Saturday 24 December 2022

 WEWE UNGEFANYA NINI

NA UNGEJISIKIAJE!?

Hatoki Mtu Hapa... Mpaka Niupate...!

Sikukuu hii, nilipata mwaliko toka kwa sahibu yangu mmoja, hayati ya ujana wetu tulikuwa wanagenzi katika moja ya shule ya awali, jijini Dar, Gerezani, Kariakoo.

Sahibu yangu huyu imepita miaka mingi hatujaonana, kuonana kwetu ilikuwa kwa nasibu, wiki moja nyuma, nikiwa zangu kwenye harakati za hapa na pale, nikasikia sauti ya mtu anasalimia.

"Kakaa salamaa," akamalizia kwa kuniita jina langu... Kugeuka nakutana na sura ya mtu ninayo ijuwa, ijapo wajihi wake amebadirika, kiribatumbo cha haja, kama kabaila shamba. Lakini sura yake ingali ileile.

Tukasalimiana kwa bashasha, tukakumbushana mengi enzi tukiwa darasani, tukawakumbuka wanagenzi wenzetu waliokuwa watundu, na wale walimu visirani.

Tukaagana kwa yeye kunipa muhaliko, sikukuu hii, niende kwake kumtembelea, ili nami nipate nafasi ya kuiona familia yake, ana mke na watoto watatu.

Siku ikafika, nikachapa lapa, kiguu na njia, nikikatiza mitaa, ni mida ya adhuhuri, baada ya mshuko, jua si kali, ila fukuto la joto, lililotokana na wingu la mvua iliyogoma kunya, lilisababisha kero kidogo kwa wengi wetu tuliokuwa tukitembea kwa miguu, sako kwa bako kuelekea maeneo tofauti.

Baada ya kusubiri kwa dakika kadhaa kituo cha basi, nikapanda moja ya mabasi, maarufu kwa jina la Daladala, abiria ni wengi, siku kama hizi za sikukuu, wengi upendelea kwenda kwenye fukwe za bahari, kuvinjari, nadhani ndio sababu iliyopelekea wingi wa watu kwenye basi na haswa vichugandevu na watoto. Baada ya mwendo wa dakika zisizopungua 25, nikafika safari yangu.

Jamaa yangu ni mtu na familia yake, anaishi na mkewe na watoto zake kadhaa, pamoja na ndugu zake na wafanyakazi wa ndani.

Ma shaa Allah, nyumba yake nzuri, imezungushiwa ukuta mrefu wa futi saba na ushee, mbele kuna geti na kibaraza cha mlinzi. Nyumba imependeza na ina watu kiasi wasiopungua 8 kwa ujumla.

Rafiki yangu ni mtu mwenye uwezo wake kifedha nadhani kutokana na cheo chake serikalini...

Nimefika kwake nikakaribishwa vizuri kwa bashasha, baada ya salamu za hapa na pale, na mazungumzo haya na yale ya enzi tukiwa shule, huku tukijiburudisha kwa sharubati, nikaomba ruhusa niende msalani.

Uzuri wa hizi nyumba, vyoo, Maliwato na Mekoni ni humo humo ndani, wakati nipo msalani nikasikia sauti ya mkewe akilalamika kupotelewa kwa Mkufu Wake wa Dhahabu.

Sikujali sana, nikamaliza haja zangu, baada ya kujisafi, nikatoka zangu na kurudi varandani nilipokuwa nimeketi na mwenyeji wangu, nikawakuta wakazi wa nyumba ile wote wamekusanywa pamoja. Na mara mke wa sahibu yangu anawauliza kwa sauti alio wakusanya, nani kauchukua mkufu wake.

Kila mmoja anakataa, wanasema kuwa hawajui mahala wapi mkufu ulipo, naye bila ajizi akasema kwa ukali tena kwa sauti iliyobeba msisitizo wa herufi kubwa "HUMU NDANI HAKUJAWAHI KUPOTELEWA NA KITU HATA SIKU MOJA, MTANIELEZA LEO MKUFU WANGU HUPO WAPI! Na HATOKI MTU HAPA, MPAKA NIUPATE MKUFU WANGU!"

Nikaona baadhi ya macho yananitazama, ilihali mwenyewe najijua kuwa sina tabia za udokozi wala wivi...!

Nikajikuta nimepigwa na ganzi, mwili ukanisisimka kama mtu aliyeona mzimu wa mtu wa kale.

Nikawatazama na wao wakanitazama, nikamgeukia kumtazama mwenyeweji wangu, akakimbiza macho na kutazama pembeni, kukapita kimya cha sekunde kadhaa...

Nikajiuliza maswali mawazoni, nikakosa majibu, kisha nikakumbuka kuwa dunia ya leo, watu hawakosi majibu, Sasa Basi Kama Ndio Wewe Yamekukuta Haya, Ungefanya Nini?

0 comments:

Post a Comment

Je Una Nasaha zozote Kuhusiana na Makala hii?

RAMADHAN KARIM

Read

Subscribe to RSS Feed Follow me on Twitter!