Monday 7 November 2022

WANAWAKE NA DAWA YA MAPENZI

Visa na Vituko Mitaani.

Nakumbuka Mwishoni Mwishoni Mwa Miaka ile ya 1980, Nilibahatika Kutembelea Mkoa wa Tabora, Mara tu Nilipopata Likizo Yangu ya Mwaka.

Baada ya safari ya siku mbili kwa Garimoshi kutokea Dar es Salaam, hatimae tukawasili mjini Tabora mida ya jioni na nikapokelewa na mwenyeji wangu na kuelekea nyumbani kwake, maeneo ya Igurubi wilayani Igunga.

Nyumba ilikuwa kubwa na mmoja wa Wapangaji alikuwa ni Mjombaake na Mwenyeji wangu, ambaye alikuwa ni Mganga wa Kienyeji aliyekuwa amepanga uwani, na alikuwa kiasi maarufu sana haswa kwa kina mama wanaotafuta dawa za mapenzi na mazindiko mbalimbali.

Nakumbuka kuna kipindi alipata mteja, mama mmoja wa Kinyamwezi. Huyo mwanamke inavyo onyesha alikua akiangaika sana kwa waganga wa kienyeji kutafuta dawa ya mapenzi ili kumtuliza mume wake.

Mwenyewe anadai kuwa mume wake alikua ni mtu wa kubadilisha vimada (siu hizi mnaita michepuko) kila siku.

Siku moja shoga yake alimwambia kuwa kuna mganga mmoja uko maeneo ya Igurubi wilayani Igunga, aende uwenda akafanikiwa shida yake. Huyo mama alikuwa anaishi maeneo ya Kaloleli uko Sikonge.

Siku ikafika akaamua kwenda kwa huyo mganga, maana huyo mganga kama nilivyo eleza tukiishi nae nyumba moja.

Kama ilivyo ada kwa mganga ukosi neno wala ukosi dawa, mganga alimpa yule mama madawa ya kila aina bila mafanikio yoyote yale.

Siku zikapita mganga nae akaona sasa hii ni shida, akimwambia yule mwanamke kuwa ameshindwa ni kujidhalilisha na wateja wanaweza kumkimbia.

Mganga akawa anafikiria amwambie masharti yepi ili bibie ashindwe na asimsumbue tena kumtafutia madawa.

Siku alipokuja tena yule mganga akamwambia amletee Nyoka aina ya Koboko ili amtengenezee dawa. Kama mnavyojua Tabora nyoka ndio kwao na haswa hao Koboko ni hatari sana kwa sumu yao.

Yule mganga akiwa na hakika kabisa yule mwanamama hawezi kumkamata huyo nyoka mwenye sifa ya ukali wa sumu na wepesi wa kugonga watu.

Basi yule bibie akakubali sharti lile akaondoka zake na kuanza kuzungukia mashimo ya nyoka uko porini.

Shimo moja baada ya jingine, kichaka kwa kichaka na mwishowe alifanikiwa kumkamata Koboko kwa kumweka unga katika chungu. Na Koboko alipoingia tu ndani ya chungu alikifunika haraka sana, kisha huyoo na baskeli yake kumpelekea mganga yule nyoka.

Kufika kwa mganga, mganga hakuamini macho yake aliposikia kuwa kaletewa nyoka, alipofunua chungu tu, nyoka katoka kwa hasira, na mganga nae kuona nyoka anamfuata uku kavimbisha shingo yake kwa shari aliyokuwa nayo akageuka akatimka mbio uku akimtukana yule mama, akisema...!

"...kama umeweza kukamata Koboko, mumeo anakushindwaje...!?"

Sisi wengine mashahidi macho tukaanguka kwa vicheko, maana zile mbio ni hatari... Yule Mganga alirudi baada ya siku tatu...



0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!