Bob Makani na hawa watatu yaani Edwin Mtei, Mzee Bob Makani na Brown Ngilulupi ndio waasisi wa CHADEMA.

Mrema alipojiunga na NCCR-Mageuz, mwaka 1995, alifanikwa sana kisiasa, maana alikoleza moto wa siasa, na alifanikiwa kuteuliwa kuwa mgombea wa urais kupitia chama hicho.

Katika uchaguzi huo, Mrema alikuwa mshindani wa karibu wa mgombea wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Benjamin William Mkapa, Mkapa alishinda uchaguzi huo wa Oktoba 29, kwa kunyakuwa asilimia 61.82 ya kura huku Mrema akiibuka wa pili kwa kupata asilimia 27.77 ya kura zote.

Umaarufu wake ilikiwezesha chama cha NCCCR- Mageuzi kunyakua viti 17 vya ubunge Tanzania Bara. Kwa kipimo cha wakati huo hii ilikuwa idadi kubwa ya viti vya ubunge kwa kuzingatia miaka mingi ya nchi kuwa katika mfumo wa chama kimoja.

Walikuwepo pia wabunge wa majimbo matatu ya Tanzania Bara: Karatu, Rombo na Kigoma Mjini kutoka CHADEMA, pamoja na wabunge zaidi ya 20 wa CUF kutoka Zanzibar.

Mara zote Mrema alikuwa akijinadi na kujenga wasifu wake juu ya uwezo wa ufuatiliaji wa kazi ikiwemo kuzuru maeneo tofauti kwa ghafla hata nyakati za usiku, na  kupambana na rushwa, ufisadi, magendo na ulanguzi wa mali.

Hata baada ya kushindwa urais, Mrema aliendelea na harakati za kuchaguliwa kwani Novemba 1996 alichaguliwa kuwa mbunge wa Temeke mkoni Dar es Salaam katika uchaguzi mdogo, baada ya Mahakama Kuu kutengua matokeo ya uchaguzi wa ubunge wa 1995 yaliyompa ushindi Ally Ramadhan Kihiyo wa CCM kwa sababu za udanganyifu.

Baadaye Mrema alikihama chama cha NCCR-Mageuzi na kujiunga na Tanzania Labour Party (TLP). Hatua hii ilikuwa baada ya mgogoro mkubwa wa kiuongozi ndani ya NCCR-Mageuzi kiasi cha kukiyumbisha chama na kukosa wabunge kwa muda mrefu.

Mrema Aligombea urais kupitia TLP mwaka 2000 na kushika nafasi ya tatu na mwaka 2005 alimaliza wa nne. Ni dhahiri kuwa matokeo hayo na idadi ya kura yalidhihirisha kushuka kwa umaarufu wake kisiasa.

Kwa takriban miaka 10 Mrema alikuwa Mwenyekiti wa bodi ya msamaha kwa wafungwa, maarufu bodi ya Parole, mara ya mwisho aliteuliwa na Rais John Magufuli mwaka 2020.

Buriani, Mwendo umeumaliza Mzee Augustino Lyatonga Mrema.

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!