Tuesday 27 September 2022

DUNIA INA MAMBO!

Miwezi kadhaa iliopita, nilipata likizo yangu ya mwaka, nikafunga safari kwenda zangu Bongo, Tanzania. Kwenye pirikapirika zangu nikamtembelea mmoja wa marafiki zangu, rafiki yangu huyu tulisoma wote shule ya sekondari, kati ya miaka ya 80. 

Rafiki yangu amepanga maeneo ya Banana, amepanga chumba kimoja (yeye mpaka leo bado mseja), vyumba vingine kuna wapangaji wengine. Kwenye maongezi akanisimulia vituko vinavyo msumbua hapo nyumbani kwake. Akasema ni siku 3 hajalala usiku kwa sababu anasikia nyayo za watu asiowaona wakitembea ndani ya chumba chake na nje ya dirisha.

Siku ya kwanza usiku wa saa nane, alihisi watu ndani ya chumba, alipovuta shuka na kudhani ni hisia tu! Akasikia nyayo za watu ndani, ndipo alipopiga kelele zilizoamsha wapangaji. Na kuamua kuingia kwenye dua na maombi, lakini hakurudi kulala kwa hofu na kukesha mpaka muda wa alfajiri wa kujiandaa kazini.

Kwa kitete siku iliyofuata akanywa dawa ya usingizi ili hasisikie chochote. Asalale! Haikuwa dawa ya kudumu, kwani aliamshwa kwa kuguswa kiunoni tena na mtu asiyemuona. Baada ya hapo akaanza kusikia kama mtu anamwaga michanga juu ya bati. Vibweka, vikahamia ndani sasa, kwa kusikia nyayo za watu wakizidi kutembea kama wanamiliki chumba.

Hivi karibuni alinipigia simu kuwa kakimbia nyumba.

Kisa hicho kikanikumbusha mambo yaliyompata mmoja wa marafiki zangu wa mtandaoni, miaka ya nyuma alipokuwa anasoma Mtwara-Masasi girls alikuwa akisikia nyayo za watu ndani ya bweni lao, wakitembea usiku wa manane ilhali kila mwanafunzi alikuwa amelala.

Siku ya kwanza alisikia sauti ya viatu vilivyotoa sauti ya 'Ko ko ko' akaamua kusoma dua na maombi. Ile anamaliza tu kufanya maombi (kusoma dua) akasikia vicheko, alipiga ukunga na kuhamia kitanda cha juu kwa mwezake. (Vitanda vya bweni nadhani mnavijua)

Vibweka havikuishia hapo, akawa anaogopa kabisa kulala peke yake. Akawa analala na rafiki yake.

Sasa siku moja alipolala na rafiki yake kulipopambazuka alfajiri, rafiki yake alimwamsha akaoge. Lakini, yeye akuamka na kumwambia kuwa hataamka muda huo, amwache mpaka baadae kidogo.

Yule Rafiki yake akaenda kuoga na kumuacha akiendelea kulala. Aliporudi akamwamsha na kusema, "Lily umeoga na kurudi kulala tena?"

Lily akashtuka lakini akahisi amesikia vibaya.

Akamjibu, "Mimi sijaoga bwana. Umenibakishia maji?"

Yule Rafiki yake akazidi kusisitiza, "Lily utachelewa, amka ujiandae. Umeshaoga then urudi kulala kweli?" Ebu acha uvivu!

Pale sasa ndio mawenge ya usingizi yalipokata kabisa. Wakabishana huku Lily akizidi kusisitiza kukataa kwamba ajaoga.

Rafiki yake akasema, "Lilian nilikuomba mpaka sabuni lakini hukunijibu wala kunitazama."

Lily kufikia hapo akwa hana budi kwenda kuoga huku akitetemeka kwa hofu. Alipokuwa anarudi kutoka kuoga kuna mwanafunzi mwezake akamuuliza, "Lily una maji mengi enhee..."

Kipindi kile maji yalikuwa yanapatikana kwa shida, na walikuwa wanayachota kwenye kisima kwa ugumu sana. Hivyo  basi, ndoo moja ya lita kumi unaweza kuoga siku 2 au 3: sasa Lily akawa anajiuliza angewenzaje kuoga mara mbili?

Alipomuliza kwa nini anasema vile, yule mwanafunzi mwenzake akasema kwa sababu amemuona ameoga mara ya pili. Kidogo amwamini rafiki yake, kwa sababu walikuwa wanaoga nje wakiwa wamejipanga kwa mstari hivyo ilikuwa ni rahisi kuonana nani kaoga nani hajaoga.

Lily alianza kushikwa na hofu kupita kipimo baada ya wote kuungana na kusisitza alioga na walimuona.

Yule rafiki yake naye alipoona vituko vikimfuata naye akamkimbia kwa hofu na kwenda kulala bweni lingine. Akabaki peke yake.

Akabaki akijiuliza maswali ambayo hata wewe utakuwa unajiuliza. Huenda utakuwa na majibu nayo, lakini upande wake mpaka leo ajawahi kupata majibu.

 

Na siku aliporudi likizo, ndio hakurudi tena kwenye ile shule! 

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!