Friday 2 December 2022

NILISHIKWA KWA TUHUMA ZA KUSAFIRISHA MADAWA YA KULEVYA.

Nilipo Ruhusiwa tu, Breki ya Kwanza Ilikuwa Maliwatoni...

Nipo Ndani ya Ndege, Aina ya Airbus, Tumehabiri Watu Wengi Sana, Hii ni Moja Kati ya Ndege Kubwa Sana za Abiria, Ndege Inamilikiwa na Shirika la Ndege la Falme za Kiarabu la Imarati (Emirates).

Nikitokea zangu ughaibuni moja kati ya nchi za Ulaya, naelekea zangu Afrika Mashariki kwa likizo fupi.

Nitakaa Dubai kwa siku kama tatu hivi, kisha baada ya hapo nitaunganisha ndege kuelekea kwenye nchi ambayo ndio kuna kitovu changu.

Ndio kwanza nimemaliza kuweka mzigo wangu kwenye Saraka (Dambra) ya kwenye ndege.

Kitu ambacho binafsi sikipendi sana na hii ni kwa sababu ya kimo changu, maana mimi si mrefu wa sifa wala si mfupi wa kuchusha.

Ghafla nikashikwa bega la kushoto, mshiko ule uliandamana na sauti kavu kidogo, ya mwanamke wa Kiafrika, mtu mzima, amekonga kiasi chake, kwa haraka haraka, nikakadiria umri wake, anapata miaka 60 au 65 hivi. Na kwa ile rafudhi yake, nikahisi kuwa anatokea Afrika Magharibi, na kama sikosei atakuwa tu ni Mpopo na kama si Mnaijeria basi ni Mghana.

Akaniomba nimsaidie kuweka begi lake kwenye saraka, yaani sehemu ya juu ya kuhifadhia mizigo.

Lakini ghafla kabla sijainama kuchukua mzigo wa yule bibi, mtu mmoja mrefu kiasi aliyekaa karibu nasi akajitokeza na kumsaidia yule mama mtu mzima.

Kila mtu akakaa kwenye kiti chake, wakati tupo angani, yule bibi akaanzisha mazungumzo. Alikuwa ni mzungumzaji mzuri, mwenye kujua mengi.

Nami kama kawaida yangu, napenda mazungumzo na haswa ninapogundua ninaweza kuelimika kwa namna moja au nyingine.

Tuliongea wakati wote, kiasi cha kuifanya safari ya saa tisa ya kwenda Dubai kuhisi imekuwa fupi sana.

Mara, sauti ya rubani ikasikikia kupitia kipaza sauti akitangaza kwamba tumeingia kwenye anga ya Dubai na muda si mrefu ndege itatua kwenye kiwanja cha ndege cha Dubai.

Ghafla yule bibi ambaye amefanya urafiki nami akanza kulalamika maumivu ya tumbo.

Nami kwa uungwana niliokua nao nikiongozwa na moyo wangu uliojaa huruma kwa yule ajuza, nilibonyeza kitufe cha msaada, na muhudumu wa kwenye ndege akaja kutusikiliza, akataka kujua shida ni nini.

Nikamwambia kuwa jirani yangu hakuwa anajisikia vizuri.

Lakini cha ajabu yule bibi, ghafla alianza kuniita mimi kuwa ni kijana wake (My son, my son...), na uku akiwa amenikamata mkono, hakutaka kuniachia.

Msimamizi akaniambia kuwa hakuna kitu wangeweza kufanya zaidi ya kumpa dawa za kupunguza maumivu na tusubiri hadi tutakapotua.

Yule muhudumu akamtaarifu rubani, naye rubani akatangaza kwamba tumepatwa na dharura ya mgonwa ndani ya ndege na akatushauri sote tutulie na tusiwe na wasiwasi kwani yule mgonjwa atahudumiwa.

Yule bibi alikuwa akilia na kutokwa na jasho kama vile aliyemwagiwa ndoo nzima ya maji.

Nikajaribu kuuachanisha mkono wake na wangu, lakini yule bibi alikataa kuniachia mkono wangu... Kila mtu alidhani kuwa mimi na yule bibi wa Kipopo ni mtu na mwanae.

Ndege ilipokwisha tua na kusimama, yule kijana aliyesaidia kuweka mzigo wa yule bibi kwenye Saraka, aliondoa mzigo wake, kisha akasaidia tena kushusha sanduku la Bibi Mpopo na kuliweka kwenye kiti.

Yule jamaa kabla ya kuondoka alininong’oneza kwa kunishauri nijitenge mbali na huyu bibi na niwaambie wahudumu wa ndani ya ndege kuwa mimi na yule bibi hatukusafiri pamoja.

Wafanyikazi wa kwenye ndege waliniuliza kama tuna uhusiano na bibi yule, niliwaambia kuwa tumekutana kwenye ndege. Sikumjua kabisa kabla...

Wakati naondoka nikamuaga na kumtakia kila la kheri, lakini yule bibi aliniomba nimsaidie kumbebea mkoba wake.

Lakini yule jamaa aliyemsaidia kuuweka mzigo kwenye saraka ya kwenye ndege aliniangalia, tukatazamana machoni, nikamuona akitikisa kichwa kwa msisitizo. Nikamuelewa!

Tukawaachia wahudumu wamsaidie.

Basi mimi na abiria wengine tukatoka ndani ya ndege na kumwacha bibi wa Kipopo anasubiri kiti cha magurudumu.

Nashuru niliweza kujikongoa kutoka kwa yule bibi, baada ya waudumu kufika na kumsaidia mizigo yake na yeye akawekwa kwenye kiti cha matairi.

Tulipokuwa tukingoja mizigo yetu, tukasikia sauti kali ikiamuru "... Stop, Stop! You are Under Arrest...!"

Nageuka kuangalia kumbe anayeambiwa asimame na kuwa amewekwa chini ya ulinzi ni yule bibi wa Kipopo alikuwa akikimbia, akijaribu kuwatoroka Askari na wafanyakazi wa kwenye ndege.

Kumbe walipo mshusha tu, tumbo lilipona ghafla na mara moja na akasimama na kuanza kukimbia uku akimuachia mkoba mmoja wa wafanyakazi wa kwenye ndege, na kukimbia kuelekea nje...!

Kwa bahati nzuri polisi wa uwanja wa ndege walikuwa na kasi kuliko yeye. Walimshika na kumrudisha uku wamemvisha pingu za mikono.

Bibi wa Kipopo bila haya wala soni usoni akaanza kuniita tena... "My son... My son, ooh! How could you do this to me, ooh...!"

Mwanangu ... Mwanangu! Unawezaje kunifanyia hivi...!

Ndio sasa nikaelewa na fahamu kunirudia uzuri, kumbe bibi alikuwa amebeba dawa za kulevya na alikuwa akijaribu kunihusisha na mimi, ili yeye apate upenyo wa kutoroka!

Kwa bahati nzuri, yule bwana ambaye alikuwa amemsaidia kushusha mzigo wake toka kwenye saraka, alijitokeza na kuwaambia polisi wa uwanja wa ndege kuwa mimi na yeye (Bibi wa Kipopo) tumekutana tu kwenye ndege.

Polisi walichukua pasipoti yangu na kumwuliza yule bibi ataje majina yangu kamili ikiwa ni kweli mimi ni mwanae na tulikuwa tukisafiri pamoja.

Kwa neema ya Mungu, sikuwa nimemwambia hata jina langu la kwanza, bibi wa Kipopo akabakia tu anag’aa ng’aa macho! Uku akiendelea tu kusema "...he is my son, ...he is my son, ooh!"

Hata hivyo Polisi wakanitaka nifuatane nao kwenye chumba kidogo ambapo nilihojiwa sana.

"Nilikutana naye wapi? ...Nilipanda wapi...? Huyo bibi alipanda wapi...!?" Na maswali mengine mengi ya kimtego.

Na mizigo yangu yote ilipekuliwa na kuchambuliwa sana, wakachukua alama za vidole vyangu ili wakaangalie kama nilisha wahi kukamatwa...!

Taarifa za kipolisi zilipokuja, alama zangu za vidole hazikupatikana popote, si kwenye mizigo ya yule bibi wala kwenye kazidata za Kipolisi!

Niliruhusiwa kuondoa baada ya takribani saa tatu za mahojiano, maana hata mwenyeji wangu alisha anza kukata tamaa.

Hakuna siku nilijawa na hofu kama hii siku, na haswa kama ujazoea maswala ya kukamatwa na polisi, tena basi nikiwa nchi ngeni, nchi ambayo kesi za dawa za kulevya hukumu yake ni kifungo cha muda mrefu kama si cha maisha, kwa kweli nilichanganyikiwa...

Nilipo ruhusiwa tu, breki ya kwanza ilikuwa ni maliwatoni, uko niliharisha kweli kweli, nadhani ni ule woga na fikra zilizonizonga kuwa sasa ndio basi tena, naiwacha dunia kizembe...!

Tangia siku ile nikajifunza jambo moja, la kutogusa mzigo wa mtu yoyote yule. Labda mzigo uwe wa familia yangu na nimeupakia na kuufunga mwenyewe... 

Zaidi ya hapo hata sijali, tena nimeapa kabisa, Haki ya Mungu tena, sikusaidii, nimekukuta uwanja wa ndege na mizigo yako hata ikiwa unayo mizigo iliyo kuelemea au umekongeka ukakongoroka utaibeba na kuishughulikia wewe mwenyewe.

Sitakupa hata toroli ya kuweka mzigo wako!

Mizigo yako... shida yako... Hiyo ndio sera yangu mpya safarini.

Na kama ni ndani ya ndege na ikiwa huwezi kuifikia sehemu ya kuwekea mizigo, kwenye saraka, na ikatokea kuwa mimi ndiye mtu wa karibu zaidi, nitakachoweza kukusaidia ni kukuambia umwite muhudumu wa kwenye ndege akusaidie...!

Maana Nazi Mbovu Harabu ya Nzima.

Nawatakia Wasafiri, Safari Njema...!

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!