Tuesday 27 September 2022

 FAIDA YA KUNYONYESHA

KATIKA miaka ya sitini na sabini, serikali mbali mbali duniani ziliwahamasisha kina mama kuacha kuwanyonyesha watoto wao maziwa ya mama. Na badala yake watumie maziwa ya kopo.

Juhudi hizo zilizaa matunda yaliyokusudiwa. Yaani kina mama wengi waliacha kuwanyonyesha watoto wao maziwa ya mama, na badala yake waliwanyonyesha maziwa ya kopo (bottle feeding).

Hata hivyo teknolojia hiyo mpya ilileta maafa ya maelfu ya watoto wadogo katika nchi mbali mbali. Hii ni kwa sababu, maziwa ya kopo hayana kinga, yanagharama kubwa, yanahitaji muda wa kuyaanda na usafi wa hali ya juu. Pia maziwa ya kopo hayana virutubisho vyote anavyovihitaji mtoto mchanga.

Baada ya maafa hayo, katika miaka ya hivi karibuni serikali kadhaa duniani zimeanza kuwahimiza kinama kuirudia teknolojia asilia. Yaani kuwanyonyesha watoto maziwa ya mama.

Hata hivyo, maisha yetu ya kila siku yanatuonyesha kwamba, kuna kinamama kadhaa hasa katika mji ambao hawajawa tayari kuirejea teknolojia hiyo ya asili, licha ya faida zake nyingi kama zinavyowekwa wazi sasa na elimu ya sayansi.

Baadhi ya kina mama hao wasiotaka kuwanyonyesha watoto wao maziwa ya mama wanaona jambo hilo ni kero na lina wanyima muda na uhuru wa ‘kustarehe’ (kwenda Bar, ufukweni, kwenye kumbi za muziki, kwenye makasino, kwenye pati, n.k.

Pia wapo wale wanao ona kwamba ‘kero’ ya kunyonyesha maziwa ya mama itawazeesha mapema na pia wataonekana kuwa hawaendi na wakati!

Kwa kuzingatia kasoro hiyo, iko haja kwa vyombo vya habari kuongeza juhudi za kuwahamasisha kina mama na jamii kwa jumla ili kuirejea teknolojia ya kuwanyonyesha watoto maziwa ya mama. Makala hii inalenga katika azma hiyo. Kwa kuielimisha jamii faida zinazopatikana katika maziwa ya mama yanapotumika kwa unyonyeshaji watoto wadogo.

Awali ya yote maziwa ya mama ni mlo kamili wenye mchanganyiko wa virutubisho vyote inavyoweza kumpa mtoto afya kwa kipindi cha miezi minne ya kwanza bila ya kuihitaji nyongeza ya chakula kingine.

Maziwa ya mama pia ni chakula na kinywaji kilicho safi na salama. Vilevile maziwa ya mama yanakinga kwa mtoto na vilevile tayari muda wote.

Pamoja na faida hizo, maziwa ya mama yana gharama nafuu yakilinganishwa na yale ya kopo. Vilevile maziwa ya mama hayachafui mazingira. Kwa maneneo mengine maziwa ya kopo (makopo na mifuko iliyowekwa maziwa) yanachafua mazingira.

Zaidi ya hayo, teknolojia ya kumnyonyesha mtoto maizwa ya mama inaongeza mapenzi baina ya mtoto na mama. Pia utafiti wa kisayansi ulioripotiwa hivi karibuni na jarida la American Academy of Pediatrics", umeonyesha kwamba unyonyeshaji wa maziwa ya mama hasa kwa muda mrefu unaongeza uwezo wa utambuzi kwa mtoto.

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!