Tuesday 13 September 2022

RAIS WA KENYA AMEAPISHWA

  • Vituo vya Ndani vya Runinga Vyanyimwa Nafasi ya Kurusha Matangazo.
  • Hofu ya Bw. William Ruto Kulipa Kisasi Yaanza Kujionyesha

Rais, William Kipchirchir Samoei Arap Ruto ameapishwa kuwa rais wa tano wa Kenya siku ya Jumanne tarehe 13 Sept 2022, katika hafla iliyohudhuriwa na makumi ya viongozi na wanadiplomasia wa kimataifa.

Angani mwonzi wa jua ulikuwa umefichwa na Mavunde yakisindikizwa na mawaga na kusababisha kibaridi cha mzizimo.

Chini ya mawingu kulikuwa na tukio adhimu, Mubashara kwenye Kituo cha Michezo cha Kimataifa cha Moi, Kasarani. Mpaka kufikia saa tano asubuhi, Uwanja ulikuwa umejaa watu pomoni zaidi ya waudhuriaji 60,000 walihudhuria wakipeperusha bendera ya Kenya na kucheza kwa furaha huku wakiburudishwa na nyimbo kadhaa wa kadha.

Ulinzi ulikuwa mkali kuzunguka eneo hilo, huku vikosi vya usalama vikijaribu kuwazuia mamia ya watu waliojaa lango la uwanja huo. Takriban dazeni ya watu walijeruhiwa walipokuwa wakigombania kuingia kupitia moja ya lango la dharura.

Katika hali hisiyo ya kawaida na iliyozusha maswali mengi kwa wamiliki wa vituo vya Runinga nchini Kenya, ni pale walipozuiwa kurusha Mubashara hafla ya kuapishwa kwa rais mpya, hali iliyotafasiriwa kuwa ni kutishia kwa uhuru wa vyombo vya habari.

Timu ya mawasiliano ya Rais mteule wa Kenya William Ruto ilivizuia vyombo vya habari vya nchini humo kuripoti habari za kuapishwa kwa rais, na kutoa haki za kipekee za utangazaji kwa kampuni ya Multichoice Kenya Ltd, mshirika wa kikundi cha Runinga cha kulipia cha Afrika Kusini.

Waandishi wa habari kutoka magazeti ya ndani na vituo vya redio waliruhusiwa kuripoti mubashara.

Wakati wa kampeni, Bw Ruto aliwahi kuvishutumu mara kadhaa vyombo vya habari vya Kenya kuwa vinaupendeleo dhidi yake, na baadhi ya wachanganuzi wa siasa za Kenya wanasema kuwa uamuzi wake huo wa kupiga marufuku vituo vya Runinga vya ndani kurusha hafla hiyo ni kulipa kisasi kwa yale yaliyotokea wakati wa kampeni.

Mutuma Mathiu, mhariri mkuu wa Nation Media Group, ambayo anamiliki vyombo vya habari vya magazeti na Runinga, alisema katika mahojiano kwamba walikuwa na jukumu la kitaifa kuwatangazia Wakenya na kuhabarisha dunia kile kinachojiri, lakini wakajikuta wanapigwa dafrao na amri ya rais mpya.

Hata hivyo, alisema, “Sidhani kama tunataka kuanzisha vita vya kupakana matope kwenye arusi na kisha kuchafua vazi la bibi-arusi.”

Bw William Ruto alishinda katika kura ya Agosti 9 kwa tofauti ya kura chache sana dhidi ya mpinzani wake, Raila Odinga, ambaye alikataa matokeo na kuyapinga katika Mahakama ya Juu. Lakini mahakama iliidhinisha ushindi wa Bw Ruto katika uamuzi uliotolewa kwa kauli moja wiki moja iliyopita.

Bw. William Ruto, mwenye umri wa miaka 55, aliwahi kuwa makamu wa rais wa nchi hiyo kwa miaka 10 iliyopita, alizaliwa katika familia ya Kikristo katika kijiji kidogo cha Bonde la Ufa nchini Kenya, ambako alisaidia kazi ya ukulima ya kupanda mahindi na kwenda shuleni bila viatu. 

Alionyesha nia yake ya awali katika siasa katika miaka ya 1990, na kuwa mshirika mkubwa wa mtawala wa muda mrefu wa Kenya, Daniel arap Moi, alishinda nafasi katika Bunge na baadaye kuhudumu kama waziri wa kilimo na elimu ya juu.

Ongezeko la utajiri wa William Ruto ndani ya muongo mmoja umewastaajabisha watu wengi sana, Bw. William Ruto aliwahi kushtakiwa na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu ilipomshtaki kwa uhalifu dhidi ya binadamu, ikimtuhumu kwa kusaidia kupanga ghasia zilizofuatia uchaguzi wa 2007. Lakini Mahakama ilitupilia mbali kesi dhidi yake mwaka wa 2016, kwa vile serikali aliyohudumu kama makamu wa rais ilizuia ukusanyaji wa ushahidi na mashahidi wakaghairi.

Licha ya ukwasi wake wa kutatanisha, akiwa na himaya ya biashara inayojumuisha hoteli za kifahari , ranchi na kiwanda kikubwa cha kusindika kuku, Bw. Ruto alianzisha kampeni yake mwaka huu kwa wachuuzi wa Kenya, umati wa vijana na wanaojitahidi kujipatia riziki. Wakati wa kampeni, Bw. Ruto alizozana na Rais wake, Uhuru Kenyatta, ambaye alimuunga mokono mpinzani wa Bw. Ruto, Bw. Odinga, waziri mkuu wa zamani na kiongozi wa upinzani .

Bw. Kenyatta hakumpongeza Bw. Ruto hadi Jumatatu jioni, alipomkaribisha katika afisi ya rais, Bw Kenyatta alikuhudhuria hafla ya kumuapisha rais mpya na kushikana mikono, lakini Bw Odinga alisema kwenye ujumbe wake wa Twitter kwamba hatahudhuria.

Dennis Itumbi, msemaji wa Bw. Ruto, alihalalisha hatua hiyo kwa kusema Multichoice Kenya sio tu mwanakandarasi pekee wa kibinafsi bali KBC ni mmiliki wa hisa ndani ya kampuni ya Multichoice Kenya. Wanjohi Githae, kutoka kwenye timu ya mawasiliano ya Bw. Ruto, alisema katika ujumbe mfupi wa simu kwamba ingawa vyombo vya habari vya ndani ya nchi vinaweza kuleta magari yao ya utangazaji, ila hakuta kuwa na nafasi ya kuegesha magari yao mahali popote karibu na uwanja.

Siku ya Jumanne asubuhi, Bw. Mathiu wa Nation Media alisema kuwa baada ya mazungumzo na timu ya Bw. Ruto, waliruhusiwa kuwa na magari yao ya kurushia matangazo, lakini matukio yote yatachukuliwa na kituo cha MultiChoice na wao watarusha matangazo yatakayorushwa na kampuni ya MultiChoice.

Mkataba na kampuni hiyo haujawekwa wazi lakini Bw. Mathiu alisema alitarajia MultiChoice haitafanya hiyana dhidi ya vyombo vingine vya ndani, kurusha matangazo watakayorusha wao.

Wachanganuzi wa vyombo vya habari wanatumai hatua hiyo haitaanzisha enzi ambayo vyombo vya habari vitakwazikwa zaidi. 

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!