Tuesday 29 November 2022

NILIKESHA NIKIMTAFUTA
Tukio Linalo Fanana na Ukweli!

Alhamdulillah Ndio Neno Nitakalo Lirudisha Kwa Mola Wangu Siku Zote Katika Uhai Wangu Ila Sintoweza Kumsahau Binaadamu Kwa Ukatili Wake...!

Siku ya Jumanne majira ya saa mbili na nusu usiku nikiwa msikitini nikimalizia swala ya isha simu yangu ikiwa katika kimemeshi iliita mara nyingi sana, huwa sina kawaida ya kupaparika ninapokuwa mbele ya Mola wangu...!

Alhamdulillah baada ya swala nilitazama simu nakuona nimekosa miito kadhaa kutoka kwa dereva wa madrassa anae mchukua mtoto wangu na kumrudisha nyumbani siku za masomo... ilikuwa yapata saa tatu hivi usiku...!

Nilishtuka kidogo nakuhisi labda kuna tatizo barabarani nikampigia kwa haraka... Swali la kwanza alilo niuliza... Leo umekuja mwenyewe kumchukua mtoto wako madrassa...!?

Nikiwa katika mshituko nilimwambia siwezi kufanya hivyo bila kutoa taarifa... Basi sheikh tupo hapa karibu saa nzima mwanao hatumuoni, na hivi sasa ni saa tatu usiku...! (Kwa kawaida huwa wanatoka saa Mbili Usiku baada ya Swala ya Isha)

Niliharakisha kwenda nyumbani na kuchukua usafiri kwa haraka na kuelekea madrassa kwake maeneo ya karibu na Vijana Mwananyamala... Kufika nakuta waalimu na walezi wote katika taharuki na kusikitika...!

Nikiwa ni mzazi nilipiga moyo konde na kutaka kujua kulikoni, maelezo yalionyesha kuwa kuna magari binafsi yanayo kuja kuwafuata watoto na yale ya madrassa walio ingia mkataba. Hisia zikaja pengine kwa utoto atakuwa amepanda gari inayokwenda njia tofauti na nyumbani...!

Basi ikawa ni kutafuta namba za simu za wazazi kuwauliza watoto wao kama walikuwa na mwanangu kwenye magari yao na majibu yalirudi yale yale kuwa hapana hatukuwa nae...!

Hapo ilikuwa yapata saa nne na nusu usiku nikiwa katika kuomba dua na kumdhukuru Allah kila wasi wasi unapo itawala nafsi yangu...!

Baada ya hapo tukapata hisia pengine wakati wa kuruhusiwa yeye hakupanda gari yoyote badala yake amefuatana na watoto wanaoishi karibu, wale wanao kwenda kwa kutembea makwao hivyo akapoteza mwelekeo asijue anapo kwenda kwa udogo wake...!

Mimi na mwalimu wake tukaamua kuongozana pamoja na tulitembea mpaka kituo kidogo cha polisi Garden pale Mkwajuni na kuulizia kama wamepata taarifa yoyote ya mtoto aliyepotea jibu lilikuwa hapana. Na askari aliyepo zamu akatuambia kuwa taarifa ya kupotelea kwa mtoto inapaswa itolewe baada saa 24 tangia kupotea.

Subhanallah mtoto mwenyewe ndio kwanza ana miaka minne, nikiwa katika mawazo masaa 24 kwa mtoto wa miaka minne, nikachoka kabisa. Nilicho amua kufanya ni kumwachia nambari zangu za simu askari wa zamu, ili kama kutakuja taarifa yoyote apate kunifahamisha.

Tukarudi madrassa na kuchukua usafiri na kuelekea kituo kingine kidogo cha polisi maeneo ya Mwinjuma ili kuwapa namba zangu kwa taarifa yoyote itakayo patikana.

Baada ya kutoka Mwinjuma, tukaamua kupita njia za ndani ndani huku nikitazama huku na kule, kila mtoto niliemuona, nilihisi anafanana na mwanangu, nasimama kuangalia kama ndie au lah.

Hatimae tukafika sehemu tukakuta mkusanyiko wa watu, nikiwa na ghamu nikawauliza nikiwa sina uhakika wa jibu nitakalopata.

Ajabu wakanambia kuna mtoto katangazwa kapotea yupo msikitni, kwa Makunganya...!

Tukatoka mbio mbio huku nimekunja kanzu yangu, makubazi mkononi kuelekea uko msikitini, uku nikiomba dua za kila aina nilizozikumbuka. Kufika tukafanikiwa kumuona kiongozi wa Msikiti, mtu wa makamu hivi, anafika miaka 50 kwa uchache, huku nikiwa na shauku ya taarifa ya mtoto wangu. Nikamuuliza kuhusiana na huyo mtoto alopotea.

Kiongozi yule akanijibu kuwa ni kweli kuna mtoto wa kike darasani la pili kapotea, umri wake unakadiriwa miaka nane mpaka kumi hivi.

Niliishiwa nguvu nakulazimika kuendelea na safari ya kurudi Mwinjuma...!

Tulipofika kituoni majibu niliyoyapata hapo ni yale yale tu, kuwa tusubiri saa 24 ndio tutoe taarifa rasmi ya kupotelewa na mtoto. Hivyo na hapo kituoni nikaacha namba zangu na kuelekea kituo kingine kidogo cha polisi pale Mtambani.

Baadaa ya kuzunguka vituo kadhaa vidogo vya polisi, vilivyo jirani nikakata shauri kwenda kituo kikubwa cha Oysterbay kutoa taarifa na kujua kama wana habari yoyote ya mtoto alopotea. Baada ya kumaliza maelezo yangu, askari alokuwa zamu akachukua Simu ya Upepo (Radio Call) ili kuwapa taarifa askari waliopo katika doria, kama watapata kumuona mtoto mwenye umri wa miaka minne akitangatanga mitaani wapate kumchukua na kumuifadhi.

Majibishano ya radio ya kituo na walioko doria yakanifahamisha kuwa, kuna operesheni maalum ilikuwa inafanyika usiku ule, na ili tatizo langu lishughulikiwe na askari walioko nje, itabidi kwanza wamalize operation zao kisha ndio watashughulika na tatizo langu.

Kwa kweli nilikuwa nimechanganyikiwa haswa, nikashindwa hata namna ya kufikiri. Ukizingatia kuwa muda umekwenda, kiasi ni saa tisa kasoro usiku.

Ghafla simu yangu ikawa inaita namba ilikuwa ngeni, baada ya kuipokea nikawa naiangalia kama vile kitu cha ajabu. Nataka kuipokea tu, ikakata.

Naangalia vizuri, betri ya simu inakaribia kumalizika, kiasi imebakiza asilimia 10% tu...!

Mara simu ikaita tena, nikaipokea kwa haraka sana na kuelekeza sikioni, kiasi nikajipiga na simu sikioni, na simu kuniponyoka, nikaiokota kwa haraka na kuilekeza sikioni tena, na kuita kwa sauti ya kitetemeshi.

Haloo, baba fulani hapa naongea, nikajitambulisha, sauti ya upande wa pili ikanitaka niende kituo cha Mwinjuma kuna taarifa muhimu inanihusu.

Moyo ukaongeza kasi mara dufu, kiasi cha pumzi kunipaa nikahisi kizunguzungu kwa mbaaali. Nikajikaza kiume nikamfahamisha askari wa pale Oyterbay kuwa nakwenda kituo kidogo pale Mwinjuma.

Baada ya kumwachia nambari zangu za simu, nilitoka mbio nikamsahau hata niliye enda naye pale kituoni, mbio mbio mpaka kituoni, Mwinjuma...!

Nimefika nikihema pumzi juu juu, kama Wibari alokoswakoswa na mbwa wa msasi , Alhamdulillah nilimkuta tayari mkuu wa madrassa na waalimu wengine nao wapo pale, baada ya kungojea kidogo askari wa zamu, aliniita na kuniambia niende upande wa pili. Nikakuta watu kama wa familia moja wanaume wawili na wanawake wawili mmoja kampakata mtoto, kumwangalia vizuri nakumuona mwanangu pembeni...!

Allah Akbar, hakika moyo wangu ulikuwa katika furaha na michirizi ya machozi katika mashavu yangu nikamnyakuwa mwanangu na kumkumbatia kwa furaha, uku namuuliza kwa upole.

Ulikuwa umeenda wapi Arhaan wangu...? Akanijibu kuwa alienda kutembea na rafiki yake...!

Nilitoa shukran zangu nyingi kwa hao wasamaria wema na kisha nikawauliza ni wapi walikompatia mtoto wangu?

Wakanambia wamemkuta sehemu inaitwa Mchangani mbali sana na madrassa kwake na walijaribu kupita nae katika madrassa nyingine kuuliza kama wanamjua walipo kosa ndio wakaamua kumleta kituoni hapo...!

Nikatoa pesa kiasi cha elfu kumi kumi mbili, ili niwape kama ahsante yangu kwao, uku nikiwaambia kuwa japo si hela nyingi, lakini niliomba wazipokee kama shukran na usumbufu walioupata.

Mmoja kati yao akanikatalia kata kata, na kunambia walicho kifanya ni wajibu wao kama wazazi, na tatizo halina mmoja, leo mimi kesho hata wao wanaweza kupata tatizo na wanatarajia wema kutoka kwa yeyote yule.

Uku machozi yakinilenga lenga, nikawashukuru sana watu wale, kisha nilimchukua binti yangu ili kurudi nae nyumbani.

Baada ya kupeana pole na waalimu wake waliohangaika kutembea mtaani usiku ule huku na kule kumtafuta hatimae tumefika nyumbani yapata saa kumi alfajiri, hoi bin taaban.

Baada ya kumuuogesha na kumpa chai tukiwa katika kumuhoji taratibu mimi na mama yake alisema kuwa alikuwa na rafiki yake anaitwa Mwajuma walitoka pamoja ni marika sawa ila huyo anaishi karibu sana na huwa anarudi kwao kwa kutembea tu.

Akaendelea kutufahamisha kuwa walipo fika kwa kina Mwajuma, waliingia ndani ila babake na Mwajuma akamwambia atoke arudi uko Madrassa.

Hebu fikiria ndugu yangu ni wazazi wa aina gani hao... Walioshindwa hata kumuuliza mtoto jina la mzazi au hata nambari za simu!?

Mbaya zaidi walipigiwa simu mwanzo kabisa, tulimpigia mama yake na Mwajuma, akawa hapokei simu, ikawa inaita tu, kisha tukampigia mumewe alipo pokea alisema kuwa hana taarifa yoyote ile kuhusu mtoto wangu.

Hakika binaadamu ni viumbe wa ajabu na katili waso na huruma, binafsi nimesamehe ila sinto sahau somo walilo nipatia usku ule...!

Nikiwa natafakari hali ya usiku ule, nikawa najiwazia tu, vipi kama angelikwenda kwenye barabara kubwa yenye magari mengi na ahadi ikatimia, si wangekuja kujuta au mioyo yao ishaingia kutu, kiasi hawana tena huruma kwa watoto wa wenzao?

Nikaamua tu kumshukuru MwenyeziMungu, mtoto wangu kapatikana salama usalmini...! Nikakatizwa na sauti ya Mwazini ikitukumbusha kuwa muda wa sala ya alfajir umetimu.

Nikanyanyuka zangu taratibu, kuelekea msikitini kutimiza wajibu wangu kwa Mola wangu...!

Alhamdulillah... Ndio neno langu la leo na mpaka kesho kwa Mola wangu...!

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!