Tuesday, 20 September 2022

MPANGO KINA WA MIAKA 5 YA KUREKEBISHA VIJANA - Panya Road

An Extensive 5 Year Reforms Program for The Youth - Panya Road

  • Hata Wafungwa Wanaweza Kufaidika Kwenye Programu Hii.
  • Tuwatumie Panya Road, Kuimarisha Uchumi kwa Kutoa Mafunzo ya Uzalishaji, Ufundi na Kazi za Amali, Mila na Utamaduni na Uzalendo.

Haya Matukio ya Panya Road, yananikumbusha tukio moja lililonitokea miaka mingi nyuma, zaidi ya miaka 40 hivi. Nakumbuka kushuhudia jamaa ninaye mfahamu, akikimbizwa na umati watu, wakimtuhumu kukwapua pochi ya mama mmoja, huku wakipiga kelele za mwizi.

Yule kijana alinipita mbio na huku akivua shati lake na kuingia kwenye jalala la taka, na kujifanya kichaa huku akigaagalika kwenye taka. Halafu aliniambia, “wakija waambie mwizi amepita.” Anamaliza kusema tu, waliokuwa wakimfukuza walifika pale, wakitweta.

Kuna waliokuwa na mawe na vipande vya tofali, wengine mapanga, marungu na silaha nyingine. Nilijua yule kijana alikuwa ni mwizi na miaka ile kulikuwa na vikundi vya vijana wahalifu wakisumbua sana watu kwa tabia zao za kukwapua kwapua watu.

Kidogo niwaambia wale watu, mwizi wao ndiye huyo hapo jaani. Lakini kitu fulani kiliniambia niache, sikumbuki kama ni woga au huruma tu iliyonijia, sikuwapenda wezi na pia sikupenda kuona wakiadhibiwa kwa kupigwa mawe au kuchomwa moto.

Walipo niuliza nikawaongopea huku nimejawa na hofu kwa mbali “Karuka huo ukuta, kadondokea upande wapili, kaacha shati lake hapa.”

Lile kundi hata sijui ilikuwaje, waliniamini, japo walikuwa na wasiwasi kidogo kwa yule kijana aliyepo jaani, lakini walinisikiza na kuamua kuondoka.

Yule kibaka, alinishukuru sana huku akinitaja kwa jina langu, kumwangalia vizuri kumbe tunafahamina, tukiishi mtaa mmoja, japo yeye alinizidi umri na hatukuwa marafiki, lakini kwa kule kutomchongea kwa wale watu, kulimfanya anione kuwa mimi ni jirani mwema.

Yule kijana alikuja kuhama, sijui walihamia wapi, ila ninachojuwa baba yake alikuwa ni mtumishi wa serikali, nadhani mzee wake alipata uhamisho mkoani.

Baada ya miaka isiyopungu ishrini, nilikuja kukutana na yule jamaa, mkoani Kigoma, keshakuwa mtu mzima, mwenye familia yake na uzuri zaidi ni mfanyabiashara mkubwa tu, akimiliki duka la spea za magari na boti za uvuvi.

Alinikumbuka nami nikamkumbuka, akanikaribisha nyumbani kwake, tukaongea mengi, akanambia kuwa hasingeweza kunisahau kwa sababu niliokoa maisha yake, na tangia siku ile aliyokimbizwa nami nikamsaidia ilikuwa kama ndio dawa, maana aliacha wizi, akajishughulisha na biashara na sasa anajitegemea na ana familia ya watoto wawili.

Lengo hapa si kuwahadithia tukio la kibaka mmoja aliyepata bahati ya kuokolewa miaka 40 nyuma, lahasha, ila nimekuwa najiuliza hivi awa vijana tunao waita Panya Road, ni kweli hatuna suluhisho la kudumu? Maana wengi wao ni vijana walio kati ya umri wa miaka 12 na 20 au 25 tu.

 

MPANGO WA KUWAWEZESHA PANYA ROAD

Binafsi natamani badala ya kuwafunga jela, tuwe na mipango maalum ya kuwarejesha Panya Road kutoka kwenye maisha ya kudhuru watu, uraibu wa dawa za kulevya na wizi na kuwageuza kuelekea kwenye maisha ya kawaida kupitia mafunzo maalum.

Kuwafundisha Panya Road kulihudumia Taifa lao na kuwatumia vijana hao katika kuwapatia mafunzo ya msingi ya kujiendeleza katika shughuli za kilimo, viwanda, uvuvi, ufundi na kazi za amali. Kuwafunza elimu ya uraia, Kuwafunza na kushiriki katika shughuli za maendeleo ya kijamii na utamaduni.

Mpango huu uwe wa miaka mitano (5), huu mpango utaratibu, kusimamia na kuendesha mafunzo endelevu hivyo basi kupitia mpango huu vijana hawa watajengeka kiuzalendo, wataweza kujitegemea na kujiamini.

Nakumbuka miaka ile kuanzia 1964 mpaka katikati ya miaka ya 70, serikali ya Tanzania ilikuwa mikakati ya kuwapeleka watu kwenye vijiji vya ujamaa.

Najua kuwa kulikuwa na matatizo ya kiutendaji, ndio maana jambo lile halikufanikiwa kama lilivyotarajiwa, lakini tunaweza kuchukua lile wazo kisha tukawashirikisha wasomi na wanaharakati wakalikarabati na kuliwasilisha tena, kisasa zaidi.

Kama vile serikali ilivyoanzisha JKT na baadae JKU kuwa ni vyombo vya kuelimisha na kuandaa vijana wa Kitanzania kiuzalendo, kimaadili, kinidhamu na kuwafanya raia wema wanaopenda kutumikia na kulinda nchi yao. Basi kwa nia ileile na uthubutu uleule, tunaweza kuanzisha "MPANGO KINA WA MIAKA 5 YA KUREKEBISHA VIJANA - PANYA ROAD" (AN EXTENSIVE 5 YEAR REFORMS PROGRAM FOR THE YOUTH - PANYA ROAD), kiufupi MKKV-Panya Road

 

WIZARA ZA SERIKALI ZITOE WATAALAMU.

Mpango huu wa miaka mitano, MKKV-Panya Road, unaweza kusimamiwa na wizara kadhaa, wakiongozwa na Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo n.k.

Kwenye hizo kambi za kudumu, vijana wapewe mafuzo ya Stadi za Maisha ya kujitegemea kinadharia na kivitendo, Kusoma, Kuandika, Kuhesabu na utoaji wa elimu ya Msingi na Sekondari kwa ujumla wake.

Programu hii ya MKKV-Panya Road, pia ijumlishe kuwaandaa awa vijana Kisaikolojia, Kuwapatia Elimu za Mafunzo ya Kilimo, Viwanda, Uvuvi, Mapishi, Elimu ya Uraia na Uzalendo, Ufugaji, Ujenzi, Ufundi wa aina mbalimbali kama vile Uashi, Useremala na Ukarabati wa magari, elimu za dini, utamaduni na michezo.

Vilevile kuwepo wataalamu wa saikolojia na ushauri nasaha watakao weza kuwashauri na kuwasaidia awa vijana katika masuala ambayo yamewafanya wawe na tabia mbaya, ili kuwasaidia kuepukana na kurejea tena kwenye maisha ya uhalifu. Na kuwabadirisha kuwa raia wema, wanaojiamini, wanaojituma, wenye uzalendo na kuipenda nchi yao.

Kwa kushiriki katika programu hii ya MKKV-Panya Road, vijana watapata fursa ya kupata ujuzi unaohitajika katika maisha yao na kuwa na ujasiri na ushindani kwa taaluma yao baada ya kuhitimu.

Mbali na ujuzi wa kujifunza ili kuwa na nguvu kitaaluma, vijana watajengeka kiuwezo na kujiamini na kuweza kuanzisha miradi yao wenyewe.

Vilevile itasaidia kuwabadirisha na kuwa raia wema, wanaojiamini, wanaojituma, wenye uzalendo na kuipenda nchi yao.


NB:

Kama kutakuwa na kesi ya mauwaji kwenye uhalifu wa hao vijana, basi Sheria ichukuwe mkondo wake.
Hili wazo ni kwa wale tu ambao hawana kesi za mauwaji.

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!